Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Furahia Wanyama Milele

Furahia Wanyama Milele

Furahia Wanyama Milele

KUNA wanyama wengi wa aina mbalimbali, na inaonekana kila mmoja ana tabia na sifa tofauti! Kuwapenda na kuwahurumia wanyama humfanya mtu amkaribie Muumba wao. Maria alijionea jambo hilo.

Karibu miaka mitatu iliyopita, wakati Maria alipoishi Lisbon, Ureno, mbwa wake kipenzi alipotea na kutangazwa kwenye redio. Shahidi mmoja wa Yehova alikuwa na uhakika kwamba alimwona mbwa kama yule aliyetajwa, basi akawasiliana na Maria. Walipokutana, walienda na kumpata mbwa. Shahidi huyo alimwambia Maria kwamba kwa kuwa anawapenda wanyama, atafurahia kuishi katika ulimwengu mpya ambao Mungu ameahidi. Alimweleza kwamba wakati huo wanadamu wataishi kwa amani na wanyama.

Maria alikubali mwaliko wa kuhudhuria mkutano wa Mashahidi. Mambo aliyosikia na kuona huko yalimchochea hivi kwamba akataka kujifunza Biblia. Funzo lilipoendelea, Maria alichochewa sana na yale aliyojifunza kumhusu Yehova Mungu na ahadi yake ya uzima wa milele katika ulimwengu mpya wenye uadilifu. (Zaburi 37:29; Yohana 17:3) Mwishowe alijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa katika Februari 16, 2002.

Kusudi la Mungu la Awali

Kama Maria, wengi wamefurahi kutambua kwamba kusudi la awali la Mungu la kwamba wanadamu waishi milele katika paradiso duniani na kuwatunza wanyama wote, litatimizwa hatimaye. (Mwanzo 1:28) Biblia inasema kwamba Mungu “hakuiumba [dunia] tu bila sababu,” lakini “aliiumba ili ikaliwe na watu.” Hivyo kulingana na ahadi ya Biblia, wanadamu walipaswa kufurahia dunia pamoja na wanyama milele.—Isaya 45:18.

Biblia pia inakazia kwamba Mungu anakusudia kutimiza kusudi lake la awali la kufanya dunia kuwa paradiso. Anasema hivi, “Mimi nimesema hilo,” na kuongezea, “pia nitalitenda.” Yehova anasema hivi: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu linalotoka katika kinywa changu. Halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”—Isaya 46:11; 55:11.

Ni wazi kwamba mwanzoni Mungu alikusudia wanadamu wafurahie paradiso duniani milele. Tuna hakika kabisa kwamba hatimaye kusudi hilo litatimia. Hebu tuchunguze jinsi Biblia inavyoelezea maisha katika ulimwengu mpya wa Mungu. Tutaona kwamba wanyama wote, wawe ni wa kufugwa au wa mwituni, wataishi kwa amani wao kwa wao na pamoja na wanadamu.—Isaya 65:17, 21-25; 2 Petro 3:13.

Wanyama-Vipenzi Katika Ulimwengu Mpya

Katika ulimwengu mpya wa Yehova, watu watagusa manyoya ya simba, wataipapasa ngozi ya simbamarara, na hata kulala msituni bila kuogopa kushambuliwa na wanyama. Ona ahadi hii ya Mungu: “Hakika mimi nitamkomesha katika nchi mnyama-mwitu mwenye kudhuru, nao [wanadamu] kwa kweli watakaa nyikani kwa usalama na kulala katika misitu.”—Ezekieli 34:25; Hosea 2:18.

Wakati huo wanyama wa mwituni watawatii hata watoto wachanga! Biblia inasema hivi: “Mbwa-mwitu kwa kweli atakaa pamoja na mwana-kondoo kwa muda fulani, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi, na ndama na mwana-simba mwenye manyoya shingoni na mnyama aliyelishwa vizuri wote pamoja; na mvulana mdogo atakuwa kiongozi juu yao.”

Lakini mambo bado! Andiko hilo linaendelea kusema hivi: “Ng’ombe na dubu watakula pamoja; watoto wao watalala pamoja. Na hata simba atakula majani kama ng’ombe. Na mtoto anayenyonya hakika atacheza juu ya shimo la nyoka; na mtoto aliyeachishwa kunyonya atatia mkono wake juu ya tundu la kupitishia nuru la nyoka mwenye sumu. Hawatasababisha madhara yoyote wala kusababisha uharibifu wowote katika mlima wangu wote mtakatifu; kwa maana dunia hakika itajawa na kumjua Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:6-9.

Katika ulimwengu mpya wa Yehova, hakutakuwa na tatizo la msongamano wa watu katika majiji makubwa ambayo hayawafai wanadamu na wanyama wao. Ni kweli kwamba hata leo watu wengi wanafurahia wanyama wao na wengi wana maoni yanayofaa kuwahusu na wanawatunza. Lakini hebu wazia taraja zuri la kufurahia wanyama-vipenzi milele katika ulimwengu mpya wenye uadilifu! Utunzaji bora watakaopata utamtukuza sana Muumba Mtukufu wa vitu vyote vilivyo hai.

Iwapo bado hujajifunza kuhusu mambo mazuri ambayo Mungu amekusudia—kama Maria alivyokuwa kabla ya kujifunza—tunakuomba kwa uchangamfu uwasiliane na wachapishaji wa gazeti hili au Shahidi wa Yehova ambaye atafurahia kukufundisha mambo hayo.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Katika ulimwengu mpya wa Mungu, watu watafurahia wanyama milele