Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ngono ya Simu Ina Ubaya Gani?

Ngono ya Simu Ina Ubaya Gani?

Vijana Huuliza . . .

Ngono ya Simu Ina Ubaya Gani?

KULINGANA na gazeti moja maarufu la Marekani, “wenzi ambao hawaishi pamoja wanapendelea ngono ya simu badala ya kuwasiliana kwa barua za mapenzi.”

Ngono ya simu ni nini? Inahusisha kuongea au kusikiliza habari za ngono kwenye simu. * Mara nyingi wale walio na mazoea hayo hupiga punyeto ili kutuliza hamu yao ya ngono. Iwe mazungumzo hayo machafu ni kati ya watu wanaochumbiana au wasiojuana, ngono ya simu inapendwa sana. Wengine hata wanaitetea hadharani.

Mwanamke mmoja anasema hivi: “Hiyo ndiyo ngono salama zaidi.” Inaonekana wengi wanakubaliana naye. Kwa mfano, katika Oktoba 2000, kikundi cha wataalamu wa afya wa Urusi walitumia matangazo ya biashara kwenye magazeti kuunga mkono ngono ya simu kwa sababu ya kuenea kwa virusi vya UKIMWI.

Hata hivyo, wengine wanaunga mkono ngono ya simu ili wapate pesa. Nchini Marekani pekee, huduma za ngono ya simu—ambazo huwawezesha watu kusikiliza mambo machafu wanapolipa pesa—ni biashara kubwa inayoleta mabilioni ya dola.

Kwa nini zoea hilo limependwa sana? Kitabu The Fantasy Factory, kinaeleza hivi: “Kukaribiana sana kimwili na kihisia ni hatari. Kuna hatari za magonjwa ya zinaa, uwezekano wa mtu kuharibu jina lake na kazi yake, kuogopa kushutumiwa na wengine, na matokeo ya tamaa ya ngono ‘zisizo za asili.’ Ngono ya simu hupunguza hatari hizo.”

Ni kweli kwamba ngono ya simu haihusishi uhusiano wa kimwili na mtu mwingine. Lakini je, hiyo inamaanisha kwamba haina ubaya au hatari zozote?

Je, Ngono ya Simu Ni Salama?

Tamaa ya ngono huwa yenye nguvu zaidi wakati wa ujana. Biblia inakiita kipindi hicho kuwa “upeo wa ujana,” wakati ambapo tamaa ya ngono ni yenye nguvu sana. (1 Wakorintho 7:36) Wakati huo muhimu maishani, kijana Mkristo anapaswa kujua jinsi ya “kukiweza chombo chake mwenyewe katika utakaso na heshima.” (1 Wathesalonike 4:4) Hiyo inamaanisha kwamba unapaswa kujua jinsi ya kushughulikia na kudhibiti hisia zako za ngono. Hilo ni muhimu ili uwe na maoni yanayofaa kuhusu ngono.

Hata hivyo, ngono ya simu humfanya mtu atake kutosheleza badala ya kudhibiti hamu yake ya ngono. Isitoshe, inamfanya mtu awe na maoni mabaya na yaliyopotoka kuhusu watu wa jinsia tofauti. Biblia inafundisha kwamba ngono inapaswa kufurahiwa na watu waliooana tu. (Waebrania 13:4) Lakini ngono ya simu huwachochea vijana wafurahie ngono nje ya ndoa. Biblia inasema kwamba furaha ya kweli huja kwa kutoa wala si kupokea. (Matendo 20:35) Lakini ngono ya simu humfundisha mtu kuwatumia wengine ili ajitosheleze mwenyewe. Biblia inawafundisha wenzi wa ndoa kusitawisha uhusiano wa karibu kwa kukuza upendo na kuaminiana. (Waefeso 5:22, 33) Hata hivyo, ngono ya simu haichangii uhusiano wa karibu wenye kufurahisha.

Zoea Hatari

Jiji la kale la Korintho lilijulikana kwa mazoea yake mapotovu. Hivyo, ilifaa mtume Paulo awaandikie Wakristo wa huko hivi: “Naogopa kwamba kwa njia fulani, kama nyoka alivyomshawishi Hawa kwa ujanja wake, huenda akili zenu zikaharibiwa kutoka kwenye unyoofu wa moyo na usafi wa kiadili ambao unamfaa Kristo.” (2 Wakorintho 11:3) Ngono ya simu ni njia moja ambayo Shetani Ibilisi anatumia kuwapotosha vijana leo.

Vijana wengine wameshindwa kuepuka kupiga simu za ngono. Kijana ambaye tutamwita Jim anaeleza jinsi inavyokuwa kwa wengine. Jim aliona namba ya huduma za ngono za simu katika tangazo la biashara. Alikariri namba hiyo na baadaye akaipiga kwa udadisi. Akapiga tena na tena. Muda si muda, alikuwa ametumia dola 600 kupiga simu!

Kuamsha hamu ya ngono ukiwa mseja hakupatani na shauri la Neno la Mungu. Linasema hivi: “Kwa hiyo, viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono.”—Wakolosai 3:5.

Hatari Wakati wa Uchumba

Vipi kuhusu watu wanaochumbiana? Bila shaka ni jambo la kawaida kwa watu wanaopendana kutaka kuonyeshana upendo. Katika nyakati za Biblia, msichana mmoja aliyemwogopa Mungu alisema hivi kuhusu mchumba wake: “Mimi ni wa mpenzi wangu, na tamaa yake imenielekea mimi.” (Wimbo wa Sulemani 7:10) Siku ya arusi inapokaribia, inafaa watu walioamua kuoana wazungumzie mambo fulani mazito. Hata hivyo, je, ngono ya simu ndiyo njia salama ya kuonyesha hisia za mahaba?

La. Hata wenzi ambao wameamua kufunga ndoa wanapaswa kufuata shauri hili la mtume Paulo: “Uasherati na ukosefu wa usafi wa kila namna au pupa visitajwe hata kidogo katikati yenu, kama inavyowafaa watu watakatifu; wala mwenendo wa aibu wala maneno ya kipumbavu wala mizaha michafu, mambo yasiyofaa, lakini badala ya hayo, utoaji wa shukrani. Kwa maana mnajua hili, nanyi mnalitambua wenyewe, kwamba hakuna mwasherati au mtu asiye safi au mtu mwenye pupa—maana yake ni kuwa mwabudu-sanamu aliye na urithi wowote katika ufalme wa Kristo na wa Mungu.”—Waefeso 5:3-5; Wakolosai 3:8.

Ni wazi kwamba mazungumzo ya kimahaba yaliyokusudiwa kuamsha mawazo yaliyopotoka au yanayomchochea mtu kupiga punyeto ni machafu machoni pa Yehova. Hata yanaweza kumfanya mtu avunje kanuni za Mungu. Kwa mfano, wenzi fulani walikuwa wanachumbiana wakiwa sehemu mbalimbali. Mwanzoni waliwasiliana kwa simu mara nyingi ili wajuane vizuri. Hata hivyo, baada ya muda mfupi, wakaanza kuzungumzia mambo machafu. Mazungumzo yao yakawa machafu zaidi na zaidi. Basi, si ajabu kwamba walipokutana hatimaye, walifanya mambo machafu.

Kwa kweli, sisi tunaotaka kumpendeza Mungu tutajitahidi sana kuepuka mtego wa ngono ya simu. Tunawezaje kufaulu?

‘Pigapiga Mwili Wako’

Mtu anaweza kuzoea ngono ya simu. Unahitaji ‘kuupigapiga mwili wako na kuuongoza kama mtumwa’ ili ukubaliwe na Yehova. (1 Wakorintho 9:27) Iwapo sasa unahusika katika ngono ya simu, tafuta msaada. Itafaa uanze kwa kuwaambia wazazi wako Wakristo. Ni kweli kwamba huenda wakakasirika. Lakini wao hasa ndio wanaoweza kukusaidia kudhibiti zoea lako ili usilirudie. Wazee katika kutaniko lenu la Mashahidi wa Yehova wako tayari na wanaweza kukusaidia.

Iwapo umefunga uchumba, jitahidi kubaki safi, hata unapozungumza kwenye simu. Mwanamke mmoja Mkristo anayeitwa Leticia, ambaye anakaribia kufunga ndoa, anasema hivi: “Mimi na mchumba wangu tumesoma makala zinazotegemea Biblia kuhusu kudumisha usafi wa kiadili. Zimetusaidia kudumisha dhamiri safi.” Mazungumzo yanapoanza kuwa machafu, usiogope kuyabadili. Zungumzieni umuhimu wa kuwa na maongezi yanayofaa.

Katika nchi fulani, matangazo ya biashara kuhusu ngono ya simu huonyeshwa kwenye televisheni usiku sana. Labda ingefaa kutotazama televisheni wakati huo. Kwa kuwa kupiga punyeto kunaweza kuamsha mawazo yaliyopotoka badala ya kuyafisha, ni muhimu kuepuka zoea hilo chafu. * Unaweza kufanikiwa kuondoa mawazo machafu akilini kwa kuzingatia mambo manyoofu. (Wafilipi 4:8) Shirikiana na marafiki wanaotumia usemi unaofaa na usome Neno la Mungu na vichapo vya Kikristo kila siku ili uimarishe azimio lako. Kwa kufanya hivyo, mawazo machafu hayataingia wala kuchafua akili yako. Zaidi ya yote, mwombe Mungu akusaidie. Mtume Petro aliandika hivi: ‘Tupeni mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.’—1 Petro 5:6, 7.

Msichana mmoja Mkristo huko Brazili anasema hivi: “Vijana wanashawishiwa sana kufanya ngono.” Hata hivyo, Yehova anajua magumu unayokabili. Uwe na hakika kwamba atakusaidia sana kubaki safi machoni pake.—Waefeso 6:14-18.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Zoea lingine lisilofaa kama hilo hufanywa kupitia mazungumzo ya ngono kwenye Internet.

^ fu. 24 Kwa madokezo juu ya kushinda zoea la kupiga punyeto, ona kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, ukurasa wa 198-211, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Ngono ya simu na mazungumzo machafu kwenye Internet yanazidi kupendwa

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Wachumba wanapaswa kujihadhari mazungumzo yao yasiwe machafu

[Picha katika ukurasa wa 22]

Kusoma Neno la Mungu na vichapo vya Kikristo kunaweza kukusaidia kudumisha usafi