Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wanyama Ni Zawadi Kutoka kwa Mungu

Wanyama Ni Zawadi Kutoka kwa Mungu

Wanyama Ni Zawadi Kutoka kwa Mungu

JE, UMEWAHI kutembelea bustani ya wanyama au kwenda kwenye sarakasi? Je, ulitamani kumshika au kumpapasa mnyama mzuri, kama vile simba au simbamarara mkubwa? Labda ulifurahia kumwona mtunzaji akiwashika. Miaka karibu 2,000 iliyopita, mwandishi mmoja wa Biblia alisema hivi: “Kila aina ya mnyama-mwitu na vilevile ndege na kitu kinachotambaa na kiumbe cha baharini ni vya kufugwa navyo vimefugwa na binadamu.”—Yakobo 3:7.

Wanyama wote wanafurahia kupendwa na kutunzwa. Unaweza kufurahia kuwaona wakichangamana na watunzaji wao. Mwandishi Mroma Pliny, aliyeandika karibu na wakati ambapo mwandishi wa Biblia Yakobo aliandika, alizungumzia ufugaji wa tembo, simba, simbamarara, tai, mamba, nyoka, na hata samaki.

Kwa kweli, watu walianza kufuga wanyama zamani sana. Muda mrefu kabla ya Yakobo na Pliny kuandika, Wamisri waliwafuga wanyama wa mwituni. Katika sehemu fulani leo, wanyama wengi wanaopatikana katika bustani za wanyama hufugwa nyumbani pia.

Jinsi Walivyoishi na Wanadamu Zamani

Biblia, ambacho ni kitabu cha zamani zaidi cha historia ya wanadamu, husema kwamba mtu wa kwanza, Adamu, aliwapa wanyama majina. Biblia inasema hivi: “Jina ambalo huyo mtu aliita kila nafsi hai, kila mmoja, hilo likawa jina lake. Basi huyo mtu alikuwa akiita majina wanyama wote wa kufugwa na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila mnyama wa mwituni.” (Mwanzo 2:19, 20) Yamkini Adamu aliwachunguza wanyama kwa makini sana ili awape majina yanayowafaa. Lakini hakuhitaji ulinzi, hata kutokana na wanyama wa mwituni. Aliishi kwa amani pamoja nao, na bila shaka alifurahia kuwa nao!

Mungu aliwapa Adamu na mke wake, Hawa, daraka la kuwatunza wanyama. Kupatana na kusudi la Mungu linaloonyeshwa katika Biblia, wanadamu walipaswa “watawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na wanyama wa kufugwa na dunia yote na kila mnyama anayetembea juu ya dunia.”—Mwanzo 1:26.

Uhusiano wa Karibu Wenye Kudumu

Watu wanapowaongoza wanyama vizuri, matokeo huwa mazuri. Mnyama anayependwa anaweza kuonwa kuwa rafiki anayethaminiwa, hata kuonwa kuwa mshiriki wa familia. Ilikuwa hivyo pia maelfu ya miaka iliyopita kama inavyoonyeshwa katika simulizi la Biblia kuhusu “mwana-kondoo jike mmoja, aliye mdogo” wa mtu mmoja maskini. Nabii Nathani alimweleza Mfalme Daudi jinsi mtu huyo maskini alivyomtunza mwana-kondoo aliposema: “Kondoo huyo alikuwa akila tonge lake, na kunywa kutoka katika kikombe chake, naye alikuwa akilala kifuani pake, na kondoo huyo akawa kama binti kwake.”2 Samweli 12:1-3.

Watu wengi leo wanaweza kuelewa jinsi mnyama anavyoweza kupendwa kama mshiriki wa familia. Fikiria familia moja inayoishi karibu na Harare, jiji kuu la Zimbabwe. Wazazi walimnunulia kila mmoja wa watoto wao mbwa. Mvulana wao mmoja mwenye umri wa miaka minane hivi alipokuwa akitembea na mbwa wake, kwa ghafula nyoka mkubwa mwenye sumu anayeitwa songwe alianguka mbele yake kutoka mtini. Nyoka huyo alimshambulia mtoto, lakini mbwa aliingilia kati upesi na kumwokoa. Je, unaweza kuwazia jinsi mbwa huyo alivyothaminiwa na familia hiyo?

Viziwi wanawathamini sana mbwa waliozoezwa kuwasaidia. Mwanamke mmoja anasimulia hivi: “Twinkie anaposikia kengele, yeye huja na kunigusa mguuni na kunipeleka kwenye mlango wa mbele. Anaposikia saa ya joko ikilia, Twinkie hunikimbilia, nami humfuata. Kukiwa na king’ora cha moshi au moto, Twinkie amezoezwa kunionya na kisha hulala chini kuonyesha kuna hatari.”

Kuna uhusiano wa pekee kati ya vipofu na mbwa wa kuwaelekeza. Mwandishi wa kitabu The Eyes That Lead, Michael Tucker ambaye huwazoeza mbwa, anasema kwamba mbwa aliyezoezwa kumwongoza kipofu anaweza kubadili kabisa maisha yake, na kumfanya “awe huru, ajitegemee, aweze kutembea, na awe na mwandamani.” Ama kweli, uhusiano mzuri kati ya mbwa hao na wenyewe ni jambo la kupendeza!

Hivyo ndivyo watu ambao wamelemaa katika njia nyinginezo huhisi pia kuhusu mbwa wao. Mwanamke mmoja anayelazimika kutumia kiti cha magurudumu, ana mbwa ambaye amezoezwa kuinua kipokezi cha simu na kuramba stempu za barua! Mbwa mwingine anajua amri 120, hata kuchukua mikebe na pakiti kutoka kwenye rafu za duka. Mwenye mbwa huyo ni mlemavu na hutumia kifaa cha leza kuonyesha bidhaa ambazo amechagua, na mbwa huyo humpelekea bidhaa hizo.

Wanyama-vipenzi huwafaidi wazee pia. Daktari wa wanyama alisema kwamba wanyama-vipenzi, kutia ndani mbwa, “huwasaidia wazee kuwa na kusudi maishani wakati huu ambapo jamii imewapuuza.” Gazeti The Toronto Star linaripoti hivi: “Wanyama-vipenzi huwasaidia watu wasifadhaike, wasiugue mara nyingi, na hata wapone baada ya kupatwa na mshtuko wa moyo.”

Kitabu The New Encyclopædia Britannica kinatoa maelezo haya ya kupendeza: “Kuwatunza wanyama-vipenzi hutoa fursa ya kuwafundisha watoto kwamba kuna faida kuchukua madaraka kwa uzito na pia kuwafundisha kuhusu ngono. Watoto huwaona wanyama hao wakijamiiana, na baadaye kupata mimba na matatizo mbalimbali wanayopata wakati wa kuzaa na kuwatunza watoto.”

Kuwapenda na Kuwatunza Wanyama-Vipenzi

Watu fulani huwapenda wanyama kuliko watu wa familia kwa sababu wanyama hao ni waaminifu sana. Katika kesi za talaka, wakati mwingine wanyama huonwa kuwa sehemu ya mali zinazogawanywa kati ya wenzi. Hata wengine wameandika katika wasia kwamba sehemu kubwa ya mali zao nyingi irithiwe na wanyama-vipenzi.

Basi haishangazi kwamba kuna biashara nyingi zinazohusiana na wanyama-vipenzi! Kuna vitabu na magazeti ambayo yanaeleza mambo mengi sana kuhusu wanyama-vipenzi. Wanapotambua kwamba watu wenye wanyama-vipenzi wako tayari kuwastarehesha wanyama wao kwa vitu vya bei ghali, wafanyabiashara huuza vitu mbalimbali vya wanyama.

Kwa mfano, kuna madaktari stadi wanaotibu magonjwa ya wanyama ya kila aina. Kuna madaktari wa akili wanaoweza kupendekeza dawa ya kumsaidia mnyama aliyeshuka moyo. Isitoshe, kuna mawakili, mawakala wa bima, na vilevile huduma za kuwasafisha na taasisi za kuwazoeza. Pia wanyama hao hufanyiwa mazishi. Vilevile kuna huduma za bei ghali za kuwazalisha wanyama kwa kutumia chembe za urithi!

Ni wazi kwamba wanyama wanapendwa sana. Katika kitabu chake The Animal Attraction, Dakt. Jonica Newby anasema hivi: “Mbwa anapotukimbilia akitikisa mkia wake na kuturamba kana kwamba kuja kwetu nyumbani ndilo jambo bora siku hiyo, unaweza kusema huo ni ‘upendo.’” Kwa hakika inaeleweka ni kwa nini watu wengi wenye wanyama-vipenzi huchochewa ‘kuwapenda’ wanyama wao pia.

Hata hivyo, kuwatendea wanyama kama wanadamu ni hatari. Hilo ni kweli kwa kuwa mnyama hawezi kumwandalia mtu mahitaji ambayo yanapaswa kuandaliwa na wanadamu. Isitoshe, kuwapatanisha wanyama-vipenzi na hali za jijini huwasababishia baadhi ya wanyama hao na wenyewe matatizo. Tutazungumzia mambo hayo katika makala inayofuata.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Wanyama wa mwituni wamefugwa tangu zamani

[Hisani]

A detail from The Great King of the Parthians Hunts With His Tame Panthers by Giovanni Stradanno: © Stapleton Collection/CORBIS

[Picha katika ukurasa wa 4]

Wachungaji Waisraeli waliwatunza kondoo kwa huruma sana

[Picha katika ukurasa wa 5]

Wanyama-vipenzi wanaweza kuwasaidia walemavu na wazee