Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni Kosa Kunywa Kupita Kiasi?

Je, Ni Kosa Kunywa Kupita Kiasi?

Maoni ya Biblia

Je, Ni Kosa Kunywa Kupita Kiasi?

KWA miaka mingi, wahusika wakuu kwenye sinema wamekuwa walevi wenye vichekesho. Ijapokuwa watu hao wanaigiza tu, vichekesho vyao vinaonyesha maoni yanayopingana ya watu wengi kuhusu kunywa kupita kiasi, yaani, ulevi ni udhaifu lakini hauna madhara yoyote.

Hata hivyo, ukweli kuhusu kunywa kupita kiasi si jambo la kuchekesha. Shirika la Afya Ulimwenguni linasema kwamba kunywa vileo kupita kiasi ni mojawapo ya hatari kubwa zaidi kwa afya ulimwenguni pote. Inasemekana kwamba mbali na uzoefu wa tumbaku, kunywa kileo kupita kiasi husababisha vifo na magonjwa mengi zaidi kuliko matumizi ya dawa nyingine za kulevya, na husababisha hasara ya dola zaidi ya bilioni 184 kila mwaka nchini Marekani.

Licha ya mambo hayo, watu wengi hawaoni ubaya kunywa kupita kiasi. Ijapokuwa wanajua hatari za kunywa kupita kiasi kwa muda mrefu, hawaoni ubaya kunywa kupita kiasi mara kwa mara. Vijana katika sehemu fulani za dunia huona kuwa wamekuwa watu wazima wanapolewa. Licha ya maonyo mengi ya mashirika ya afya, watu wengi zaidi wenye umri mbalimbali hata wanakunywa chupa tano au zaidi wakati mmoja. Si ajabu kwamba watu wengi wanajiuliza ikiwa ni vibaya kunywa kupita kiasi. Biblia inasema nini?

Divai na Kileo Ni Zawadi Kutoka kwa Mungu

Biblia hutaja divai na kileo mara nyingi. Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Nenda, ukale chakula chako kwa kushangilia na kunywa divai yako kwa moyo mchangamfu, kwa sababu tayari Mungu wa kweli amependezwa na kazi zako.” (Mhubiri 9:7) Mtunga-zaburi alisema kwamba Yehova Mungu ndiye anayeandaa “divai ambayo hufanya moyo wa mwanadamu anayeweza kufa ushangilie.” (Zaburi 104:14, 15) Ni wazi kwamba divai ni kati ya zawadi ambazo Yehova amewapa wanadamu.

Ni wazi kwamba Yesu alikubali matumizi ya divai. Muujiza wake wa kwanza ulihusisha kugeuza maji kuwa divai bora katika karamu ya harusi. (Yohana 2:3-10) Pia alitumia divai kuwa mfano wa damu yake alipoanzisha Mlo wa Jioni wa Bwana. (Mathayo 26:27-29) Biblia pia inataja kwamba divai ina faida za kiafya kwa kuwa mtume Paulo alimtia moyo Timotheo ‘atumie divai kidogo kwa ajili ya tumbo lake.’—1 Timotheo 5:23; Luka 10:34.

Kiasi Kinahitajiwa

Ona kwamba Paulo alipendekeza kunywa “divai kidogo” tu. Biblia inakataza waziwazi matumizi ya kupita kiasi ya kileo. Makuhani Wayahudi wangeweza kunywa kwa kiasi wakati ambao hawakuwa kazini. Hata hivyo, walikatazwa kunywa vileo walipokuwa wakifanya kazi zao za ukuhani. (Mambo ya Walawi 10:8-11) Miaka mingi baadaye, Wakristo wa karne ya kwanza walionywa kwamba walevi “hawataurithi ufalme wa Mungu.”—1 Wakorintho 6:9, 10.

Isitoshe, katika maagizo yake kwa Timotheo, Paulo anasema kwamba wale wanaoongoza kutanikoni, hawapaswi kuwa ‘walevi wenye fujo’ au “wenye kunywa divai nyingi.” * (1 Timotheo 3:3, 8) Hata Biblia inaamuru kwamba walevi wasiotubu waondolewe katika kutaniko la Kikristo. (1 Wakorintho 5:11-13) Kama Maandiko yanavyosema kwa kufaa, “divai ni mdhihaki.” (Methali 20:1) Kunywa kileo kupita kiasi kunaweza kumfanya mtu ashindwe kujizuia au afanye maamuzi mabaya.

Kwa Nini Neno la Mungu Hushutumu Kunywa Kupita Kiasi?

Yehova ‘anayetufundisha ili tujifaidi wenyewe,’ anajua kwamba tukitumia kitu chochote vibaya, hatimaye tutajiumiza na kuwaumiza wengine. (Isaya 48:17, 18) Ndivyo ilivyo tunapotumia vileo. Neno la Mungu linauliza: “Ni nani aliye na ole? Ni nani aliye na wasiwasi? Ni nani aliye na ugomvi? Ni nani aliye na mahangaiko? Ni nani aliye na majeraha yasiyo na sababu? Ni nani aliye na macho mazito?” Linajibu: “Ni wale wanaokaa muda mrefu kwenye divai, wale wanaoenda kutafuta divai iliyochanganyika.”—Methali 23:29, 30.

Watu wamefanya mambo mengi mabaya na hatari baada ya kunywa kupita kiasi, kama vile kuendesha gari wakiwa wamelewa na hivyo kuhatarisha uhai wao na wa wengine, kuvutiwa isivyofaa na mwenzi wa mtu mwingine na hivyo kuharibu mahusiano, kuzungumza na kutenda kipumbavu au hata mambo mapotovu. (Methali 23:33) Kwa kufaa imesemwa kwamba kunywa kupita kiasi ni mojawapo ya mambo maovu yanayowakumba wanadamu leo. Si ajabu kwamba Mungu anahimiza hivi: “Usiwe kati ya watu wanaokunywa divai mno”!—Methali 23:20.

Kwenye Wagalatia 5:19-21, Paulo anasema vipindi vya kulewa na karamu za kupindukia ni “matendo ya mwili” yaliyo kinyume cha matunda ya roho ya Mungu. Kunywa kupita kiasi kutaharibu uhusiano wa mtu pamoja na Mungu. Basi, ni wazi kwamba Wakristo wanapaswa kuepuka kunywa kileo kupita kiasi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Kwa kuwa waangalizi na watumishi wa huduma wanapaswa kuwawekea mfano kondoo kwa maamuzi na tabia zao na kufuata kanuni za juu za Yehova kadiri wanavyoweza, takwa hilo linawahusu Wakristo wengine pia.