Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Ponografia Asanteni sana kwa makala “Ponografia Inadhuru au Haidhuru?” (Julai 22, 2003) Nilihitaji shauri hilo la moja kwa moja. Muda mrefu kabla sijawa Mkristo, nilikuwa nikitazama ponografia. Makala hizo zilinisaidia nitambue wazi madhara ya kutazama ponografia na jinsi ninavyoweza kuacha zoea hilo sugu.

E. P., Marekani

Ndoa yangu yenye furaha iliyodumu kwa miaka 22 iliishia katika talaka miaka miwili iliyopita. Ponografia ilinifanya nibaki bila mume, na watoto bila baba mpendwa. Zoea hilo baya lilimfanya mume wangu aliyekuwa mpole na mwenye fadhili abadilike na kuwa mwenye hasira, mwongo, na mkatili. Nilikuwa mpweke kwa sababu ya zoea hilo, lakini sasa nimetambua kwamba hilo ni tatizo linalowakabili wengi. Asanteni sana kwa makala hizo nzuri.

L. T., Marekani

Kabla sijajifunza Biblia, nililemewa na zoea la kutazama ponografia kwa zaidi ya miaka 10. Haidhuru jinsi wengine wanavyoliona, hilo ni zoea baya kabisa. Kabla sijawa Shahidi wa Yehova, nilizoea kutumia karibu dawa zote za kulevya. Kati ya mazoea yote niliyokuwa nayo, kutazama picha chafu ndilo lililokuwa zoea gumu zaidi kuacha. Tafadhali endeleeni kuchapisha makala kama hizo.

J. A., Marekani

Vijana Huuliza Nawashukuru kutoka moyoni kwa makala “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Nataka Kila Kitu Ninachofanya Kiwe Kikamilifu?” (Julai 22, 2003) Mimi ni mhudumu wa wakati wote mwenye umri wa miaka 25. Tangu nilipokuwa mdogo, nimekuwa nikijilinganisha na dada na ndugu yangu ambao ni wakubwa wangu kwa miaka minne na mitatu. Nilihisi kwamba sifai chochote. Ili nikabiliane na hisia hizo, nilijitahidi kuwa mkamilifu. Makala hiyo ilieleza hisia zangu kabisa. Ninataka kubadili mawazo yangu.

M. Y., Japan

Nina umri wa miaka 16, na hivi majuzi iligunduliwa kwamba nimeshuka moyo. Sikuzote nimekuwa nikijaribu kufanya mambo kwa ukamilifu, nami hujiona kuwa siwezi kutekeleza jambo lolote. Makala hiyo ilikuja kwa wakati unaofaa kabisa. Sikuweza kujizuia kulia nilipokuwa nikiisoma. Sikutambua kwamba kuna wengi wanaokabiliana na hisia kama hizo. Asanteni kwa makala hizo za “Vijana Huuliza.” Ninatazamia makala inayofuata.

L. S., Marekani

Kome-Milia Nina umri wa miaka 12 na nilifurahia makala “Wadudu Wasumbufu Wanaosafisha Maji.” (Julai 22, 2003) Nilishangazwa na wazo kwamba kome wa kike anaweza kutaga mayai 500,000 kwa mwaka na kwamba inaelekea kuna kome 700,000 katika eneo la meta moja ya mraba. Tunapaswa kuilinda bahari kwa sababu kome-milia na viumbe wengine wanaishi humo. Tunapofanya hivyo, tunamheshimu Yehova Mungu pia. Tafadhali endeleeni kuandika makala za kupendeza kama hizo!

E. T., Italia

Makala za Zamani Hivi majuzi iligunduliwa kwamba binti yangu ana ugonjwa wa Parkinson. Nilipata makala yenye habari kuhusu ugonjwa huo katika toleo la Kiingereza la Januari 8, 1988 la Amkeni! Familia yetu yote ilisoma makala hiyo, pamoja na binti yangu, mara kadhaa. Habari hiyo imetusaidia kukabiliana na hali hiyo vizuri zaidi. Hata ingawa makala hiyo iliandikwa zaidi ya miaka 15 iliyopita, ilitusaidia sana. Mara kwa mara, Amkeni! huwa na makala kuhusu magonjwa ambayo hatujayasikia, na bila shaka zinawasaidia wale walio na magonjwa hayo. Nawashukuru sana kwa kazi mnayofanya.

E. M., Japan