Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Musa Ashambuliwa

Musa Ashambuliwa

MARA nyingi Wayahudi, Wakristo, na Waislamu hawakubaliani kuhusu mambo mengi. Hata hivyo, licha ya tofauti zao, dini hizo hukubaliana kuhusu jambo moja: zinamheshimu sana mwanamume anayeitwa Musa. Wayahudi wanamtambua kuwa “mwalimu mkuu zaidi kati ya walimu wote Wayahudi,” yaani, mwanzilishi wa taifa la Kiyahudi. Wakristo wanamwona kuwa mtangulizi wa Yesu Kristo. Na Waislamu wanamtambua Musa kuwa mmoja wa manabii wao wa kwanza wakuu zaidi.

Kwa hiyo, Musa ni mmojawapo wa watu wenye uvutano mkubwa sana katika historia ya wanadamu. Hata hivyo, kwa zaidi ya miaka mia moja, Musa ameshambuliwa na wasomi na makasisi. Mbali na kutilia shaka kwamba Musa alifanya miujiza na kuwaongoza Waisraeli kutoka Misri, wengi hupinga hata kuwapo kwake. Kitabu Moses—A Life cha Jonathan Kirsch kinasema: “Yale tunayoweza kusema kumhusu Musa ni kwamba huenda mtu fulani kama yule anayezungumziwa katika Biblia aliishi wakati na mahali pasipojulikana zamani za kale, na huenda mambo machache aliyofanya ndiyo yametumiwa kutunga hadithi ambayo imesimuliwa kwa karne nyingi hivi kwamba amekuwa mtu maarufu na anayezua ubishi ambaye anazungumziwa katika Biblia.”

Kwa kuona mambo kijuujuu, ubishi huo unaweza kuonekana kuwa wa kweli. Kwa mfano, wahakiki wanasema kwamba uthibitisho wa kiakiolojia umegunduliwa unaoonyesha kwamba watu fulani katika nyakati za Biblia waliishi, kama vile Mfalme Yehu wa Israeli. Lakini hakuna uthibitisho wowote wa kiakiolojia uliogunduliwa kuonyesha kwamba Musa aliishi. Hata hivyo, hiyo haithibitishi kwamba Musa ni mtu wa kuwaziwa tu. Wakati mmoja, wapinzani walisema kwamba watu fulani wanaotajwa katika Biblia, kama vile Mfalme Belshaza wa Babiloni na Mfalme Sargoni wa Ashuru, walikuwa watu wa kuwaziwa mpaka akiolojia ilipothibitisha kwamba waliishi.

Mwandishi Jonathan Kirsch anasema hivi: “Vitu vya kale vya Waisraeli vilivyosalia ni vichache sana hivi kwamba kukosekana kwa uthibitisho wa kwamba Musa aliishi isipokuwa ule ulio katika Biblia hakushangazi wala hakuthibitishi jambo lolote.” Kulingana na Kirsch, watu fulani husema kwamba haielekei kuwa Musa ni mtu wa kuwaziwa tu, kwa sababu “haingewezekana . . . , kubuni hadithi tata yenye matukio mengi na mazungumzo mengi sana kadiri hiyo.”

Uwe unafuata dini au la, yaelekea unajua mambo fulani muhimu kumhusu Musa: jinsi alivyozungumza na Mungu kwenye mti uliokuwa ukiwaka moto, jinsi Waisraeli walivyotoka utumwani Misri, na kugawanyika kwa Bahari Nyekundu. Lakini je, tuna sababu ya kuamini kwamba mambo hayo yalitokea? Au Musa ni mtu anayesimuliwa katika hadithi tu? Makala ifuatayo itazungumzia maswali hayo yenye kusisimua.