Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Idadi ya Watu, Biblia, na Wakati Ujao

Idadi ya Watu, Biblia, na Wakati Ujao

Idadi ya Watu, Biblia, na Wakati Ujao

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI SWEDEN

IDADI ya watu ulimwenguni iliongezeka kutoka bilioni 1.65 mwanzoni mwa karne ya 20 kufikia bilioni 6 mwishoni mwa karne hiyo. Je, idadi ya watu ulimwenguni itaendelea kuongezeka sana hivyo? Je, watu wataongezeka kupita kiasi katika milenia hii? Wataalamu wa takwimu hushughulikia masuala hayo tata, na taaluma hiyo huitwa demografia.

Kulingana na kamusi Webster’s Dictionary, demografia ni ‘uchunguzi wa idadi ya watu [hasa] kuhusiana na ukubwa na wingi, usambazaji, na takwimu zinazohusu uzazi, vifo, ndoa, afya, na maradhi.’ Wataalamu huchunguza mambo matatu ambayo huathiri idadi ya watu, yaani idadi ya watoto wanaozaliwa, idadi ya watu wanaokufa, na idadi ya watu wanaohamia nchi nyingine.

Demografia ya kihistoria ni uchunguzi wa ongezeko na upungufu wa idadi ya watu wakati uliopita. Wataalamu wa taaluma hiyo huchunguza kwa makini jamii za kale kwa kutumia maandishi, magofu, mifupa ya watu, na vitu vingine. Demografia hiyo hutegemea makadirio na utafiti wa kisayansi. Kitabu Atlas of World Population History kinasema: “Taaluma ya historia ya demografia haitegemei mambo ya hakika yanayoweza kuthibitishwa, hivyo haiwezi kutegemeka.” Hata hivyo, makadirio yanayohusu idadi ya watu ni muhimu kwa wanafunzi wa Biblia. Ama kweli, mara nyingi makadirio hayo hupatana na masimulizi ya Biblia.

Ongezeko la Idadi ya Watu Baada ya Gharika

Biblia inasema kwamba ni watu wanane tu waliookoka Gharika ya siku za Noa. Wataalamu fulani wa takwimu wanakadiria kwamba miaka 1,400 hivi baadaye, huenda idadi ya watu ulimwenguni ilifikia milioni 50. Je, inawezekana watu kuongezeka kutoka watu 8 hadi milioni 50 katika miaka 1,400?

Kwanza kabisa, idadi ya watu milioni 50 ni kadirio tu. Hata hivyo, inafaa kuona vile Biblia inavyosema kwenye Mwanzo 9:1: “Naye Mungu akambariki Noa na wanawe, akawaambia: ‘Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia.’” Kisha, katika sura ya 10 na 11, tunasoma juu ya familia 70 ambazo zilitokana na wana wa Noa—Shemu, Hamu, na Yafethi. Tunapoendelea kusoma, tunafikia ukoo wa Shemu hadi Abrahamu, ambao ‘walizaa wana na mabinti.’ Huenda wakati huo watu walizaa sana kulingana na amri ya Mungu ya ‘kuijaza dunia.’

Namna gani idadi ya watu waliokufa? Sura hizo za Mwanzo zinaeleza pia jinsi wanadamu walivyoishi maisha marefu sana miaka mingi baada ya Gharika. * Wakati watu wanapozaliwa sana na wachache kufa, kunakuwa na ongezeko la haraka.

Maisha ya Waisraeli Huko Misri

Watafiti fulani hawaamini kwamba Waisraeli waliongezeka haraka walipoishi katika nchi ya Misri kama Biblia inavyosimulia. Biblia inasema kwamba mbali na wake za wana wa Yakobo, “nafsi zote za nyumba ya Yakobo zilizokuja Misri zilikuwa 70.” (Mwanzo 46:26, 27) Hata hivyo, Waisraeli walipoondoka Misri miaka 215 baadaye, walikuwa wameongezeka sana na kufikia “wanaume mia sita elfu wanaotembea kwa miguu, bila kuhesabu watoto.” (Kutoka 12:37) Tukihesabu wanawake na watoto, huenda walikuwa Waisraeli milioni tatu hivi kwa ujumla! Je, hilo linawezekana?

Ili kujibu swali hilo, ona Biblia inavyosema kuhusu ongezeko la Waisraeli huko Misri: “Wana wa Israeli wakazaa na kuanza kujaa; nao wakazidi kuongezeka na kuwa wenye nguvu zaidi kwa kiwango kisicho cha kawaida, hivi kwamba wakaijaza nchi.” Ongezeko la Waisraeli wakati huo lilikuwa la kipekee.—Kutoka 1:7.

Kumekuwa na ongezeko kama hilo katika mataifa ya leo kama vile Kenya katika miaka ya 1980. Hata hivyo, kilichofanya ongezeko la Waisraeli liwe la kipekee ni kwamba liliendelea kwa muda mrefu.

Biblia inatoa sababu nyingine ya ongezeko la haraka la Waisraeli. Hakukuwa na upungufu wa chakula wakati Waisraeli walipokuwa Misri. Ni kweli kwamba kunapokuwa na njaa, watu wengi hufa mapema. Hivyo, watoto wachache huzaliwa wakati huo. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba Waisraeli walikuwa na chakula tele. Familia ya Yosefu ilipowasili Misri, Farao alimwambia Yosefu hivi: “Wape makao baba yako na ndugu zako katika sehemu bora kabisa ya nchi. Wape makao katika nchi ya Gosheni.” (Mwanzo 47:6) Hata baada ya Waisraeli kuwa watumwa wa Wamisri, inaonekana walikuwa na chakula cha kutosha. Kwa kweli, baada ya kukombolewa kutoka utumwani, Waisraeli walikumbuka mkate, samaki, matango, matikiti-maji, vitunguu vya majani, vitunguu, vitunguu-saumu, na vyungu vya nyama ambazo walikula wakiwa utumwani.—Kutoka 16:3; Hesabu 11:5.

Katika Karne ya Kwanza W.K.

Pia demografia inaweza kutusaidia kuelewa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kwa mfano, tunaposoma amri ya Yesu kwa wafuasi wake ya ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,’ huenda tukajiuliza, ‘Kazi hiyo ya kuhubiri ingefanywa kwa kadiri gani?’ (Mathayo 28:19) Ni watu wangapi walioishi katika Miliki ya Roma katika karne ya kwanza? Wengine hukadiria kwamba idadi ya watu ilikuwa kati ya milioni 50 na 60. Ikiwa ndivyo ilivyokuwa, Wakristo hao walioeneza injili walikuwa na kazi kubwa sana!

Tunaposoma Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, tunaona kwamba mtume Petro alisafiri mbali hadi Babiloni kuhubiri habari njema. (1 Petro 5:13) Kwa nini alienda Babiloni? Maelezo haya ya kitabu The New Encyclopædia Britannica yanatusaidia kuelewa: “Mbali na Palestina, maeneo mengine yaliyokuwa na Wayahudi wengi ni Siria, Asia Ndogo, Babilonia, na Misri, kwani inakadiriwa kwamba kila moja lilikuwa na angalau Wayahudi 1,000,000.” Kwa kuwa Petro alipewa kazi ya kuwahubiria Wayahudi hasa, ilifaa asafiri kwa jamii ya Wayahudi huko Babiloni. (Wagalatia 2:9) Kwa kuwa kulikuwa na Wayahudi wengi huko, alikuwa na eneo kubwa la kuhubiri!

Namna Gani Wakati Ujao?

Kama ambavyo tumeona, wataalamu wa takwimu wanataka kujua mambo fulani kuhusu historia ya wanadamu. Wao husema nini kuhusu wakati ujao? Wanauliza maswali muhimu. Je, watu wataongezeka kupita kiasi katika milenia hii? Hakuna anayejua kwa hakika. Kwa kuwa idadi ya watoto wanaozaliwa imepungua katika nchi nyingi, watafiti fulani wanatabiri kwamba idadi ya watu ulimwenguni haitaongezeka.

Hata hivyo, si wataalamu wote wanaokubaliana na hilo. Gazeti Population Today linasema: “Leo, kuna aina mbili za ongezeko la idadi ya watu: kuna nchi ambazo watu huzaa watoto wawili au mmoja tu na nyingine ambazo watu huzaa watoto wengi. Nchi ambazo wazazi huzaa ‘watoto wawili au mmoja’ zinatia ndani nchi za Ulaya, Marekani, Kanada, Japan, na nchi chache zinazoendelea haraka . . . Tofauti na hizo, nchi zenye ongezeko kubwa la idadi ya watu ni nchi za Afrika, Asia, na Amerika ya Latini, ambapo wazazi huzaa zaidi ya watoto wawili. Katika nchi hizo, zilizo na zaidi ya nusu ya watu wote ulimwenguni, kwa wastani kila mwanamke huzaa watoto wanne.”

Hivyo, ingawa idadi ya watu imepungua katika nchi fulani, imeongezeka au kubaki vilevile katika nchi nyingine. Gazeti Population Today linamalizia kwa kusema hivi kuhusu matumaini ya wakati ujao: “Katika nchi nyingi zinazoendelea, ongezeko kubwa la idadi ya watu halijakoma. Mwisho wa ‘ongezeko kubwa kupita kiasi la idadi ya watu’ ulimwenguni pote utakuja ikitegemea kiasi cha pesa ambazo nchi zinazohusika zinatumia kupunguza vifo vya watoto wachanga, kuwaelimisha wanawake, na kuandaa njia za kupanga uzazi.”

Je, idadi ya watu ulimwenguni itazidi ile iliyopo sasa ya watu bilioni sita? Tutajua wakati ujao. Lakini tunajua kusudi la Mungu ni kwamba dunia ijazwe, lakini si kupita kiasi. (Mwanzo 1:28) Na tuna uhakika kabisa kwamba chini ya Ufalme wa Mungu, jambo hilo litatimizwa.—Isaya 55:10, 11.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Baadaye, maisha ya wanadamu yalipungua hadi miaka 70 au 80 kama ilivyoonyeshwa na Musa karibu mwaka wa 1500 K.W.K.—Zaburi 90:10.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Waokokaji wa Gharika walizidisha idadi ya watu ulimwenguni ambayo sasa imepita bilioni sita

[Picha katika ukurasa wa 13]

Kwa miaka 215, idadi ndogo ya Waisraeli waliokuwa Misri iliongezeka na kufikia milioni tatu hivi