Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imani ya Familia Yajaribiwa

Imani ya Familia Yajaribiwa

Imani ya Familia Yajaribiwa

INDIA, msichana mwenye kuvutia wa umri wa miaka tisa kutoka Wisconsin, Marekani, ameugua sana. Amefanyiwa upasuaji mara tatu na kupata matibabu mengine mengi. Mama yake, Lori, anasema: “Kwa miaka sita ilibidi India akimbizwe hospitalini mara nyingi, alale huko, na amwone daktari mara kwa mara.”

India alianza kuugua alipokuwa na umri wa miezi 18. Alianza kupatwa na dalili zisizo za kawaida, kama vile kuendesha, homa kali, kufura tumbo, na kukonda sana. Pia aliumwa na tumbo. Kila usiku kwa miaka miwili, India aliamka mara nyingi akilia na hata nyakati nyingine akipiga mayowe kwa uchungu.

Madaktari walipokuwa wakijaribu kutafuta ugonjwa wake, India aliendelea kuteseka sana. Lori anasema: “Mtoto wetu hangeweza kula.” Baba yake, Mark, anasema: “Tulimtazama msichana wetu mchanga akidhoofika na hatukujua la kufanya. Nakumbuka usiku mmoja nikiwa hoi tukizungumza na Lori kuhusu mazishi ya India kwa kuwa tuliona kana kwamba angekufa.”

Hatimaye, iligunduliwa kwamba India alikuwa na vidonda katika utumbo mpana. Pia alikuwa na ugonjwa unaoathiri mirija ya nyongo katika ini. Magonjwa hayo yanaweza kutibiwa. Hata hivyo, alihitaji kufanyiwa upasuaji na kutumia dawa kwa ajili ya vidonda katika utumbo mpana. Watu wanaougua magonjwa hayo wanahitaji kutunzwa daima ili wapone.

Sasa miaka saba imepita tangu India alipoanza kuugua. Kwa sababu ya jitihada za madaktari, anaendelea kupona. Kwa kuwa wao ni Mashahidi wa Yehova, Mark na Lori wanahisi kwamba imani yao katika Neno la Mungu—hasa linalosema kuhusu magonjwa, kifo, na tumaini la ufufuo wakati ujao—imewasaidia kuvumilia. Imemsaidia India pia. Lori anasema: “Sikuzote India amezungumza waziwazi kuhusu tumaini la ufufuo linalotajwa katika Biblia. Tumaini hilo ni halisi sana kwake.”

Wakati mmoja ambapo India alikuwa katika chumba cha michezo hospitalini, alikutana na msichana mdogo ambaye dada yake alikuwa na ugonjwa wa lukemia. Lori anaeleza kilichofuata: “Msichana huyo alimwambia India anahofia kwamba dada yake atakufa. Kisha India akamweleza maoni ya Biblia kuhusu kifo na kwamba haogopi kufa. Siku iliyofuata mama ya msichana huyo alikuja kuniuliza maswali. Alishangaa jinsi ambavyo India alizungumza waziwazi na bila woga kuhusu mambo hayo.”

Mark na Lori wametambua kwamba sala za waamini wenzao ni msaada mkubwa. Mark anasema: “Zamani nilipowaambia watu kwamba ningesali kwa niaba yao au niliposali pamoja nao, sikuzote nilitamani kufanya zaidi. Sasa natambua umuhimu wa sala hizo. Sala ndio msaada mkubwa zaidi ambao tulihitaji wakati huo wa taabu. Tuna undugu wenye upendo kama nini!”

Mark pia anahisi kwamba ugonjwa wa India umewasaidia kujua mambo ya kutanguliza. Anasema: “Maoni yetu kuhusu vitu vya kimwili yamebadilika kabisa. Mtoto wako anapokuwa mgonjwa, vitu hivyo vinaonekana kuwa bure kabisa! Mambo muhimu maishani ni uhusiano wetu pamoja na Yehova Mungu na undugu wetu wenye upendo.”

Mark, Lori, India, na ndugu na dada zake, wanatazamia kwa hamu wakati uliotabiriwa na nabii Isaya ambapo “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—Isaya 33:24; Ufunuo 21:4.

[Picha katika ukurasa wa 22]

India Erickson

[Picha katika ukurasa wa 23]

Hospitali ya Watoto ya San Diego

[Picha katika ukurasa wa 23]

India na familia yao