Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwa Wenye Amani Kazini

Kuwa Wenye Amani Kazini

Kuwa Wenye Amani Kazini

KWA nini watu fulani huwadhulumu wengine? Biblia inatusaidia kuelewa jambo hilo. Inaeleza kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo na ndiyo sababu tunakabili “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Watu wengi ni “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi.” (2 Timotheo 3:1-5) Katika nyakati hizi ngumu, tabia hizo zimezidi na dhuluma ni mojawapo ya matokeo yake. Basi unawezaje kuwa mwenye amani kazini?

Kutatua Hali ya Kutoelewana

Mara nyingi dhuluma huanza wakati ambapo wafanyakazi hawatatui hali ya kutoelewana. Hivyo, badala ya kujiingiza katika mambo ya wengine, tatua mambo haraka usipoelewana na wengine. Tatua hali hiyo kwa busara na heshima. Zungumza na mtu mmoja-mmoja wala si kikundi. Ukiona kwamba mtu ana jambo dhidi yako, jaribu kusuluhisha mambo kabisa. Kumbuka shauri hili la Yesu: “Uwe tayari kusuluhisha mambo upesi pamoja na mtu anayekushtaki.”—Mathayo 5:25.

Isitoshe, kila mtu kazini hufaidika kunapokuwa na mawasiliano mazuri. Basi, jaribu kuzungumza vizuri na msimamizi wako bila kuonyesha kwamba unajaribu kujipendekeza kwake. Pia, kumbuka kwamba mawasiliano mazuri pamoja na wafanyakazi wenzako na wasaidizi wako yatakusaidia kushinda mfadhaiko. Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri, lakini katika wingi wa washauri mambo hutimizwa.”—Methali 15:22.

Hivyo, jitahidi juu chini kupatana na wafanyakazi wenzako. Hiyo haimaanishi ufanye mambo ili kuwapendeza watu tu kwa kukubali kila kitu shingo upande huku ukivunja kanuni zako eti ili udumishe amani. Lakini ukiwa mchangamfu na mwenye urafiki unaweza kuboresha hali. Uwe mwangalifu kuhusu yale unayosema na jinsi unavyoyasema. Biblia inatoa mashauri haya ya busara: “Jibu, linapokuwa la upole, hugeuza ghadhabu.” (Methali 15:1) “Utulivu wa ulimi ni mti wa uzima.” (Methali 15:4) “Kwa subira kiongozi hushawishiwa.” (Methali 25:15) “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.”—Wakolosai 4:6.

“Usawaziko Wenu na Ujulikane”

Mtume Paulo aliwashauri hivi Wakristo huko Filipi: “Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.” (Wafilipi 4:5) Ukifuata kanuni hiyo, jiwekee viwango vya mwenendo unaofaa. Epuka kujiamini kupita kiasi au kuwa mwenye haya sana. Wafanyakazi wenzako wakikuudhi, usijaribu kulipiza kisasi. Hutapata faida yoyote kwa kutenda maovu. Watendee wengine kwa heshima na staha, na inaelekea watakutendea vivyo hivyo.

Zaidi ya kufikiria mwenendo wako, fikiria pia mavazi yako. Jiulize: ‘Mavazi yangu yanaonyesha nini? Je, mavazi yangu yanaamsha tamaa mbaya? Je, ninavalia shaghalabaghala? Je, nijiwekee sheria kuhusiana na mavazi nitakayovaa kazini?’

Katika tamaduni nyingi, wafanyakazi wenye bidii wanaheshimiwa na kuthaminiwa sana. Kwa hiyo, jaribu kupata heshima kwa kufanya kazi kwa ustadi. Uwe mwenye kutegemeka na mwenye kuaminika. Hiyo haimaanishi ujaribu kufanya kila kitu kikamilifu. Mwanamke mmoja aliyedhulumiwa alikubali baadaye kwamba yeye ndiye aliyesababisha hali hiyo. Anasema: “Nilitaka kuwa mkamilifu.” Baadaye, mwanamke huyo alitambua kwamba haiwezekani kuwa mkamilifu: “Mimi hufanya kazi vizuri, lakini si lazima nifanye kila kitu kikamilifu.”

Usiathiriwe kupita kiasi na maneno yanayoumiza. Wakati mwingine unapochambuliwa bila sababu, hiyo haimaanishi unadhulumiwa. Mfalme Sulemani aliandika hivi katika Biblia: “Usiwe na haraka kuudhika katika roho yako . . . Pia, usiweke moyoni mwako maneno yote ambayo huenda watu wakasema, . . . kwa maana moyo wako mwenyewe unajua vema kwamba hata mara nyingi wewe, naam hata wewe, umewalaani wengine.”—Mhubiri 7:9, 21, 22.

Kwa kweli, kufuata kanuni hizo nzuri hakumaanishi kwamba hutadhulumiwa kamwe. Licha ya jitihada zako nzuri, huenda wafanyakazi wengine wakakudhulumu. Ufanye nini?

Tafuta Msaada

Gregory anasema hivi: “Nilipopuuzwa na wafanyakazi wenzangu kwa miezi kadhaa, niliumia kihisia.” Yaliyompata ni kama yale yanayowapata wale wanaodhulumiwa ambao hukasirika, hujiona kuwa wenye hatia, huaibika, huchanganyikiwa na kujiona kuwa hawafai. Kudhulumiwa kunaweza kumfanya hata mtu aliye imara kufadhaika. Biblia inasema kwamba “uonevu mtupu unaweza kumfanya mtu mwenye hekima atende kiwazimu.” (Mhubiri 7:7) Kwa hiyo ufanye nini?

Uchunguzi unaonyesha kwamba haifai kushughulikia dhuluma bila kuomba msaada. Anayedhulumiwa anaweza kupata wapi msaada? Makampuni fulani makubwa yanawasaidia wafanyakazi wao wanaohisi kwamba wanadhulumiwa. Makampuni hayo yanajua kwamba yatafaidika kwa kukomesha dhuluma. Kulingana na kadirio moja, wafanyakazi wanaowadhulumu wengine hutumia asilimia 10 ya muda wa kazi kufanya hivyo. Ikiwa kuna mpango wa kuwasaidia wanaodhulumiwa, mtu anaweza kuomba msaada huo. Mshauri wa kampuni hiyo au kampuni nyingine ambaye hana upendeleo, anaweza kuwasaidia wote wanaohusika kuzungumzia hali hiyo na kuwa na mwenendo mzuri kazini.

Hakuna Suluhisho Kamili

Inafaa tutambue kwamba hakuna suluhisho kamili la dhuluma. Hata wale wanaotumia kanuni za Biblia zinazopatikana katika makala hii huenda wakaendelea kudhulumiwa kazini. Hapana shaka kwamba Yehova Mungu anaona uvumilivu wao na jitihada zao za kuonyesha sifa za Kikristo licha ya hali ngumu.—2 Mambo ya Nyakati 16:9; Yeremia 17:10.

Dhuluma inapozidi, wengine huamua kutafuta kazi nyingine. Wengine hawana la kufanya kwa kuwa huenda si rahisi kupata kazi nyingine au msaada. Monika, aliyetajwa katika makala iliyotangulia, aliona kwamba tatizo lake lilisuluhishwa baada ya muda wakati mmoja wa wale waliokuwa wakimdhulumu sana alipoacha kazi. Hivyo, kukawa na amani kazini na alimaliza mafunzo yake kabla ya kuamua kutafuta kazi mahali pengine.

Peter, aliyetajwa katika makala ya kwanza, alitulia kabisa alipostaafu mapema. Hata hivyo, Peter alisaidiwa na mke wake alipokuwa akidhulumiwa. Anasema: “Alijua mambo yaliyokuwa yakinipata, naye aliniimarisha sana.” Kwa kuwa Monika na Peter ni Mashahidi wa Yehova, waliimarishwa na imani yao walipokuwa wakivumilia majaribu hayo. Walipofanya kazi ya kuhubiri walijiheshimu zaidi, na waliposhirikiana na waamini wenzao walihakikishiwa kwamba wana marafiki wenye kutegemeka.

Hata uwe katika hali gani, jitahidi uwezavyo kupatana na wafanyakazi wenzako. Ukidhulumiwa, jitahidi kufuata shauri hili la mtume Paulo: “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu. . . . Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote. . . . Usiache ushindwe na uovu, bali endelea kuushinda uovu kwa wema.”—Waroma 12:17-21.

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Ukiwa mchangamfu na mwenye urafiki unaweza kuboresha hali

[Blabu katika ukurasa wa 9]

“Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.”—WAROMA 12:18

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Shughulikia haraka hali ya kutoelewana