Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Ndoa Inapaswa Kuonwa Kuwa Takatifu?

Kwa Nini Ndoa Inapaswa Kuonwa Kuwa Takatifu?

Maoni ya Biblia

Kwa Nini Ndoa Inapaswa Kuonwa Kuwa Takatifu?

WATU wengi leo wanaweza kudai kwamba wanaiona ndoa kuwa takatifu. Basi kwa nini ndoa nyingi sana huvunjika? Kwa wengine, ndoa ni ahadi ya kimahaba tu na mapatano ya kisheria. Lakini ahadi zinaweza kuvunjwa. Watu wenye maoni hayo huvunja ndoa yao haraka mambo yakienda mrama.

Mungu anauonaje mpango wa ndoa? Jibu linapatikana katika Neno lake Biblia, kwenye Waebrania 13:4: “Ndoa na iheshimiwe kati ya wote.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “-a kuheshimiwa” linamaanisha kitu chenye thamani na kinachothaminiwa sana. Tunapothamini kitu, tunakihifadhi na kukichunga kisipotee, hata bila kupenda. Inapaswa kuwa hivyo pia katika mpango wa ndoa. Wakristo wanapaswa kuona ndoa kuwa yenye kuheshimiwa, yaani kitu chenye thamani wanachotaka kutunza.

Bila shaka, Yehova alianzisha mpango mtakatifu wa ndoa kati ya mume na mke. Lakini tunaweza kuonyeshaje kwamba tuna maoni kama yake kuhusu ndoa?

Upendo na Heshima

Wenzi wa ndoa wanapaswa kuheshimiana ili waheshimu mpango wa ndoa. (Waroma 12:10) Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wa karne ya kwanza: “Kila mtu mmoja-mmoja kati yenu na ampende hivyo mke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.”—Waefeso 5:33.

Ni kweli kwamba, nyakati nyingine huenda mwenzi wa ndoa akatenda bila upendo au heshima. Hata hivyo, Wakristo wanapaswa kuonyesha upendo na heshima. Paulo aliandika hivi: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia.”—Wakolosai 3:13.

Kutumia Wakati Pamoja

Wenzi wa ndoa wanaoona ndoa kuwa takatifu hutumia wakati kutimiza mahitaji ya kimwili na ya kihisia ya wenzi wao. Hilo linatia ndani ngono. Biblia inasema: “Mume na ampe mke wake haki yake; lakini mke pia na amfanyie vivyo hivyo mume wake.”—1 Wakorintho 7:3.

Hata hivyo, wenzi fulani wa ndoa wameona inafaa kwa mume kuhamia sehemu nyingine kwa muda ili kuchuma pesa zaidi. Nyakati nyingine hali hiyo imeendelea kwa muda mrefu isivyotazamiwa. Mara nyingi, hali hiyo imedhoofisha ndoa na wakati mwingine imesababisha uzinzi na talaka. (1 Wakorintho 7:2, 5) Kwa sababu hiyo, wenzi wengi Wakristo wameamua kwamba ni afadhali kutochuma pesa nyingi badala ya kuhatarisha ndoa ambayo wanaiona kuwa takatifu.

Matatizo Yanapotokea

Matatizo yanapotokea, Wakristo wanaoiheshimu ndoa yao hawafanyi haraka kutengana au kutalikiana. (Malaki 2:16; 1 Wakorintho 7:10, 11) Yesu alisema: “Kila mtu anayemtaliki mke wake, isipokuwa kwa sababu ya uasherati, anamweka katika hali ya kuweza kufanya uzinzi, na yeyote yule anayemwoa mwanamke aliyetalikiwa anafanya uzinzi.” (Mathayo 5:32) Kuamua kutalikiana au kutengana bila sababu za Kimaandiko ni kutoheshimu ndoa.

Maoni yetu kuhusu ndoa yanaonyeshwa na mashauri ambayo tunawapa wengine walio na matatizo makubwa ya ndoa. Je, sisi hupendekeza kutengana au kutalikiana haraka-haraka? Ni kweli kwamba huenda kukawa na sababu nzuri za kutengana kama vile kuumizwa sana kimwili au kutotegemeza familia kimakusudi. * Pia, kama ilivyotajwa juu, Biblia inaruhusu talaka ikiwa tu mwenzi wa ndoa amefanya uasherati. Hata hivyo, Wakristo hawapaswi kuwaamulia wengine jambo hilo. Isitoshe, yule mwenye tatizo la ndoa ndiye atakayekabili matokeo ya uamuzi wake wala si yule anayemshauri.—Wagalatia 6:5, 7.

Epuka Maoni ya Kutojali

Katika sehemu nyingine watu wanafunga ndoa ili wakubaliwe kuishi katika nchi fulani. Kwa kawaida, watu hao hukubali kumlipa raia wa nchi hiyo ili wafunge ndoa naye. Mara nyingi wenzi hao ijapokuwa wameoana, huishi mbalimbali labda hata bila kudumisha urafiki wowote. Punde wanapokubaliwa kuishi katika nchi hiyo, wanatalikiana. Wanaona ndoa kuwa mapatano ya kibiashara tu.

Biblia haiungi mkono maoni hayo ya kutojali. Licha ya nia zao, watu wanaofunga ndoa huingia katika mpango mtakatifu ambao Mungu anataka uwe wa kudumu. Watu wanaohusika katika mapatano hayo bado ni mume na mke, na wanapaswa kutimiza matakwa ya Biblia kuhusu talaka halali inayomruhusu mtu kuoa tena.—Mathayo 19:5, 6, 9.

Kama shughuli nyingine yoyote, ndoa yenye mafanikio inahitaji jitihada na uvumilivu. Wale wasioiona kuwa takatifu hutalikiana haraka. Au wanaweza kuamua kuishi tu katika ndoa yenye matatizo. Kwa upande mwingine, wale wanaoiona ndoa kuwa takatifu, wanajua kwamba Mungu anawataka waishi pamoja. (Mwanzo 2:24) Pia wanatambua kwamba wanamheshimu Mungu akiwa Mwanzilishi wa mpango wa ndoa kwa kuboresha ndoa yao. (1 Wakorintho 10:31) Maoni hayo huwasaidia kuvumilia na kujitahidi kufanikisha ndoa yao.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Ona toleo la Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1988, ukurasa wa 22-23.