Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jamani! Mbona Ananitesa?

Jamani! Mbona Ananitesa?

Vijana Huuliza . . .

Jamani! Mbona Ananitesa?

“Mara nyingi [mpenzi wangu] hunilaumu-laumu kwa mambo ya upuuzi. Lakini nampenda kwa dhati.”—Kathrin. *

“Kwa nje hungejua, lakini nilikuwa nikiumia sana kihisia.”—Andrea, aliyezabwa kofi na mpenzi wake.

NI JAMBO ambalo hutokea mara nyingi: Msichana anafanya urafiki na kijana anayeonekana kuwa mwenye kuvutia na mwenye heshima. Lakini pole kwa pole anaanza kubadilika. Anaacha kutumia maneno matamu ya mapenzi na badala yake anamdhihaki na kumchambua kwa madharau. Mwanzoni, msichana huyo anapuuza mambo hayo akiyaona kuwa utani. Hata hivyo, mambo yanakuwa mabaya zaidi mpenzi wake anapoanza kumshambulia-shambulia kwa maneno, kufoka kwa hasira, na kujuta. Msichana huyo anajilaumu, anaumia moyoni, na kutazamia kwamba mambo yatabadilika. Lakini wapi! Sasa mpenzi wake anaanza kupiga kelele. Pindi moja akiwa amepandwa na hasira, anamsukuma kwa jeuri! Msichana huyo anahofia kwamba wakati ujao atapigwa. *

Vijana wanaodhulumiwa na wapenzi wao, kimwili au kwa maneno, hushambuliwa kila wakati kwa kuchambuliwa, kwa maneno yenye kuumiza, na kwa hasira. Je, ndivyo maisha yako yalivyo? (Ona sanduku “Dalili Fulani Unazopaswa Kuzingatia.”) Ikiwa ndivyo, basi huenda ukawa umefadhaika na kuaibika sana hivi kwamba hujui la kufanya.

Hali kama hizo ni za kawaida. Watafiti wanakadiria kwamba mtu 1 kati ya 5 amewahi kutendewa kwa jeuri na mpenzi wake. Tukitia ndani wale wanaotukanwa na wapenzi wao, basi watu 4 kati ya 5 wanakabili hali hiyo. Kinyume na maoni ya watu wengi, si wanawake tu wanaodhulumiwa. Kulingana na uchunguzi mmoja wa Uingereza, “karibu asilimia ileile ya wanaume na wanawake” waliripoti kwamba wanatendewa kwa jeuri na wapenzi wao. *

Lakini kwa nini mambo hayo hutokea wakati wa uchumba? Ufanyeje ukijipata katika hali hiyo?

Maoni ya Mungu

Kwanza, unapaswa kutambua kwamba Mungu anaona jambo hilo kuwa zito. Ni kweli kwamba watu wasio wakamilifu wanaweza kusema na kufanya mambo yanayowaumiza wengine. (Yakobo 3:2) Pia, ni kweli kwamba hata watu wanaopendana na kuaminiana, watakosana mara kwa mara. Kwa mfano, mtume Paulo na Barnaba, walikuwa Wakristo wakomavu. Hata hivyo, pindi moja waliwaka kwa “hasira kali.” (Matendo 15:39) Kwa hiyo, ikiwa unamchumbia mtu, huenda mara kwa mara kutatokea kutoelewana.

Isitoshe, haifai kutarajia kwamba mchumba wako hatasema kamwe jambo lenye kuumiza. Nyote mnatarajia kuoana. Kwa hiyo, ikiwa kuna jambo fulani au tabia isiyompendeza, je, haitafaa azungumze nawe kuhusu jambo hilo kwa sababu anakupenda? Ni kweli kwamba mtu huumia anapokosolewa. (Waebrania 12:11) Lakini, ikiwa mtu anayekukosoa anafanya hivyo kwa upendo, hayo si matusi.—Methali 27:6.

Hata hivyo, kanuni hiyo haionyeshi kwamba ni sawa kupiga kelele, kumzaba mtu makofi, kumpiga ngumi, au kumtusi. Biblia inashutumu “ghadhabu, hasira, ubaya, matukano.” (Wakolosai 3:8) Yehova hukasirika sana wakati mtu anapotumia “nguvu” kuwashushia wengine heshima, kuwatisha, au kuwakandamiza. (Mhubiri 4:1; 8:9) Kwa hakika, Neno la Mungu huwaamuru waume “kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe . . . , kwa maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake kwa vyovyote; bali huulisha na kuutunza.” (Waefeso 5:28, 29) Mwanamume anayemtusi au kumdhulumu mwanamke anayemchumbia anaonyesha kwamba hastahili kuwa mwenzi wa ndoa. Isitoshe, anamchukiza Yehova Mungu mwenyewe!

Si Kosa Lako!

Mara nyingi watu wanaowadhulumu wachumba wao huwalaumu. Kwa hiyo, huenda ukahisi kwamba ni kosa lako wakati mpenzi wako anapokasirika. Lakini, huenda si wewe unayechochea hasira yake. Wanaume wengi wadhalimu walilelewa katika familia zilizozoea kutenda kwa jeuri au kutumia maneno yenye kuumiza. * Katika nchi fulani, vijana huathiriwa na desturi zinazoonyesha kwamba wanaume ndio bora. Marafiki pia wanaweza kumchochea kijana aonyeshe kwamba yeye ni mwanamume. Kwa sababu ya kutojiamini, huenda akaona kwamba unamdharau unaposema au kufanya jambo lolote lile.

Hata hali iweje, mtu mwingine anapofoka kwa hasira hilo si kosa lako. Matusi na jeuri hayakubaliki kamwe.

Badili Maoni Yako

Hata hivyo, huenda ukahitaji kubadili maoni yako. Kwa nini? Kwa mfano, ikiwa msichana amelelewa katika familia yenye jeuri na iliyozoea kutumia maneno yenye kuumiza, huenda akaona tabia hiyo kuwa sawa. Badala ya kuchukizwa na mwenendo huo usio wa Kikristo, anaweza kuuvumilia na hata kuufurahia. Naam, wasichana fulani waliozoea kudhulumiwa wanasema kwamba hawapendezwi na wanaume wapole sana. Wasichana wengine hufikiri kimakosa kwamba wanaweza kuwabadili wapenzi wao.

Ikiwa hayo ndiyo maoni yako, unahitaji ‘kugeuka kwa kufanya upya akili yako.’ (Waroma 12:2) Kupitia sala, kujifunza, na kutafakari, unapaswa kuzingatia maoni ya Yehova kuhusu dhuluma na hata kuichukia. Unapaswa kutambua kwamba hustahili kudhulumiwa. Ukiwa na kiasi unaweza kutambua kwamba huna uwezo wa kumbadili mpenzi wako mwenye hasira. Ni jukumu lake kubadilika!—Wagalatia 6:5.

Wasichana wengine huvumilia kudhulumiwa kwa sababu wanajidharau. Kathrin aliyetajwa mwanzoni anasema, “Sidhani ninaweza kuishi bila yeye, na sifikiri ninaweza kumpata mtu mwingine aliye afadhali.” Vivyo hivyo, mwanamke mwingine anayeitwa Helga alisema hivi kuhusu mpenzi wake, “Nilimruhusu anipige kwa sababu ni afadhali kupigwa kuliko kutotambuliwa hata kidogo.”

Je, maoni hayo yanaonyesha uhusiano mzuri kati ya watu wanaochumbiana? Je, kweli unaweza kumpenda mtu ikiwa hujipendi? (Mathayo 19:19) Jitahidi kujiheshimu. * Kuvumilia kudhulumiwa na mchumba hakutakusaidia kufanya hivyo. Kama mwanamke anayeitwa Irena anavyosema kutokana na yale yaliyompata, kuvumilia dhuluma “kunaweza kufanya ujidharau kabisa.”

Kuona Mambo Waziwazi

Huenda ikawa vigumu kwa wengine kukubali kwamba wanachumbiana na mtu asiyefaa, hasa ikiwa wamesitawisha hisia zenye nguvu za mahaba. Lakini ona mambo waziwazi. Methali moja ya Biblia inasema: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha, lakini wasio na uzoefu wameendelea mbele nao lazima waumie.” (Methali 22:3) Mwanamke mmoja anayeitwa Hanna anakumbuka hivi, “Ukimpenda mtu, huoni makosa yake, unaona sifa nzuri tu.” Hata hivyo, ikiwa anakudhulumu, ni muhimu kuona sifa zake waziwazi. Na ikiwa mpenzi wako anakutisha au kufanya ujidharau, basi mambo si mazuri. Usifiche hisia zako, usipuuze makosa yake, wala kujilaumu. Mambo ya hakika yanaonyesha kwamba mdhalimu asiporekebishwa, atazidisha dhuluma yake. Huenda usalama wako umo hatarini sana!

Jambo la busara ni kutojiingiza katika uhusiano pamoja na mtu asiyejizuia. (Methali 22:24) Basi ikiwa mtu usiyemjua vizuri anataka kukuchumbia, inafaa utafute habari fulani kumhusu. Unaweza kupendekeza mshirikiane naye mkiwa katika kikundi cha watu. Hilo linaweza kukusaidia kumjua kabla ya kusitawisha hisia za kimahaba haraka. Jiulize maswali muhimu kama vile: Rafiki zake ni nani? Anapenda muziki, sinema, na michezo gani? Je, mazungumzo yake yanaonyesha anapenda mambo ya kiroho? Zungumza na watu wanaomjua, kama vile wazee wa kutaniko lao. Watakuambia ikiwa ‘anashuhudiwa vema’ na wengine kutokana na mwenendo wake mkomavu na wa kumcha Mungu.—Matendo 16:2.

Lakini unaweza kufanya nini ikiwa tayari unadhulumiwa na mpenzi wako? Makala nyingine ya wakati ujao itazungumzia swali hilo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 5 Makala hii imeandikwa kwa ajili ya watu wanaoshambuliwa kwa maneno na kupigwa. Shauri linaloweza kuwasaidia watu wenye tabia hiyo lilitolewa katika makala “Kutoka Maneno Yaumizayo Hadi Maneno Yaponyayo” na “Kudhulumu—Kuna Ubaya Gani?” katika matoleo yetu ya Oktoba 22, 1996, na Machi 22, 1997.

^ fu. 7 Kanuni zinazozungumziwa hapa zinawahusu wanaume na wanawake.

^ fu. 14 Ona makala “Kufunua Visababishi vya Usemi Wenye Kuudhi,” katika toleo letu la Oktoba 22, 1996.

^ fu. 20 Ona sura ya 12 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku katika ukurasa wa 21]

Dalili Fulani Unazopaswa Kuzingatia

▪ Mara nyingi yeye husema mambo yanayoshusha heshima yako, ya familia yenu, au ya rafiki zako, mnapokuwa peke yenu au pamoja na wengine

▪ Hupuuza mapendezi yako au hisia zako

▪ Hujaribu kutawala maisha yako, kila wakati akitaka kujua mahali unapoenda na kukuamulia kila kitu

▪ Hukupigia kelele, hukusukuma, au kukutisha

▪ Hujaribu kukushawishi umwonyeshe upendo kwa njia zisizofaa

▪ Kila mara unapofanya kitu, unahofia kwamba atakasirika

[Picha katika ukurasa wa 20]

Kuchambuliwa au kutusiwa daima kwaweza kuonyesha kwamba uhusiano si mzuri