Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuuongoza Ulimi Kama Farasi Anavyoongozwa kwa Hatamu

Kuuongoza Ulimi Kama Farasi Anavyoongozwa kwa Hatamu

Kuuongoza Ulimi Kama Farasi Anavyoongozwa kwa Hatamu

Mfalme mwenye hekima Sulemani wa Israeli la kale alisema: “Farasi ni kitu kilichowekwa tayari kwa ajili ya siku ya pigano.” (Methali 21:31) Kwa miaka mingi, askari wapanda-farasi wamepigana na kushinda vita vingi. Tangu nyakati za kale, majeshi yalitumia hatamu kuongoza farasi.

Kitabu Encyclopædia Britannica, chasema kwamba hatamu ni “kamba zinazoshikilia lijamu mdomoni mwa farasi na hivyo humwezesha mtu kumwongoza kwa kutumia kamba hizo.” Hatamu za kale hazitofautiani sana na zile zinazotumiwa leo, nazo zilitumiwa sana kuwaongoza na kuwapanda farasi.

Daudi, baba ya Sulemani, alirejelea umuhimu wa hatamu alipoandika hivi: “Msijifanye kama farasi au nyumbu wasio na uelewaji, ambao roho yao yenye nguvu huzuiwa na hatamu au lijamu.” (Zaburi 32:9) Farasi wa kufugwa walikuwa waandamani waaminifu. Aleksanda Mkuu alimpenda sana farasi wake aliyeitwa Bucephalus hivi kwamba akaliita jiji moja la India kwa jina la farasi huyo.

Ingawa watu wameweza kuwaongoza farasi kwa maelfu ya miaka, wameshindwa kuongoza hali yao ya kutokamilika. Yakobo, mwanafunzi Mkristo aliandika hivi: “Kwa maana sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyo ni mtu mkamilifu, anayeweza kuuongoza kwa lijamu mwili wake wote pia.” (Yakobo 3:2) Kwa kweli, ni nani kati yetu anayeweza kusema kwamba hajawahi kusema neno la kipuuzi, lenye kuumiza, au lenye kukasirisha?

Kwa hiyo basi, kwa nini tujitahidi kuuongoza ulimi wetu mtundu, ambao ‘hakuna mtu anayeweza kuufuga’? (Yakobo 3:8) Watu hutumia muda mrefu kumzoeza farasi kwa sababu wanajua kwamba mnyama huyo aliyezoezwa atawafaidi hatimaye. Hali kadhalika, kadiri tunavyouzoeza na kuuongoza ulimi wetu vizuri zaidi, ndivyo utakavyozidi kutufaidi.

Maneno ya fadhili yanaweza kufariji na kutia moyo rafiki zetu, wafanyakazi wenzetu, na watu wa ukoo. (Methali 12:18) Maneno kama hayo yanaweza kufanya maisha ya watu tunaoshirikiana nao yawe yenye kufurahisha. Hata hivyo, ulimi usioongozwa unaweza kuleta matatizo. Biblia inaonya hivi: “Achungaye . . . ulimi wake hujiepusha na matatizo.” (Methali 21:23, Biblia Habari Njema) Kadiri tunavyofanikiwa kuuongoza ulimi wetu, tunajifaidi sisi wenyewe na wale wanaotusikiliza. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Biblia huwakumbusha Wakristo kwamba maneno yao yanahusiana sana na ibada yao. Inasema: “Ikiwa mtu yeyote anajiona kuwa mwabudu anayeshikilia vizuri namna ya ibada na bado hauongozi ulimi wake, bali anaendelea kuudanganya moyo wake mwenyewe, namna ya ibada ya mtu huyo ni ya ubatili.”—Yakobo 1:26.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Aleksanda Mkuu

[Hisani]

Alinari/Art Resource, NY