Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mailyn Atapata Uso Mpya

Mailyn Atapata Uso Mpya

Mailyn Atapata Uso Mpya

SIMULIZI LA MAMA YA MAILYN

Ilikuwaje hata binti yangu mpendwa, Mailyn, mwenye umri wa miaka 11 akahitaji uso mpya? Hebu nisimulie.

Mailyn ni binti yangu wa pili. Alizaliwa mnamo Agosti 5, 1992 huko Holguín nchini Kuba. Mimi, baba yake, na dada yake, tulifurahi sana alipozaliwa. Lakini furaha yetu ikakatishwa. Siku chache baada ya Mailyn kuzaliwa, nilipata ugonjwa wa tetekuwanga, na mwezi mmoja baadaye yeye pia akaambukizwa.

Mwanzoni, hali yake haikuonekana kuwa mbaya sana lakini ilizidi, ikabidi alazwe hospitalini. Mailyn alipata matibabu mazuri, lakini mfumo wake wa kinga ulikuwa umedhoofika sana hivi kwamba akapata ambukizo lingine. Niliona wekundu usio wa kawaida upande mmoja wa pua yake ndogo. Madaktari walisema kwamba hali hiyo imesababishwa na aina ya bakteria kali isiyo ya kawaida.

Ijapokuwa alipewa dawa za kuua bakteria hiyo bila kukawia, baada ya siku chache, bakteria hiyo ilianza kuuharibu uso wake. Kufikia wakati ambapo madaktari waliweza kuzuia kuenea kwa ugonjwa huo, Mailyn alikuwa amepoteza sehemu kubwa ya pua yake, midomo yake, ufizi na kidevu chake. Pia alikuwa na matundu upande mmoja wa jicho.

Mimi na mume wangu tulipomwona, tulibubujikwa na machozi. Jambo kama hilo lingewezaje kumpata binti yetu mchanga? Mailyn alikuwa katika wodi ya wagonjwa mahututi kwa siku kadhaa, na madaktari walifikiri kwamba atakufa. Mume wangu alikuwa akiniambia, “Jitayarishie chochote.” Hata hivyo, nilipoushika mkono wa Mailyn, alinishika kwa nguvu sana hivi kwamba nilijua ataendelea kuishi. Nilimwambia mume wangu: “Binti yetu hatakufa. Lakini katika hali hiyo, maisha yake yatakuwaje?” Kila asubuhi tulipoamka, tulidhani kwamba ilikuwa ndoto tu.

Tulipokuwa hospitalini, binti yetu mkubwa Maydelis, aliyekuwa na umri wa miaka sita, alikuwa akiishi na wazazi wangu. Alitamani sana kumwona dada yake akirudi nyumbani. Alipoondoka nyumbani, Mailyn alikuwa mrembo na mwenye macho ya kupendeza. Lakini Maydelis alipomwona dada yake tena, Mailyn alikuwa na sura ya kutisha.

‘Mbona Mtoto Wangu Anateseka Sana?’

Mailyn aliruhusiwa kuondoka hospitalini baada ya kukaa huko mwezi mmoja na nusu. Hatukurudi kwetu jijini kwa kuwa hatukutaka mtu yeyote amwone. Tulijitenga na kuishi katika nyumba ndogo huko mashambani, karibu na shamba la wazazi wangu.

Mwanzoni nilimnywesha Mailyn maziwa yangu kidogo-kidogo kupitia tundu lililokuwa usoni pake mahali mdomo ulipokuwa awali. Hangeweza kunyonya. Hata hivyo, vidonda vilipoanza kupona, karibu tundu hilo lizibike. Ningeweza tu kumlisha vyakula vya majimaji kwa kutumia chupa. Alipotimia umri wa mwaka mmoja, tulirudi Holguín, ambako madaktari walimfanyia upasuaji mara nne ili kupanua tundu hilo.

Nilikuwa nikijiuliza, ‘Mbona mtoto wangu anateseka sana?’ Nilitafuta majibu kwenye vituo vya kuwasiliana na pepo na kusali kwa kutumia sanamu zangu za kidini. Lakini sikupata faraja yoyote. Nilichanganyikiwa hata zaidi niliposikia maneno ya kuumiza kutoka kwa watu wa ukoo na marafiki. Wengine walisema, “Mungu anajua kwa nini anaruhusu mambo haya.” Na wengine wakaniambia, “Haikosi ni adhabu kutoka kwa Mungu.” Pia sikujua nitakalomwambia Mailyn atakapokuwa mkubwa. Wakati fulani alipokuwa mchanga bado, Mailyn alimuuliza baba yake, “Mbona sina pua kama watu wengine?” Baba yake hakumjibu bali alitoka nje na kulia. Nilijaribu kumweleza kilichokuwa kimetendeka. Bado anakumbuka jinsi nilivyokuwa nikimwambia kwamba mdudu mdogo alikula pua na mdomo wake.

Msingi wa Kuwa na Tumaini

Nilipokuwa nimekata tamaa kabisa, nilikumbuka kwamba mmoja wa jirani zangu ni Shahidi wa Yehova. Nilimwomba anionyeshe katika Biblia kwa nini Mungu anaruhusu binti yangu mchanga ateseke sana. Pia nilimuuliza, “Ikiwa ugonjwa huu ni adhabu kutoka kwa Mungu kwa sababu ya jambo ambalo nimefanya, mbona Mailyn ndiye anayeadhibiwa?”

Jirani yangu alianza kunifundisha Biblia akitumia kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. * Hatua kwa hatua nikaanza kutambua kwamba ugonjwa wa Mailyn haukusababishwa na Mungu na kwamba kwa kweli anatujali. (Yakobo 1:13; 1 Petro 5:7) Nikaanza kuthamini lile tumaini la ajabu kwamba kuteseka kutakomeshwa chini ya utawala wa Ufalme wake wa mbinguni mikononi mwa Yesu Kristo. (Mathayo 6:9, 10; Ufunuo 21:3, 4) Ujuzi huo ulinitia nguvu na kunichochea kuhudhuria mikutano ya Kikristo ya Mashahidi wa Yehova. Mwanzoni, mume wangu hakufurahishwa na mapendezi yangu mapya ya kiroho. Hata hivyo, hakunizuia kujifunza Biblia, maadamu kufanya hivyo kulinisaidia kuvumilia hali yetu ngumu.

Msaada Kutoka Ng’ambo

Mailyn alipokuwa na umri wa miaka miwili, daktari maarufu ambaye hutengeneza upya viungo huko Mexico alipata habari zake na kujitolea kumtibu bila malipo. Upasuaji wa kwanza ulifanywa mwaka wa 1994. Mimi na Mailyn tulikaa Mexico kwa mwaka mmoja hivi. Mwanzoni hatukuweza kuwasiliana na Mashahidi wa Yehova, hivyo hatukuweza kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Nilidhoofika kiroho. Kisha Shahidi mmoja mwenyeji akawasiliana nasi, tukaanza kushirikiana tena na waamini wenzetu kwa kadiri ilivyowezekana. Tuliporudi Kuba, nikarudia kujifunza Biblia na hali yangu ya kiroho ikaboreka.

Wakati huo mume wangu bado hakuwa anapendezwa na mambo ya Biblia. Kwa hiyo, ili kuamsha upendezi wake, nilikuwa nikimwomba anisomee sehemu mbalimbali za vichapo vya Biblia ili niweze kuzielewa vizuri zaidi. Hatimaye alikubali kujifunza Biblia kwa kuwa alihofia kwamba zile safari za muda mrefu huko Mexico zingeharibu uhusiano wetu wa familia. Aliona kwamba kuwa na mapendezi sawa ya kiroho kungeweza kutusaidia kushughulikia hali yetu vizuri wakati ambapo hatukuwa pamoja. Na ndivyo ilivyokuwa. Mimi, mume wangu, na binti yetu mkubwa tulibatizwa mwaka wa 1997 na kuwa Mashahidi wa Yehova.

Mara chache za kwanza tulipokuwa Mexico, Mailyn alikuwa akisema kwamba kama mdudu huyo mdogo hangeula uso wake, hatungekuwa mbali na baba na dada yake. Ilisikitisha sana kwamba familia yetu ililazimika kutengana kwa muda mrefu. Hata hivyo, ninakumbuka ziara moja iliyotutia moyo sana kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Mexico, inayoitwa Betheli. Mailyn alikuwa amesema kwamba hataki kupasuliwa tena—kwa mara ya tano tangu tulipofika huko—kwa kuwa alipata maumivu mengi alipokuwa akipona. Lakini Mashahidi kadhaa waliokuwa wakitumikia kwenye ofisi ya tawi walimwambia kwamba ikiwa hangeogopa na awaruhusu madaktari wamfanyie upasuaji, wangemfanyia karamu baada ya kutoka hospitalini. Kwa hiyo akakubali kupasuliwa.

Acha Mailyn aeleze alivyohisi: “Wazo la kuwa na karamu Betheli, lilinisisimua. Kwa hiyo, sikuogopa wakati wa upasuaji. Karamu hiyo ilikuwa nzuri sana, na kulikuwa na ndugu na dada wengi wa kiroho. Walinipa kadi nyingi na bado ninazo. Walinitia nguvu na hivyo kuniimarisha kuvumilia pindi nyingine za upasuaji ambazo zingefuata.”

Maendeleo na Msaada wa Kuvumilia

Mailyn, ambaye ana umri wa miaka 11, amepasuliwa mara 20 kurekebisha uso wake. Ingawa amesaidiwa sana, bado hawezi kufungua kinywa chake kabisa. Hata hivyo, sikuzote amekuwa na ujasiri na mtazamo mzuri. Pia anathamini sana mambo ya kiroho. Alijiandikisha kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi katika kutaniko letu akiwa na umri wa miaka sita, naye akabatizwa Aprili 27, 2003. Nyakati fulani yeye huongoza mafunzo matatu ya Biblia. Pindi moja alipokuwa Mexico, alizungumza na mtu aliyekubali ajifunze naye Biblia. Mailyn alimwalika kwenye Ukumbusho wa kifo cha Kristo na kwenye mikutano mingine ya kutaniko, ambayo alihudhuria akiwa na hamu kubwa.

Mailyn anapohubiri nyumba kwa nyumba, watu fulani humtazama na kumwuliza ikiwa aliungua. Mailyn huchukua nafasi hiyo kuzungumza nao kuhusu tumaini la kwamba Yehova atampa uso mpya katika Paradiso inayokuja.—Luka 23:43.

Maumivu ambayo Mailyn amepata kutokana na upasuaji na dhihaka za watoto wengine hayana kifani. Ni nini ambacho kimemsaidia kuvumilia? Mailyn anajibu hivi kwa usadikisho: “Yehova ni halisi sana kwangu. Yeye hunipa nguvu na ujasiri wa kuvumilia. Sitaki kuendelea kupasuliwa kwa sababu madaktari tayari wamefanya wanachoweza. Hawawezi kamwe kunirudishia sura niliyozaliwa nayo. Lakini ninajua kwamba Yehova atanipa uso mpya katika ulimwengu mpya, nami nitakuwa mrembo tena.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 26]

“Yehova atanipa uso mpya katika ulimwengu mpya”

[Blabu katika ukurasa wa 27]

Hatua kwa hatua nikaanza kutambua kwamba ugonjwa wa Mailyn haukusababishwa na Mungu