Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ulimwengu Usio na Magonjwa

Ulimwengu Usio na Magonjwa

Ulimwengu Usio na Magonjwa

“Nchi zote zinapaswa kushirikiana ili kuhakikisha kwamba watu wote wanapata matibabu ya msingi, kwani, watu wa nchi moja wakiwa na afya nzuri watu katika nchi nyingine watafaidika.” —AZIMIO LA ALMA-ATA, SEPTEMBA 12, 1978.

MIAKA 25 iliyopita watu fulani walionelea kwamba haingewezekana kwa kila mtu duniani kupata matibabu ya msingi. Wajumbe katika Mkutano wa Kimataifa Kuhusu Matibabu ya Msingi, uliofanywa huko Alma-Ata, panapoitwa Kazakhstan leo, waliazimia kwamba wanadamu wote wachanjwe dhidi ya magonjwa hatari ya kuambukiza kufikia mwaka wa 2000. Pia, walitumainia kwamba kufikia mwaka huo, watu wote duniani wangekuwa na mazingira safi na maji safi. Mataifa yote yaliyo wanachama wa Shirika la Afya Ulimwenguni yalitia sahihi azimio hilo.

Bila shaka mradi wenyewe ulistahili pongezi, lakini kutekelezwa kwa azimio hilo kumekuwa jambo lenye kuvunja moyo sana. Matibabu ya msingi hayapatikani kwa watu wote ulimwenguni, nayo magonjwa ya kuambukiza yanazidi kuhatarisha afya ya mabilioni ya watu duniani. Mara nyingi magonjwa hayo hatari huwashambulia watoto na watu wazima walio katika upeo wa maisha yao.

Hata tisho la yale magonjwa matatu, UKIMWI, kifua-kikuu, na malaria, halijachochea ‘nchi zishirikiane.’ Hazina ya Kupambana na UKIMWI, Kifua-kikuu na Malaria iliyoanzishwa majuzi, iliomba serikali zichange dola bilioni 13 ili kusaidia kuzuia kuenea kwa magonjwa hayo. Hata hivyo, kufikia katikati ya mwaka wa 2002, dola zipatazo bilioni 2 tu ndizo zilizokuwa zimetolewa. Mwaka huohuo dola bilioni 700 hivi zilitumiwa katika shughuli za kijeshi! Ni jambo lenye kusikitisha kwamba katika ulimwengu wa leo uliogawanyika, ni mambo machache sana yanayoweza kuunganisha mataifa yote kwa faida ya watu wote.

Ingawa maofisa wa afya wana nia njema, hawana uwezo wa kupambana na magonjwa ya kuambukiza. Huenda serikali zisitoe pesa zinazohitajiwa. Dawa nyingi hazina nguvu ya kuangamiza bakteria sugu, na watu wengi wanaishi maisha yanayohatarisha afya yao. Isitoshe, matatizo makubwa kama vile umaskini, vita, na njaa hufanya iwe rahisi kwa mamilioni ya watu kushambuliwa na viini mbalimbali.

Mungu Anatujali

Lakini kuna utatuzi. Tuna hakika kwamba Yehova Mungu anahangaikia sana afya ya wanadamu. Mfumo wetu wa kinga huthibitisha hilo. Sheria nyingi ambazo Yehova aliwapa Waisraeli wa zamani zilionyesha nia yake ya kuwalinda dhidi ya magonjwa ya kuambukiza. *

Yesu Kristo pia, aliye na utu kama wa Baba yake wa mbinguni, huwahurumia wagonjwa. Injili ya Marko inataja pindi moja ambapo Yesu alikutana na mtu mwenye ukoma. Mtu huyo mwenye ukoma alisema hivi: “Ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.” Yesu alijawa na huruma alipoona uchungu wa mtu huyo, akamwambia, “Ninataka. Takasika.”—Marko 1:40, 41.

Yesu hakuwaponya kimuujiza watu wachache tu. Mwandishi wa Injili, Mathayo, aliandika kwamba Yesu “a[li]enda akizunguka katika Galilaya yote, akifundisha . . . na kuhubiri habari njema ya ufalme na kuponya kila namna ya ugonjwa na kila namna ya udhaifu katikati ya watu.” (Mathayo 4:23) Kusudi la maponyo yake halikuwa kuwasaidia tu watu waliougua huko Yudea na Galilaya. Maponyo hayo yanatuonyesha jinsi magonjwa yote yatakavyokomeshwa wakati ambapo Ufalme wa Mungu, ambao Yesu alihubiri, utakapotawala wanadamu bila kupingwa.

Afya Duniani Pote Si Ndoto Tu

Biblia inatuhakikishia kwamba watu wote wanaweza kuwa na afya nzuri. Mtume Yohana aliona kimbele wakati ambapo ‘hema la Mungu litakuwa pamoja na wanadamu.’ Baada ya Mungu kufanya hivyo, “kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” Je, hilo linasikika kuwa jambo lisilowezekana? Katika mstari unaofuata, Mungu mwenyewe anatangaza hivi: “Maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.”—Ufunuo 21:3-5.

Bila shaka, ili magonjwa yaondolewe ni lazima umaskini, njaa, na vita viondolewe, kwa sababu mambo hayo hutokea sambamba. Kwa hiyo, Mungu atatumia Ufalme wake, serikali ya mbinguni mikononi mwa Kristo, kutimiza kazi hiyo kubwa. Sala za mamilioni ya watu zitajibiwa wakati ambapo serikali hiyo itakuja na kuhakikisha kwamba mapenzi ya Mungu yanatimizwa duniani.—Mathayo 6:9, 10.

Ufalme wa Mungu utakuja wakati gani? Alipokuwa akijibu swali hilo, Yesu alitabiri kwamba ulimwengu ungekumbwa na mfululizo wa matukio muhimu ambayo yangekuwa ishara ya kuonyesha kwamba Ufalme utachukua hatua hivi karibuni. Alisema kwamba mojawapo ya mambo hayo ni kuzuka kwa ‘tauni mahali pamoja baada ya pengine.’ (Luka 21:10, 11; Mathayo 24:3, 7) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “tauni” linamaanisha “ugonjwa wowote hatari wa kuambukiza.” Bila shaka, katika karne ya 20 kulikuwa na magonjwa mengi sana ya kuambukiza, licha ya maendeleo mengi katika sayansi ya tiba.—Ona sanduku “Vifo Kutokana na Tauni Mbalimbali Tangu 1914.”

Unabii wa kitabu cha Ufunuo, unaolingana na maneno ya Yesu katika Injili, unaonyesha wapanda-farasi kadhaa wanaoandamana na Yesu Kristo anapoanza kutawala mbinguni. Mpanda-farasi wa nne ameketi juu ya “farasi wa rangi ya kijivu,” naye anatokeza “pigo lenye kufisha.” (Ufunuo 6:2, 4, 5, 8) Idadi ya watu ambao wamekufa kutokana na magonjwa hatari ya kuambukiza tangu mwaka wa 1914 inathibitisha kwamba mpanda-farasi huyo amekuwa akimwendesha farasi wake. Kuenea kwa “pigo lenye kufisha” ulimwenguni pote ni uthibitisho mwingine wa kwamba Ufalme wa Mungu uko karibu. *Marko 13:29.

Ingawa sayansi ya tiba imefanikiwa kupunguza magonjwa ya kuambukiza kwa miaka kadhaa, magonjwa mapya yamezuka. Bila shaka, tunahitaji suluhisho la kudumu kwa tatizo hilo. Muumba wetu ameahidi kufanya hivyo. Nabii Isaya anatuhakikishia kwamba chini ya Ufalme wa Mungu, “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” Isitoshe, “[Mungu] atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote.” (Isaya 25:8; 33:22, 24) Siku hiyo itakapofika, magonjwa yatakuwa yamekomeshwa kabisa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Sheria ya Musa ilikuwa na maagizo kuhusu namna ya kuondoa takataka, namna ya kudumisha usafi wa mazingira na wa kimwili, na kuwatenga watu waliokuwa na magonjwa ya kuambukiza. Dakt. H. O. Philips anasema kwamba “mambo yanayopatikana katika Biblia kuhusu maisha, kupima magonjwa, matibabu, na mbinu za kuzuia magonjwa, ni ya kiwango cha juu zaidi na yenye kutegemeka zaidi kuliko dhana za Hippocrates.”

^ fu. 15 Unaweza kupata habari zaidi zinazothibitisha kwamba Ufalme wa Mungu unaokuja uko karibu, katika sura ya 11 ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

Vifo Kutokana na Tauni Mbalimbali Tangu 1914

Takwimu zinazofuata ni makadirio tu. Hata hivyo, zinaonyesha kiwango ambacho tauni mbalimbali zimewahangaisha wanadamu tangu 1914.

Ndui (kati ya milioni 300 na milioni 500) Hakuna matibabu yoyote yanayofaa yaliyovumbuliwa. Hatimaye mradi mkubwa wa kimataifa wa kuwachanja watu ulifanikiwa kuondolea mbali ugonjwa huo kufikia mwaka wa 1980.

Kifua-kikuu (kati ya milioni 100 na milioni 150) Leo, ugonjwa huo huua watu wapatao milioni mbili kila mwaka, na mtu 1 kati ya watu 3 ulimwenguni ana viini vya ugonjwa huo.

Malaria (kati ya milioni 80 na milioni 120) Miaka 50 ya kwanza ya karne ya 20, idadi ya watu waliokuwa wakifa kutokana na malaria ilikuwa milioni mbili hivi kila mwaka. Leo, idadi kubwa ya watu wanaokufa kutokana na ugonjwa huo inapatikana barani Afrika, kusini mwa Sahara, ambapo bado malaria huua zaidi ya watu milioni moja kila mwaka.

Homa ya Hispania (kati ya milioni 20 na milioni 30) Wanahistoria fulani husema kwamba watu wengi zaidi walikufa kutokana na ugonjwa huo kuliko inavyokadiriwa. Ugonjwa huo hatari ulienea ulimwenguni mwaka wa 1918 na 1919, baada tu ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. “Hata ile tauni ya majipu haikuua watu wengi hivyo mara moja,” chasema kitabu Man and Microbes.

Homa ya Chawa (milioni 20 hivi) Mara nyingi ugonjwa huo ulikuwa ukizuka wakati wa vita, navyo Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilitokeza tauni ya chawa iliyokumba nchi za Ulaya Mashariki.

UKIMWI (zaidi ya milioni 20) Tauni hii ya siku zetu sasa inaua watu milioni tatu kila mwaka. Makadirio ya sasa ya shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulika na UKIMWI yanaonyesha kwamba “kusipokuwa na jitihada za kutosha za kuuzuia na kuutibu, watu milioni 68 watakufa . . . kati ya mwaka wa 2000 na 2020.”

[Picha katika ukurasa wa 11]

Chini ya Ufalme wa Mungu, magonjwa kama haya hayatakuwa tisho tena

UKIMWI

Malaria

Kifua-kikuu

[Hisani]

AIDS: CDC; malaria: CDC/Dr. Melvin; TB: © 2003 Dennis Kunkel Microscopy, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Yesu aliponya kila namna ya ugonjwa na udhaifu