Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuhangaika Kunaonyesha Kwamba Mtu Hana Imani?

Je, Kuhangaika Kunaonyesha Kwamba Mtu Hana Imani?

Maoni ya Biblia

Je, Kuhangaika Kunaonyesha Kwamba Mtu Hana Imani?

“MAHANGAIKO YAMEPIGWA MARUFUKU.” Mwanzoni mwa karne ya 20, padri mmoja aliandika makala yenye kichwa hicho. Katika makala hiyo aliandika kwamba kuhangaikia vitu vya kimwili si kosa tu bali ni “dhambi nzito sana.” Hivi karibuni, mtu mmoja aliandika hivi kuhusu kushinda wasiwasi na mahangaiko: “Tukiwa na wasiwasi, ni wazi kwamba hatumwamini Mungu.”

Waandishi hao wawili walifikia mkataa wao kwa kutumia Mahubiri ya Mlimani ya Yesu, ambapo alisema: “Acheni kuhangaika.” (Mathayo 6:25) Kwa kuwa watu wengi sana leo huhangaika, tunaweza kuuliza hivi: Je, Mkristo anapaswa kuhisi hatia kwa kuhangaika? Je, kuhangaika kunaonyesha kwamba mtu hana imani?

Mungu Anajua Kwamba Sisi Si Wakamilifu

Biblia haifundishi kwamba mahangaiko yote husababishwa na ukosefu wa imani. Kwa kuwa tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” haiwezekani kuepuka kabisa mahangaiko. (2 Timotheo 3:1) Wakristo waaminifu huhangaishwa kila siku na magonjwa, uzee, matatizo ya kiuchumi, mizozo ya familia, uhalifu, na matatizo mengine. Hata katika nyakati za kale, watumishi wa Mungu walikuwa na wasiwasi na mahangaiko.

Hebu fikiria masimulizi ya Biblia kumhusu Loti. Mungu alimwagiza akimbilie milimani ili asifagiliwe mbali wakati wa uharibifu wa Sodoma na Gomora. Hata hivyo, Loti alihangaika na kusema: “Sivyo, tafadhali, Yehova!” Kisha akaongezea hivi akisitasita: “Lakini mimi—mimi siwezi kukimbilia eneo lenye milima kwa sababu naogopa nisije nikafikiwa na msiba nife.” Kwa nini Loti aliogopa eneo hilo lenye milima? Biblia haielezi. Vyovyote vile, Loti aliogopa sana. Mungu alitendaje? Je, Loti aliadhibiwa kwa sababu ya kukosa imani au kutomtumaini Mungu? Hapana. Badala yake, Yehova alimjali, akamruhusu Loti akimbilie jiji lililokuwa karibu.—Mwanzo 19:18-22.

Biblia ina mifano mingine ya waabudu waaminifu waliohangaika sana katika pindi fulani. Nabii Eliya aliogopa na kukimbia alipotishwa kuuawa. (1 Wafalme 19:1-4) Musa, Hana, Daudi, Habakuki, Paulo, na wanaume na wanawake wengine wenye imani thabiti walikuwa na mahangaiko pia. (Kutoka 4:10; 1 Samweli 1:6; Zaburi 55:5; Habakuki 1:2, 3; 2 Wakorintho 11:28) Hata hivyo, Mungu aliwahurumia, akaendelea kuwatumia katika utumishi wake, na kwa kufanya hivyo akaonyesha kwamba anawajali kwelikweli wanadamu wasio wakamilifu.

“Dhambi Ambayo Hututatanisha kwa Urahisi”

Hata hivyo, mahangaiko yakiendelea yanaweza kudhoofisha imani yetu na kufanya tuache kumtumaini Mungu. Mtume Paulo alisema kwamba ukosefu wa imani ni “dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi.” (Waebrania 12:1) Kwa kujitia ndani, inaonekana Paulo alikubali kwamba yeye pia angeweza ‘kutatanishwa kwa urahisi’ mara kwa mara, imani yake ilipokuwa dhaifu.

Huenda ndivyo ilivyokuwa kumhusu Zekaria, alipokosa kumwamini malaika aliyemwambia kwamba mke wake angechukua mimba. Pindi moja, mitume wa Yesu walishindwa kuponya kwa sababu ya ‘imani yao kidogo.’ Hata hivyo, watu hao waliendelea kupata kibali cha Mungu.—Mathayo 17:18-20; Luka 1:18, 20, 67; Yohana 17:26.

Kwa upande mwingine, Biblia pia inataja mifano ya watu walioacha kumtumaini Mungu na kupatwa na matokeo mabaya. Kwa mfano, Waisraeli wengi waliotoka Misri hawakuruhusiwa kuingia Nchi ya Ahadi kwa sababu ya ukosefu wao wa imani. Wakati mmoja, hata walimpinga Mungu, wakisema: “Kwa nini mmetutoa Misri ili tufe nyikani? Kwa maana hakuna mkate wala maji.” Mungu alionyesha kwamba amechukizwa kwa kutuma nyoka wenye sumu ili wawaadhibu.—Hesabu 21:5, 6.

Wakaaji wa Nazareti, mji wa nyumbani wa Yesu, walikosa pendeleo la kuona miujiza zaidi ikifanywa katika eneo la kwao kwa sababu hawakuwa na imani. Isitoshe, kizazi kiovu cha wakati huo kilipokea hukumu kali kutoka kwa Yesu kwa sababu hakikuwa na imani. (Mathayo 13:58; 17:17; Waebrania 3:19) Mtume Paulo alionya hivi kwa kufaa: “Jihadharini, akina ndugu, ili moyo mwovu unaokosa imani usije ukasitawi ndani ya yeyote kati yenu kwa kujiondoa kwa Mungu aliye hai.”—Waebrania 3:12.

Naam, katika hali zisizo za kawaida, moyo mwovu unaweza kumfanya mtu akose imani. Lakini sivyo alivyokuwa Zekaria wala wale mitume wa Yesu waliotajwa katika mifano iliyotajwa awali. Ukosefu wao wa imani ulitokana na udhaifu wa muda. Maisha yao kwa ujumla yalionyesha kwamba walikuwa “safi moyoni.”—Mathayo 5:8.

Mungu Anajua Mahitaji Yetu

Maandiko hutusaidia kutofautisha mahangaiko ya kawaida na ile dhambi ya ukosefu wa imani. Kuwa na mahangaiko ya kila siku au hata kukosa imani kidogo kwa sababu ya udhaifu wa kibinadamu si sawa na kukosa kumtumaini Mungu kabisa kunakotokana na moyo mwovu na mgumu. Kwa hiyo, Wakristo hawapaswi kuhisi hatia kwa sababu ya mahangaiko yao ya mara kwa mara.

Hata hivyo, tunapaswa kuwa waangalifu ili mahangaiko yetu yasipite kiasi na kutulemea. Ndiyo sababu Yesu alisema maneno haya ya hekima: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’” Kisha akaongeza maneno haya yenye kufariji: “Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote. Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.”—Mathayo 6:25-33.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Mtume Paulo alikuwa na mahangaiko