Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Ukamilifu Ninataka kuwashukuru kwa zile makala, “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Nataka Kila Kitu Ninachofanya Kiwe Kikamilifu?” na “Nawezaje Kuacha Kutarajia Ukamilifu?” (Julai 22 na Agosti 22, 2003) Nililemewa sana na tatizo langu la kutaka kila kitu ninachofanya kiwe kikamilifu, hivyo nikapoteza shangwe yangu. Kwa kuwa niliogopa kukosea, hata niliepuka kujibu katika mikutano ya Kikristo. Ninamshukuru sana Yehova kwa makala hizo. Zinanisaidia kudhibiti maoni yangu yasiyofaa.

S. M., Italia

Makala hizo zilinisaidia kushughulikia tatizo ambalo nimekuwa nalo kwa miaka 50. Nilidhani hakuna ubaya kutaka kila kitu ninachofanya kiwe kikamilifu, kwani nilifikiri kwamba ninampa Yehova kilicho bora. Sikujua ni kwa nini mara nyingi sikuelewana na watoto wangu, wafanyakazi wenzangu, na ndugu zangu Wakristo. Sasa natambua kwamba nilikuwa nimekosa usawaziko na maoni yangu hayakupatana na maoni ya Yehova. Kwa kuwa “mwadilifu kupita kiasi” nimejiletea huzuni na kuwahuzunisha wengine. (Mhubiri 7:16) Si rahisi kushinda tatizo hilo, lakini kwa msaada wa Yehova nitajitahidi.

C. H., Marekani

Ni kweli kabisa kwamba mtu anapotaka kila kitu anachofanya kiwe kikamilifu anaweza kushindwa kutenda lolote! Nimevunjika moyo kwa miaka mingi huku nikijiuliza ni kwa nini siwezi kutimiza mambo ambayo nilitamani sana kuyafanya. Sasa ninaelewa ni kwa nini mara nyingi hakuna aliyetaka kuwa karibu nami. Ninajua kwamba nina kazi ngumu mbele yangu, lakini Yehova atanisaidia.

L. R., Marekani

Nimepambana na tatizo hilo kwa miaka kadhaa, kila mara nikihisi kwamba chochote ninachofanya hakifai. Inafariji kujua kwamba kuna wengine wanaopambana na tatizo la kutaka kufanya mambo kikamilifu.

A. B., Kanada

Ninatambua akilini kwamba hakuna mtu anayeweza kuwa mkamilifu, lakini hisia zangu hunichochea nitake kufanya mambo kikamilifu. Nilitiwa moyo sana kusoma kwamba Yehova hatazamii ukamilifu kutoka kwetu na kwamba anaangalia kilicho moyoni. Ninashukuru kwa makala hizo.

S. K., Ujerumani

Sikuzote kuogopa kushindwa kumenizuia kuchukua hatua. Nimejifunza kwamba kutaka kufanya mambo kikamilifu humfanya mtu akasirike nyakati zote, atazamie mabaya, ashuke moyo na kujiona kuwa hafai. Bado sijatatua kabisa tatizo langu, lakini ninataka siku moja niweze kujicheka ninapokosea.

A.  I., Japani

Nimekuwa na mfadhaiko mwingi na mahangaiko mengi akilini. Nimekuwa nikijilaumu na kusema kwamba, “Mimi ni bure kabisa.” Makala zenu zimenisaidia kuwa na maoni mazuri na zimenitia moyo. Ule mzigo mzito uliokuwa ukiulemea moyo wangu—ile tamaa ya kufanya mambo kikamilifu—umepungua. Maandiko yamenisaidia kubadili mtazamo wangu na kusitawisha maoni yanayofaa.

M. N., Japani

St. Petersburg Tunawashukuru kwa makala “St. Petersburg Ni Njia ya Urusi ya Kuelekea Ulaya.” (Agosti 22, 2003) Tulipokuwa kwenye fungate yetu ya majuma mawili, tulitembelea maeneo maarufu huko St. Petersburg. Hatutasahau kamwe ziara yetu kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova, Ukumbi wa Maonyesho wa Mariinsky, Jumba la Makumbusho la Hermitage, na Peterhof. Asanteni sana kwa makala hiyo. Tuliitumia tulipokuwa tukitembelea jiji hilo lenye kuvutia!

A. na O. S., Urusi