Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakati Ambapo Hakuna Mtu Atakayehisi Upweke Tena

Wakati Ambapo Hakuna Mtu Atakayehisi Upweke Tena

Wakati Ambapo Hakuna Mtu Atakayehisi Upweke Tena

KITABU cha Mwanzo 2:18 kinasema kwamba mwanadamu wa kwanza alipoumbwa, “Yehova Mungu a[li]endelea kusema: ‘Si vema huyo mwanamume aendelee kuwa peke yake. Nitamfanyia msaidizi, awe kikamilisho chake.’” Wanadamu waliumbwa wawe pamoja na wengine na kutegemeana.

Rafiki bora zaidi tunayeweza kumpata ni Yehova Mungu. Mtume Paulo anakiri kwamba Yehova ni “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote.” (2 Wakorintho 1:3, 4) Yehova mwenyewe huhuzunishwa anapoona yeyote kati ya watumishi wake akiteseka. Yeye ni Mungu mwenye hisia-mwenzi. “Kwa maana yeye mwenyewe analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” (Zaburi 103:14) Je, huvutiwi na Yehova Mungu na kuthamini uangalifu wake wenye upendo, fadhili, na jinsi anavyotujali?

Yehova Huwategemeza Wapweke

Watumishi wa zamani wa Mungu walikabili hali zilizowafanya wahisi upweke. Yehova aliwategemeza na kuwafariji. Kwa mfano, mfikirie Yeremia, aliyepata utume wa kuwa nabii akiwa kijana. Kati ya watu 40 walioandika Biblia, yaelekea Yeremia ndiye aliyeeleza mengi zaidi kuhusu hisia zake. Aliogopa na kuhisi kwamba hakustahili kupokea mgawo wake wa kwanza kutoka kwa Mungu. (Yeremia 1:6) Ili kutimiza mgawo wake, alihitaji kumtegemea Yehova kabisa. Kwa kweli, alimwona Yehova kuwa “mwenye nguvu anayetisha.”—Yeremia 1:18, 19; 20:11.

Miaka 300 hivi kabla ya wakati wa Yeremia, Malkia Yezebeli aliapa kumwua Eliya aliposikia kuhusu kuuawa kwa manabii wake wa Baali. Eliya alikimbia kilometa zipatazo 450 hadi Horebu katika Rasi ya Sinai. Kisha akaingia pangoni ili kukaa humo usiku, naye Yehova Mungu akamwuliza hivi: “Una kazi gani hapa, Eliya?” Eliya akaeleza kwamba anahisi kuwa yeye peke yake ndiye mwabudu wa Yehova katika Israeli yote, nabii pekee aliyekuwa na bidii kwa ajili ya utumishi wa Mungu. Yehova alimhakikishia kwamba hakuwa peke yake. Yehova alikuwa pamoja naye. Waisraeli wenzake 7,000 walikuwa pamoja naye pia, ingawa Eliya hakujua. Yehova alimfariji, akamtuliza Eliya na kuimarisha imani yake. Alimchochea Eliya, na kumtia moyo asiuache mgawo wake. (1 Wafalme 19:4, 9-12, 15-18) Tukihisi upweke au kuhisi kwamba hatufai, kama alivyohisi Eliya, sisi pia tunaweza kumwomba Yehova atuimarishe. Pia, kwa kutumia utambuzi, wazee Wakristo wanaweza kuwafariji wale walio waaminifu, wakiwasaidia kuona sehemu wanayotimiza katika kusudi la Mungu.—1 Wathesalonike 5:14.

Kutokana na mfano huo na mingine mingi, tunaweza kuona kwamba Yehova yuko tayari kuwategemeza na kuwafariji kwa upendo wale wanaohisi upweke. Naam, “Yehova atakuwa kilele salama kwa ajili ya mtu yeyote aliyekandamizwa, kilele salama wakati wa taabu.”—Zaburi 9:9; 46:1; Nahumu 1:7.

Mtu Aliyekuwa na Hisia Nyingi na Huruma

Yesu Kristo alimwiga Yehova kwa kudhibiti hisia zake kikamili. Luka anaeleza jinsi Yesu alivyofanya alipoukaribia umati uliokuwa ukienda kumzika mfu katika jiji la Naini: “Kulikuwa na mfu akiwa anapelekwa nje, mwana mzaliwa-pekee wa mama yake. . . . Bwana alipomwona akamsikitikia, akamwambia: ‘Acha kulia.’ Ndipo akakaribia na kuligusa sanduku, na wachukuzi wakasimama tuli, naye akasema: ‘Kijana, ninakuambia, Inuka!’ Na huyo mfu akaketi na kuanza kusema, naye akamkabidhi kwa mama yake.” (Luka 7:12-15) Hisia za Yesu zilichochewa sana. Alikuwa mwenye huruma. Hebu wazia shangwe ya mjane huyo mpweke Yesu alipomfufua mwana wake! Upweke wake uliisha.

Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yesu anaweza “kuusikitikia udhaifu wetu.” Yeye huwasikitikia watu wenye upweke ambao ni wanyofu. Ama kweli, kupitia yeye tunaweza “[kupokea] rehema na kupata fadhili zisizostahiliwa kuwa msaada kwa wakati unaofaa.” (Waebrania 4:15, 16) Kwa kumwiga Yesu, tunaweza kuwasikitikia walio na huzuni, wanaoteseka, na wapweke. Tukiwasaidia wengine, hatutahisi upweke. Lakini, bado kuna njia nyingine inayoweza kutusaidia kushinda hisia mbaya za upweke.

Neno la Yehova Linaweza Kutusaidia Kushinda Upweke

Wengi wameona kwamba “kupitia faraja kutokana na Maandiko [tuna] tumaini.” Neno la Mungu lina mashauri mengi yanayoweza kutusaidia kushinda upweke. (Waroma 15:4; Zaburi 32:8) Kwa mfano, Neno la Mungu hutuhimiza ‘tusijifikirie wenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.’ (Waroma 12:3) Ili tutumie shauri hilo, huenda tukahitaji kubadili maoni yetu. Kuwa na unyenyekevu na kiasi, yaani kutambua uwezo wetu, kutatusaidia kuwa na usawaziko na kutotazamia mambo yanayopita uwezo wetu. Neno la Mungu hutushauri pia tupendezwe kikweli na wengine. (Wafilipi 2:4) Unapojitahidi kupendezwa na kuwahangaikia wengine, wao pia watapendezwa na kukuhangaikia. Ushirika huo mzuri huondoa upweke na hufanya maisha yetu yawe na kusudi.

Biblia hututia moyo sisi Wakristo ‘tusiache kukusanyika pamoja sisi wenyewe.’ (Waebrania 10:24, 25) Kwa hiyo, shiriki katika utendaji wenye manufaa, kama vile kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova kwa ukawaida. Bila shaka, mikutano ya Kikristo inaweza kuchangia afya yetu ya kiroho, kihisia, na kimwili. Kuzungumza na wengine kuhusu habari njema za Ufalme wa Mungu kunaweza kufanya maisha yetu yawe na furaha. Kufanya hivyo hutufanya tukazie fikira zetu mambo yanayofaa, huimarisha imani yetu, na kulinda tumaini letu.—Waefeso 6:14-17.

Mkaribie Yehova katika sala. Daudi alisihi hivi: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza.” (Zaburi 55:22) Ukijifunza Neno la Mungu, utakuwa na furaha. (Zaburi 1:1-3) Ukilemewa na hisia za upweke, tafakari upendo wa Yehova unaofunuliwa katika Neno lake. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Nafsi yangu imekuwa ikishikamana na mavumbi. Nihifadhi hai kulingana na neno lako.”—Zaburi 119:25.

Wakati Ambapo Hakuna Mtu Atakayesema, “Mimi Ni Mpweke”

Yehova Mungu ameahidi ulimwengu mpya usio na mahangaiko, mambo yenye kufadhaisha, na hisia mbaya. Biblia inasema hivi: “Atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:4) Naam, baadhi ya mambo hayo ya zamani yatakayopitilia mbali ni maumivu ya kimwili, ya kiakili, na ya kihisia yanayotupata leo.

Dunia itajaa watu wenye urafiki, ambao wataboresha maisha yetu. Yehova atautumia Ufalme wake wa mbinguni ulio mikononi mwa Yesu Kristo kutuondolea kabisa upweke tunaohisi. Atatupatia mambo mapya na ya ajabu ya kufanya katika paradiso duniani. Hivi karibuni, siku itafika ambapo hatutasema tena kamwe, “Ninahisi upweke.”

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Yehova atatusaidia tusihisi upweke, hata tunapokuwa peke yetu

[Picha katika ukurasa wa 10]

Tunajifunza nini kutokana na masimulizi ya Biblia kuhusu Yeremia na Eliya?