Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Magumu ya Vita Yalinitayarisha kwa Ajili ya Maisha

Magumu ya Vita Yalinitayarisha kwa Ajili ya Maisha

Magumu ya Vita Yalinitayarisha kwa Ajili ya Maisha

SIMULIZI LA ERNST KRÖMER

“Hiki ndicho chumba chenu.” Hivyo ndivyo mimi na mwenzangu tulivyokaribishwa Gabon, Afrika Magharibi. Kulikuwa na nafasi ya godoro tu. Tuliishi katika chumba hicho kwa miezi sita.

MAISHA niliyoishi katika shamba moja wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu yalinitayarisha kuishi katika hali ngumu. Vita vilipozuka mwaka wa 1939, Ujerumani ya Nazi ilinyakua nchi ya Poland mara moja. Nilikuwa na umri wa miaka minne wakati huo. Mbali na wazazi wangu, nilikuwa na dada wawili wakubwa na ndugu na dada mdogo. Baba alituambia tuwe tayari kwa ajili ya nyakati ngumu iwapo Ujerumani ingeshindwa vitani.

Tuliishi Löwenstein, kijiji kidogo cha Ujerumani huko Lower Silesia, ambayo sasa ni sehemu ya Poland. Tulipanda nafaka na kufuga wanyama katika shamba letu la ekari 60 hivi. Baba alikuwa pia msimamizi wa wakulima katika eneo hilo. Wanazi walipoanza kusimamia eneo hilo, walimtumia baba kuwatayarisha wakulima ili waunge mkono vita.

Baba alikuwa ametumikia jeshini wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, na sasa kazi aliyopewa na Wanazi katika serikali ilimwokoa asiende vitani. Wazazi wangu walikuwa wamejiuzulu kanisani kwa miaka mingi kwa sababu walikatishwa tamaa na matendo ya makasisi wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Kwa hiyo, nilipokuwa nikikua sikupendezwa na dini hata kidogo.

Nilianza shule mwaka wa 1941, lakini niliichukia na niliona kwamba ningeweza kufanya mambo mengine ya kupendeza badala ya kutazama ubao darasani. Mwishoni mwa mwaka 1944, miezi sita tu kabla ya vita kwisha, Breslau (ambalo sasa ni Wrocław) jiji kuu la Lower Silesia, lilivamiwa na Warusi. Jumamosi moja jioni, tuliona mwangaza mkali ukitoka kwenye jiji hilo lililokuwa umbali wa kilometa 50, ambao ulisababishwa na mizinga na milipuko ya mabomu yaliyorushwa na ndege. Muda si muda ikatubidi tukimbilie milimani. Vita vilipokwisha, tulirudi nyumbani huko Löwenstein.

Baada ya Vita

Baada ya vita kulikuwa na nyakati ngumu. Wanawake walibakwa na kulikuwa na uporaji kila siku. Mifugo yetu mingi iliibwa.

Baba alikamatwa mnamo Julai mwaka wa 1945. Baada ya kuhojiwa kikatili usiku, kwa siku saba, aliachiliwa. Miezi mitatu baadaye alikamatwa tena. Hatukumwona tena baada ya hapo. Wanaume wawili kutoka Poland walinyakua shamba letu. Mnamo Aprili 1946 Wajerumani wote katika kijiji chetu waliambiwa waondoke na kuchukua tu vitu ambavyo wangeweza kubeba.

Mama alikuwa amejitayarishia hilo, kwa hiyo hakuwa na wasiwasi. Alikuwa na kikapu kikubwa chenye magurudumu kilichokuwa na matandiko, na kila mmoja wetu alikuwa na mfuko uliojaa vitu tulivyohitaji. Askari wa Poland walituingiza ndani ya mabehewa ya mifugo, watu 30 wakiingizwa katika kila behewa. Majuma mawili baadaye, tulifika kaskazini-magharibi mwa Ujerumani, karibu na Uholanzi.

Familia yetu yenye watu 19, kutia ndani watu wa ukoo, ilipewa vyumba viwili na serikali kwenye shamba moja lililokuwa kilometa nane hivi kutoka Quakenbrück. Baadaye, baadhi ya watu wetu wa ukoo walihamia kwa wakulima wengine, hivyo tukaacha kusongamana sana.

Mama alijitoa mhanga kwa ajili yetu, mara nyingi akikosa kula ili tupate chakula. Hatukuwa na kuni katika majira ya kwanza ya baridi kali. Kuta na dari zilifunikwa na tabaka kubwa la barafu na vyumba vyetu vilikuwa kama pango la barafu. Uzuri ni kwamba tulikuwa na matandiko yaliyotupasha joto, hivyo hatukuumia sana.

Kukutana na Mashahidi

Wapata mwaka wa 1949, Mama alipokea gazeti la Mnara wa Mlinzi kutoka kwa shangazi yangu mmoja. Makala moja katika gazeti hilo ilimkumbusha kwamba wakati wa vita alikuwa amesikia kwenye redio Hitler akishutumu ‘kikundi cha watu’ waliokuwa wametabiri kuanguka kwa Ujerumani. Mama hakujua watu hao ni akina nani. Aliposoma kwenye Mnara wa Mlinzi kwamba walikuwa Mashahidi wa Yehova, alipendezwa na kuamua kujifunza Biblia pamoja nao.

Siku moja katika Aprili 1954, niliwapata wenzi wa ndoa Mashahidi wakimfunza Mama. Baada ya funzo, nilikubali kupokea kijitabu Can You Live Forever in Happiness on Earth? na kuandikisha gazeti la Mnara wa Mlinzi. Niliposoma kijitabu hicho, nilisadiki kwamba nimepata kweli. Kwa hiyo nikampa mwajiri wangu akisome. Nilipomwuliza maoni yake kukihusu, alisema: “Maelezo yake ni mazuri sana, lakini ni vigumu kuyaamini. Siwezi kuyaamini.”

Nikamwambia, “Nina hakika huu ndio ukweli, na nitaufuata.” Kisha, akasema hivi akitikisa kichwa: “Ujumbe huu ni wa mtu mpole. Wewe ni mkatili sana, huwezi kuwa Shahidi.” Lakini nikaanza kufanya mabadiliko maishani.

Ijapokuwa hakukuwa na Mashahidi katika eneo hilo, nilijifunza peke yangu na kuendesha baiskeli kwa kilometa kumi hivi kila juma ili kuhudhuria mikutano. Baadaye nilihudhuria kusanyiko la mzunguko, ambapo makutaniko kadhaa ya Mashahidi yalikusanyika kwa ajili ya ibada. Nikiwa huko nilihubiri hadharani pamoja na wengine kwa mara ya kwanza. Muda si muda nikaanza kufanya hivyo kwa ukawaida. Mnamo Julai 14, 1954, mimi na Mama tukabatizwa. Baadaye, nyanya yangu wa upande wa mama akawa Shahidi pia akiwa na umri wa miaka 80.

Kwa kuwa kazi yangu shambani ilichukua wakati mwingi sana, niliiacha na kupata kazi nyingine kwenye hifadhi ya misitu. Baadaye familia yetu ilihamia Reutlingen, mji mdogo karibu na Stuttgart. Tulipokuwa huko dada yangu mdogo Ingrid akawa Shahidi pia, na ni yeye tu kati ya ndugu na dada zangu aliyepata kuwa Shahidi.

Kuhubiri Wakati Wote

Kwa kuwa Baba alikuwa ametoweka kwa muda mrefu, mnamo mwaka wa 1957, Mama aliandikisha kisheria kwamba Baba amekufa. Kwa hiyo, alianza kupata malipo ya uzeeni yaliyomwezesha kuishi bila msaada wangu wa kifedha. Kwa kuwa sasa sikuwa na madaraka hayo ya kifamilia, nilipata kazi ya muda na mnamo Aprili 1957 nikaanza kuhubiri wakati wote nikiwa painia. Baadaye nilipokea mgawo wa kutumikia nikiwa painia wa pekee. Shahidi mmoja aliposikia hivyo, aliniita ofisini mwake na kusema: “Nina hakika utahitaji msaada.” Kisha akanipa maki 500 za Ujerumani. Nilizitumia kununua nguo nilizohitaji na bado nikabaki na maki 200.

Mnamo mwaka wa 1960, nilijitolea kutumikia huko Austria, ambako nilifurahia kuhubiri katika kijiji kidogo cha Scheibbs, na kwa muda mfupi katika jiji la Linz, lakini baadaye mwaka huohuo, nikapata msiba nilipokuwa nikiendesha pikipiki, nikavunjika mguu wa kulia. Baada ya kufanyiwa upasuaji mara kadhaa, niliweza kuendelea na mgawo wangu. Hata hivyo, mnamo 1962, ilinibidi kurudi nyumbani huko Reutlingen ili kushughulikia matatizo ya uhamaji. Nilipokuwa huko, nilifanyiwa upasuaji mwingine kuondoa chuma kilichokuwa kimewekwa ndani ya mguu wangu. Niliacha upainia kwa miezi sita ili kutafuta pesa za kulipia gharama za matibabu.

Mwangalizi asafiriye alipotembelea kutaniko nililokuwa nikitumikia, alipendekeza kwamba niombe kutumikia katika ofisi ya tawi ya Mashahidi ambayo wakati huo ilikuwa huko Wiesbaden, Ujerumani. Nilifanya hivyo, na majuma mawili baadaye, nilipokea telegramu iliyosema kwamba ninapaswa kufika huko haraka iwezekanavyo. Juma moja baadaye katika Mei 1963, nilikuwa nikifanya kazi ya kuchapisha magazeti kwenye ofisi ya tawi ya Ujerumani, inayoitwa Betheli.

Nilijifunza kwa Bidii

Betheli ndipo mahali pazuri zaidi nilipowahi kuishi, na nilijizoeza kufanya kazi ngumu haraka. Mwaka wa 1965, nilienda Hispania kupeleka vitabu vya Biblia kisiri kwa kuwa kazi ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku huko. Safari hiyo ilinichochea kujifunza lugha nyingine, basi nikaamua kujifunza Kiingereza. Nilitumia kila nafasi kujifunza. Wakati huo kikundi cha kwanza cha Kiingereza kilianzishwa huko Ujerumani, hivyo nikajiunga nacho. Mara ya kwanza nilipojifunza makala ya funzo la Mnara wa Mlinzi katika Kiingereza, nilitumia saa saba. Nilipotumia saa tano tu mara ya pili, nilijua kwamba ninafanya maendeleo.

Mwaka wa 1966, nilialikwa kuhudhuria darasa la 43 la shule ya Gileadi huko Marekani ambayo huwazoeza wahudumu wa Mashahidi wa Yehova kwa ajili ya kazi ya umishonari. Kisha, baada ya kuhitimu, mimi na Günther Reschke tulitumwa huko Gabon, Afrika Magharibi, mnamo Aprili 1967. Tulipofika Libreville, jiji kuu la Gabon, tulikaa kwenye kile chumba kidogo kilichotajwa katika utangulizi, na tuliweka nguo zetu katika chumba cha kulia chakula. Miezi sita baadaye tulihamia makao mengine ya mishonari.

Huko Gabon, tatizo langu kubwa lilikuwa kujifunza Kifaransa. Hatimaye, baada ya jitihada nyingi nikakijua kwa kiasi fulani. Kisha mwaka wa 1970, kazi yetu ya kuhubiri ikapigwa marufuku kwa ghafula nchini Gabon, nasi mishonari tukaamuriwa tuondoke nchini humo kabla ya majuma mawili kwisha.

Nilihamia Jamhuri ya Afrika ya Kati

Nilitumwa katika Jamhuri ya Afrika ya Kati pamoja na mishonari wengine. Kifaransa kilikuwa lugha rasmi ya nchi hiyo, lakini tulilazimika kujifunza Kisango ili tuweze kuwahubiria watu wengi. Tulitumwa tuanzishe makao ya mishonari katika mji wa Bambari, karibu kilometa 300 kutoka Bangui, jiji kuu la nchi hiyo. Ingawa mji wa Bambari haukuwa na stima wala maji ya mabomba, makutaniko mawili ya huko yalihitaji msaada wetu. Mambo niliyojionea wakati wa vita huko Ulaya yalinisaidia sana kuvumilia hali za maisha huko Bambari na vilevile sehemu nyingine tulizoishi baadaye.

Baada ya kutumikia kwa miaka miwili huko Bambari, nilipewa mgawo wa kutembelea makutaniko nikiwa mwangalizi asafiriye. Kulikuwa na makutaniko 40 hivi nchini humo, nami nilikaa kwa juma moja na kila kutaniko nililogawiwa. Nilikuwa na gari dogo, lakini barabara za vumbi zilipokuwa mbovu, nilitumia usafiri wa umma.

Bangui ndipo palipokuwa mahali pekee pa kurekebishia magari nchini humo. Kwa kuwa nilihitaji kusafiri sana katika huduma yangu, nilinunua vifaa fulani pamoja na vitabu vyenye mwongozo wa kurekebisha magari, hivyo mara nyingi nilikuwa nikijirekebishia gari langu. Wakati mmoja mwanzi wa beringi ya mtaimbo-endeshi ulivunjika na gari likakwama. Nyumba iliyokuwa karibu ilikuwa umbali wa kilometa 60 hivi kutoka nilipokuwa. Nilikata mti kutoka kwenye msitu na kutengeneza mwanzi wa beringi. Nikitumia mafuta mengi, niliuunganisha kwa waya kwenye mtaimbo-endeshi na kufaulu kuendelea na safari yangu.

Ilikuwa vigumu kutumikia katika maeneo ya mashambani kwa sababu ni wachache tu waliojua kusoma au kuandika. Katika kutaniko moja, ni mtu mmoja tu aliyejua kusoma na alikuwa na kigugumizi. Funzo la Mnara wa Mlinzi lilikuwa gumu sana, lakini imani yangu iliimarishwa nilipoona kutaniko hilo likijitahidi sana kuelewa habari zilizozungumziwa.

Baadaye niliwauliza jinsi walivyofaidika ikiwa hawakuzielewa habari hizo vizuri. Jibu walilotoa lilitia moyo sana: “Sisi hutiana moyo.”—Waebrania 10:23-25.

Ingawa wengi wa ndugu zangu Wakristo hawakujua kusoma na kuandika, walinifunza mengi juu ya maisha na jinsi ya kuishi. Nilianza kuthamini umuhimu wa shauri la Maandiko la ‘kuwaona wengine kuwa bora.’ (Wafilipi 2:3) Ndugu zangu Waafrika walinifundisha mengi kuhusu upendo, fadhili, na ukarimu na jinsi ya kuishi mashambani. Sasa nilielewa kwa ukamili maneno ambayo Ndugu Nathan Knorr, ambaye wakati huo alikuwa msimamizi wa Shule ya Gileadi, alisema katika hotuba yake ya kutuaga wakati wa kufuzu kutoka shule hiyo. Alisema: “Tuwe wanyenyekevu, tusifikiri tunajua kila kitu. Hatujui mambo yote. Tuna mengi sana ya kujifunza.”

Kuishi Katika Maeneo ya Mashambani ya Afrika

Niliishi na ndugu wenyeji nilipotembelea makutaniko mbalimbali. Kwa kawaida, juma la ziara yangu lilikuwa kipindi cha sherehe, hasa kwa watoto. Hiyo ni kwa sababu washiriki wa kutaniko nililotembelea walikuwa wakienda kuwinda au kuvua samaki ili kuhakikisha kuna chakula cha kumtosha kila mtu.

Nilipokuwa nikiishi na akina ndugu katika vibanda vyao, nilikula vyakula vingi kutia ndani mchwa na nyama ya tembo. Nyani waliliwa mara nyingi. Nguruwe wa mwituni na nungunungu hasa walikuwa watamu sana. Hata hivyo, kuna siku ambazo chakula hakikuwa kingi. Ilichukua muda kuzoea chakula hicho kipya, lakini hatimaye tumbo langu liliweza kumeng’enya karibu kila aina ya chakula. Nilijifunza kwamba kula papai pamoja na mbegu zake kunafaidi tumbo.

Mambo mengi yasiyotazamiwa yanaweza kutokea katika maeneo ya mashambani. Wakati mmoja nilidhaniwa kuwa mzuka unaoishi ndani ya maji. Watu wengine wanaamini kwamba mzuka unaweza kumvuta mtu na kumtumbukiza majini. Pindi moja nilipotoka kuoga mtoni, msichana mmoja aliyekuwa amekuja kuteka maji aliniona, akapiga mayowe na kutoroka. Shahidi mwenzangu alipojaribu kuwaeleza kwamba mimi ni mhubiri anayetembelea eneo hilo wala si mzuka, watu hawakuamini. Walisema, “Mzungu hawezi kamwe kuja hapa msituni.”

Mara nyingi nililala nje kwa kuwa kulikuwa na hewa safi. Nyakati zote nilibeba neti kwa sababu ilinilinda kutokana na nyoka, nge, panya, na vinginevyo. Neti ilinilinda mara kadhaa nilipovamiwa na siafu. Usiku mmoja nilimulika neti kwa tochi nikaona siafu wengi. Nilitoroka kwa sababu ingawa siafu ni wadogo, wanaweza hata kuwaua simba.

Nilipokuwa katika eneo la kusini mwa Jamhuri ya Afrika ya Kati, karibu na Mto Kongo, niliwahubiria Mbilikimo ambao ni wawindaji hodari na wanajua vyakula vinavyoweza kuliwa na visivyoweza kuliwa. Baadhi yao huzungumza Kisango, na walifurahi kusikiliza. Walikubali tuwarudie, lakini tuliporudi hatukuwapata kwani walikuwa wamehamia eneo lingine. Wakati huo hakuna Mbilikimo aliyepata kuwa Shahidi, lakini baadaye nilipata kujua kwamba baadhi yao wamekuwa Mashahidi katika Jamhuri ya Kongo.

Nilitumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko katika Jamhuri ya Afrika ya Kati kwa miaka mitano. Nilisafiri kotekote nchini, mara nyingi nikitembelea makutaniko yaliyo mashambani.

Kutumikia Katika Ofisi ya Tawi ya Nigeria

Mnamo Mei 1977, nilialikwa kutumikia katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Lagos, Nigeria. Wakati huo, nchi hiyo ya Afrika yenye idadi kubwa zaidi ya watu ilikuwa na Mashahidi wapatao 100,000 na 80 hivi walitumikia katika ofisi ya tawi. Nilipewa kazi ya kurekebisha na kutunza magari katika gereji.

Mwaka wa 1979, nilirudia kazi ya kilimo niliyokuwa nimefanya nilipokuwa nikikua huko Ulaya. Shamba lililokuzwa chakula cha wafanyakazi wa ofisi ya tawi lilikuwa Ilaro, kilometa 80 hivi kutoka Lagos. Nilijifunza kwamba kazi ya kilimo katika misitu ya mvua ya kitropiki inatofautiana sana na ile ya Ulaya. Baada ya kufanya kazi huko kwa miaka mitatu na nusu, nilirudi Lagos na kufanya kazi tena katika gereji.

Mnamo mwaka wa 1986, nilipelekwa Igieduma karibu kilometa 360 kutoka Lagos, ambapo makao mapya makubwa ya ofisi ya tawi yalikuwa yanajengwa. Makao hayo yaliwekwa wakfu mnamo Januari 1990. Yana matbaa, shamba dogo, na majengo ya makazi kwa ajili ya watu zaidi ya 500. Makao hayo yako kwenye uwanja wa ekari 140 na yamezingirwa kwa ukuta wenye urefu wa karibu meta 2. Kwa sasa ninasimamia shamba na utunzaji wa uwanja, na kazi hiyo inafanywa na wafanyakazi 35 hivi.

Kwa miaka 27 hivi, nimeishi Nigeria na nimefurahia migawo yangu mbalimbali katika ofisi ya tawi. Ninafurahi kwamba Mama yangu anaendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova na kwamba dada yangu mdogo Ingrid, aliyetumikia kwa miaka 14 akiwa painia wa pekee, bado anamtumikia Yehova pamoja na mume wake.

Yajapokuwa magumu ambayo nimekabili, nimefurahia sana kumtumikia Yehova pamoja na ndugu zangu wa kiroho katika Afrika Magharibi. Ninashukuru kwa sababu nimekuwa na afya njema mpaka sasa na ninasali kwamba mambo yazidi kuwa hivyo ili niendelee kwa bidii kumtumikia Mungu wetu mkuu, Yehova.

[Ramani katika ukurasa wa 21]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Nigeria

Jamhuri ya Afrika ya Kati

Gabon

[Hisani]

Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Nikiwa na mama yangu, Gertrud, na dada yangu Ingrid, mwaka wa 1939

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nikitumikia nikiwa mishonari huko Gabon

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nikiwa katika Jamhuri ya Afrika ya Kati, niliishi katika vijiji kama hiki