Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nifanyeje Mpenzi Wangu Aache Kunitesa?

Nifanyeje Mpenzi Wangu Aache Kunitesa?

Vijana Huuliza . . .

Nifanyeje Mpenzi Wangu Aache Kunitesa?

“Leo mpenzi wangu alinipiga kwa mara ya kwanza. Aliomba msamaha, lakini sijui nifanyeje sasa.”—Stella. *

KULINGANA na The Journal of the American Medical Association, “inakadiriwa kwamba msichana 1 kati ya kila wasichana 5 walio shuleni ameripoti kutendewa vibaya kimwili na/au kingono na mpenzi wake.” Uchunguzi uliofanywa Ujerumani miongoni mwa vijana wenye umri wa kati ya miaka 17 na 20, ulionyesha kwamba zaidi ya asilimia 25 ya wasichana waliripoti kwamba walikuwa wamelazimishwa kujihusisha katika mahusiano ya kingono yanayotia ndani kutendewa vibaya kimwili, kutishwa, kupewa dawa za kulevya, au pombe. Kulingana na uchunguzi mmoja huko Marekani, asilimia 40 ya vijana waliohojiwa walisema kwamba wameona wanafunzi wenzao “wakiwatukana wapenzi wao kikatili.” *

Je, wewe ni msichana anayepanga kuolewa na mtu fulani anayekutukana, anayekupigia kelele, anayekusukuma, au kukuzaba kofi? Makala iliyotangulia katika mfululizo huu ilionyesha kwamba matendo kama hayo ni ya kawaida sana. * Pia ilionyesha kwamba Yehova Mungu hakubali matusi au mwenendo mbaya na kwamba wanaodhulumiwa hawapaswi kuona tabia hiyo kuwa ya kawaida wala hawapaswi kujilaumu. (Waefeso 4:31) Hata hivyo, si rahisi kujua la kufanya unapokuwa katika hali hiyo. Huenda bado unampenda mpenzi wako ingawa ana tabia mbaya. Au hata huenda ukahofia kile atakachofanya ukimchambua. Unapaswa kufanya nini?

Chunguza Hali Yako

Kwanza unahitaji kutulia na kuchunguza vizuri yale yaliyotukia. (Mhubiri 2:14) Je, kweli umetukanwa? Je, mpenzi wako alitenda kwa ukatili kimakusudi, au je, alikuwa tu ‘akisema bila kufikiri’? (Methali 12:18) Jambo hilo limetukia mara ngapi? Je, limetokea mara moja tu hivi kwamba unaweza kulipuuza? Au je, ana mazoea ya kusema mambo ya kukushushia heshima au yanayoudhi?

Ikiwa huna hakika kuhusu hisia zako, zungumza na mtu mwingine mwenye umri mkubwa na mwenye hekima zaidi wala si mtu wa rika lako. Labda unaweza kuzungumza na wazazi wako au Mkristo mkomavu. Mazungumzo hayo yanaweza kukusaidia kujua ikiwa unahangaika bure au ikiwa kuna tatizo kubwa.

Ikiwa unaona hakuna hatari, unaweza kupanga kuzungumza na mpenzi wako kuhusu jambo hilo. (Methali 25:9) Mwambie kwa utulivu jinsi tabia yake inavyokuathiri. Mwambie kilichokuudhi hasa. Sema waziwazi mambo ambayo huwezi kuyavumilia. Anaonaje unapomwambia mambo hayo? Je, anapuuza maoni yako au hata kuropoka kwa hasira? Hiyo inaonyesha wazi kwamba hana nia ya kubadilika.

Hata hivyo, vipi akionyesha unyenyekevu wa Kikristo na kusikitika kikweli? Basi, huenda ikawezekana kurekebisha uhusiano wenu. Hata hivyo, jihadhari! Mara nyingi watu wanaowashambulia wengine kwa maneno hujifanya kwamba wamesikitika sana baada ya kumuumiza mtu, lakini wanarudia kufanya hivyo wanapoudhika tena. Baada ya muda itajulikana wazi ikiwa kweli ana nia ya kubadilika. Jambo moja linaloweza kuonyesha kwamba anataka kubadilika ni ikiwa yuko tayari kuomba msaada kutoka kwa wazee Wakristo.—Yakobo 5:14-16.

Tambua kwamba “wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Hata ukitafuta namna gani, hutapata mtu mkamilifu. Wenzi wote wa ndoa hupata “dhiki katika mwili” kwa kiasi fulani kwa sababu ya kutokamilika. (1 Wakorintho 7:28) Hatimaye, itakubidi uamue ikiwa unaweza kuvumilia kasoro zake unapoishi naye. Njia bora ya kuamua jambo hilo ni kuruhusu wakati upite.

Jeuri Inapozuka

Hata hivyo, mambo huwa tofauti wakati mtu anayekushambulia kwa maneno anapotumia matusi, vitisho vya jeuri au anapokutesa kimwili labda kwa kukusukuma, au kukuzaba kofi. Hiyo inaonyesha kwamba hana sifa ya kujizuia; na kwamba hata anaweza kufanya matendo mabaya zaidi ya jeuri.

Haingefaa kwa watu wawili ambao hawajafunga ndoa kuwa peke yao. Lakini, ukijikuta peke yako pamoja na mtu mwenye jeuri, ‘usimlipe uovu kwa uovu.’ (Waroma 12:17) Kumbuka: “Jibu, linapokuwa la upole, hugeuza ghadhabu, lakini neno linaloumiza hufanya hasira ipande.” (Methali 15:1) Tulia. Mwombe akupeleke nyumbani. Ikiwa ni lazima, nenda zako—au hata ukimbie!

Mwanamke anaweza kufanya nini mwanamume akijaribu kumlazimisha kufanya ngono? Bila shaka, ni jambo la hekima kwa watu wanaochumbiana kuweka mipaka kuhusu namna ya kuonyeshana mahaba tangu mwanzo wa uchumba wao. (1 Wathesalonike 4:3-5) Kijana akimshurutisha msichana avunje kanuni za Biblia, msichana huyo anapaswa kumweleza waziwazi kabisa kwamba hatakubaliana naye. (Mwanzo 39:7-13) “Usikubali hata kidogo,” anasihi Anne, aliyekubali kufanya ngono baada ya kushurutishwa. “Jiheshimu. Tafadhali, usifanye kosa hilo, hata kama unampenda kadiri gani!” Akipuuza kukataa kwako, mwambie kwamba lolote atakalofanya zaidi ya hapo litakuwa sawa na ubakaji. Akiendelea, tafuta msaada na ujaribu kumzuia kama ambavyo ungefanya ikiwa mtu mwingine angejaribu kukubaka. *

Vyovyote vile, shauri la Biblia kwenye Methali 22:24 linafaa: “Usishirikiane na mtu yeyote mwenye mazoea ya kukasirika; wala usiende pamoja na mtu wa mifoko ya ghadhabu.” Si lazima uendelee kuwa katika uhusiano na mtu anayekuumiza. Ni wazi kwamba lingekuwa jambo la kipumbavu kukutana na mwanamume anayekudhulumu ili kumjulisha kwamba umevunja uhusiano huo. Yaelekea jambo muhimu ni kuwajulisha wazazi wako yaliyotukia. Haikosi watakasirika na kuudhika kwa sababu umetendewa vibaya. Lakini wanaweza kukusaidia kujua hatua zaidi zinazopasa kuchukuliwa. *

Kujaribu Kumbadili

Kwa vyovyote vile, si jukumu lako kumbadili mpenzi wako. Irena anasema hivi: “Unafikiri kwamba unampenda, utaweza kushughulikia hali hiyo, na kwamba unaweza kumsaidia. Lakini huwezi.” Nadine pia anaungama hivi: “Sikuzote mimi hufikiri ninaweza kumbadili.” Ukweli ni kwamba, ni yeye tu anayeweza ‘kufanya upya akili yake’ na kubadilika. (Waroma 12:2) Na hilo ni jambo gumu litakalochukua muda mrefu.

Kwa hiyo, shikilia uamuzi wako na usikubali achezee hisia zako kwa njia yoyote ile. Jitahidi usiwe na uhusiano wa karibu pamoja naye, iwe ni kihisia au kimwili. Usimruhusu akubembeleze, akusihi, au hata akutishe ili mwendeleze uhusiano. Wakati Irena alipovunja uhusiano wake na mpenzi wake mwenye jeuri, mvulana huyo alitisha kujiua. Ni wazi kwamba mtu kama huyo anahitaji msaada, lakini si msaada wako. Njia bora ya kumsaidia ni kupinga kabisa mwenendo usiopatana na kanuni za Kikristo. Ikiwa anataka kubadilika, yuko huru kutafuta msaada.

Hata hivyo, watu fulani hufikiri kwamba ndoa inaweza kutatua tatizo hilo. Mtafiti mmoja anasema: “Wanawake wanaofunga ndoa na wanaume wadhalimu, na wanaume wanaofunga ndoa na wanawake wadhalimu mara nyingi hushangaa wanapotambua kwamba jeuri hiyo haikomi. Watu wengi huamini kwamba baada ya kutia sahihi cheti cha ndoa, matatizo yote yatatoweka. Hiyo si kweli hata kidogo.” Ukweli ni kwamba mara nyingi dhuluma inayoanza wakati wa uchumba huendelea katika ndoa.

Biblia inasema: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha.” (Methali 22:3) Ni vigumu kuvunja uhusiano na mtu unayempenda. Lakini mambo yatakuwa magumu zaidi ukijikuta katika ndoa yenye dhuluma. Isitoshe, usihofu kwamba hutapata mwenzi anayekufaa. Kwa kuwa umepata ujuzi, utajitahidi hata zaidi kutafuta mtu mwanana, mwenye fadhili, na mwenye kujizuia.

Kurudia Hali ya Kawaida

Unaweza kuhuzunika sana unapodhulumiwa kimwili au kwa maneno. Mary, aliyedhulumiwa, anashauri hivi: “Tafuta msaada, zungumza na mtu bila kukawia. Nilifikiri ningetatua tatizo hilo mwenyewe, lakini kuzungumza na watu kumenisaidia.” Zungumza na wazazi wako, rafiki mkomavu anayeaminika, au mzee Mkristo. *

Pia wengine wamejihisi vizuri kwa kufanya shughuli mbalimbali kama vile kusoma vitabu vinavyofaa, kucheza, au kufanya mambo wanayopenda. Irena anakumbuka hivi: “Jambo muhimu zaidi lilikuwa kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kikristo.”

Ni wazi kwamba Yehova hakubali maneno au matendo ya dhuluma. Kwa msaada wake, unaweza kujilinda dhidi ya dhuluma.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 4 Ijapokuwa wanaume na wanawake wanaweza kutukanwa na kutendewa vibaya kimwili, shirika la Vituo vya Marekani vya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa linasema kwamba “wanawake hujeruhiwa zaidi ya wanaume.” Vyovyote vile, ili kurahisisha habari hii, tutazungumza juu ya wanaume wanaowadhulumu wanawake.

^ fu. 5 Ona makala “Vijana Huuliza . . . Jamani! Mbona Ananitesa?” katika toleo la Amkeni! Mei 22, 2004.

^ fu. 15 Gazeti la Amkeni! la Machi 8, 1993, linazungumzia jinsi ya kuepuka kubakwa.

^ fu. 16 Katika visa fulani, kama vile majaribio ya ubakaji, huenda wazazi wako wakaamua kuripoti kisa hicho kwa polisi. Hilo linaweza kuwazuia wasichana wengine wasipatwe na hali hiyo yenye kusikitisha.

^ fu. 23 Katika visa vya mfadhaiko, huenda wengine wakaamua kutibiwa na daktari au mtaalamu mwingine wa akili.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Mara nyingi dhuluma inayoanza wakati wa uchumba huendelea katika ndoa

[Picha katika ukurasa wa 25]

Usilazimishwe kufanya mambo machafu