Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kupata Wapi Majibu?

Unaweza Kupata Wapi Majibu?

Unaweza Kupata Wapi Majibu?

JE, WEWE huudhika kwa sababu ya mjadala unaoendelea kuhusu mageuzi na uumbaji? Ikiwa ndivyo, kuna wengi kama wewe.

Kwa upande mmoja kuna wanasayansi wenye elimu ya juu na wasomi wengine ambao kwa kutumia lugha ya kitaalamu husisitiza kwamba ikiwa una elimu na maarifa, lazima ukubali nadharia ya mageuzi kuwa jambo hakika. Kwa upande mwingine, kuna washupavu wa kidini ambao hutumia semi zenye kuchochea hisia, huku wakisema kwamba ikiwa una imani ya kweli, lazima ukubaliane na maoni yao kuhusu uumbaji.

Maoni hayo yanayopita kiasi hayawavutii watu wengi wenye kutumia akili. Suala la kuwapo kwa Mungu haliwezi kujibiwa kwa maoni ya kishupavu yasiyoweza kuthibitishwa. Kumbuka kwamba hilo si suala la kujadiliwa tu wala si suala la kisayansi lisilo na maana yoyote. Mambo yanayohusika yanaweza kuathiri maisha yako ya sasa na ya baadaye.

Tatizo la Wanasayansi

Kama tulivyoona, kuna idadi kubwa ya wanasayansi maarufu wenye elimu ya juu ambao husema kwamba uthibitisho unaonyesha kuna Mbuni au Muumba. Pia wanasayansi fulani hutilia shaka msimamo wa kisayansi wa wenzao ambao hupinga kuwapo kwa Mungu.

Kwa mfano, mwanafizikia wa jiolojia, John R. Baumgardner alisema: “Chini ya hali hizo, mwanasayansi yeyote mnyoofu angewezaje kusema kwamba utata uliopo katika mifumo ya uhai ulitokea wenyewe tu? Kwa maoni yangu, kufanya hivyo ni kukiuka kabisa kanuni za sayansi.”

Mwanafizikia mashuhuri, Richard Feynman alitokeza wazo lingine linalohusu kufuata kanuni za sayansi. Katika hotuba yake ya ufunguzi kwenye chuo kikuu kimoja, alizungumzia “kanuni fulani hususa ya sayansi.” Alisema kwamba kanuni hiyo inahusisha “kukubali kwamba huenda umekosea.” Pia alisema: “Kufanya hivyo, ni wajibu wetu, hasa mbele ya wanasayansi wenzetu, na pia mbele ya watu wa kawaida.”

Ni mara ngapi wanamageuzi hutumia taarifa, “huenda nimekosea” wanapoeleza nadharia zao? Inasikitisha kwamba hawafanyi hivyo. Kwa kweli, unyenyekevu na uaminifu unapaswa kuwafanya wanasayansi wengi zaidi kukubali kwamba sayansi, inayohusisha elimu ya vitu vinavyoonekana tu, haiwezi kujibu maswali kuhusu kuwapo kwa Muumba. Vipi viongozi wa kidini wanaounga mkono nadharia zisizo za kweli kuhusu uumbaji?

Tatizo la Wanadini

Viongozi wa kidini pia wamekosa unyenyekevu na uaminifu. Kwani, uaminifu wao u wapi wanapodai kwamba Biblia hufundisha jambo ambalo haifundishi? Unyenyekevu wao u wapi wanapotanguliza maoni yao na desturi wanazopenda badala ya Biblia? Hivyo ndivyo watu wengi wanaodai kuamini nadharia zisizo za kweli kuhusu uumbaji hufanya.

Kwa mfano, watu hao husema kwamba ulimwengu wote mzima uliumbwa kwa siku sita za saa 24 miaka 6,000 hivi iliyopita. Kwa kufundisha hivyo, wanaipinga Biblia ambayo inasema kwamba Mungu aliumba mbingu na dunia “hapo mwanzo”—wakati fulani usiotajwa, kabla ya zile “siku” hususa za uumbaji kuanza. (Mwanzo 1:1) Masimulizi ya kitabu cha Mwanzo yanaonyesha kwamba neno “siku” linaweza kutumiwa kwa njia mbalimbali. Kwenye Mwanzo 2:4, kipindi chote kizima cha siku sita kinachotajwa katika sura inayotangulia kinaitwa siku moja tu. Kwa hiyo, hizo hazikuwa siku halisi zenye saa 24, bali zilikuwa vipindi virefu vya wakati. Yaonekana kila kipindi kilikuwa na urefu wa maelfu ya miaka.

Inasikitisha kwamba mara nyingi walimu wa dini hukosea wanapozungumzia imani. Baadhi yao hudai kwamba imani ni kuamini kitu kwa dhati pasipo uthibitisho wa kutosha. Watu wengi wanaotumia akili wanaona kwamba hiyo ni sawa na kudanganyika kwa urahisi. Biblia hufafanua imani kwa njia tofauti kabisa: “Imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.” (Waebrania 11:1) Kwa hiyo imani ya kweli si wepesi wa kudanganyika. Inategemea uthibitisho, uhakikisho unaopatana na akili.

Kwa hiyo, imani katika Mungu inategemea uthibitisho gani? Kuna mambo mawili yenye kusadikisha.

Kuchanganua Uthibitisho

Mtume Paulo alichochewa kuandika kwamba “sifa [za Mungu] ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu.” (Waroma 1:20) Kwa maelfu ya miaka, wanaume na wanawake wenye hekima wameona uthibitisho wa kuwapo kwa Mungu katika ulimwengu wa asili.

Kama tulivyoona, sayansi inaweza kutusaidia kuona uthibitisho wa kuwapo kwa Mungu. Kadiri tunavyozidi kujifunza kuhusu utata na utaratibu uliopo ulimwenguni, ndivyo tunavyokuwa na sababu nyingi zaidi za kumcha Yule aliyebuni vitu vyote. Wanasayansi kadhaa wanaukubali uthibitisho huo na kuuona kuwa wenye kusadikisha. Bila shaka, wanaweza kusema kwamba sayansi imewasaidia kumjua Mungu. Inaonekana kwamba wanasayansi wengine hawawezi kusadikishwa hata kuwe na uthibitisho mwingi kiasi gani. Vipi wewe?

Ikiwa ungependa kuchanganua uthibitisho uliopo kuhusu suala hilo, tunakuhimiza ufanye hivyo. Kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? kimekusudiwa kukusaidia kupata majibu ya maswali hayo muhimu. * Isitoshe, kitakusaidia kuzingatia uthibitisho mwingine wa kuwapo kwa Mungu: yaani, Biblia.

Biblia ina uthibitisho mwingi unaoonyesha kwamba iliongozwa na mtu mwenye akili nyingi kuliko mwanadamu. Kwa mfano, ina unabii mwingi, au historia iliyoandikwa zamani. Baadhi yake hufafanua hali zilizopo katika ulimwengu wa leo! (Mathayo 24:3, 6, 7; Luka 21:10, 11; 2 Timotheo 3:1-5) Wanadamu hawawezi kutabiri wakati ujao kwa usahihi. Ni nani isipokuwa Mungu ambaye anaweza kufanya hivyo?

Hata hivyo, mbali na kujibu maswali kuhusu kuwapo kwa Mungu, Biblia ina habari nyingine nyingi. Hutufundisha jina lake, hutueleza utu wake, na kutujulisha jinsi ambavyo amewashughulikia wanadamu kwa miaka mingi. Hata inafunua kusudi lake kwa ajili yetu. Katika mambo yote hayo, sayansi haiwezi kutupa majibu. Kwa kweli, sayansi ya wanadamu haiwezi kutupa tumaini lolote maishani mwetu. Wala haiwezi kutusaidia kuwa na maadili yanayofaa.

Msingi wa Maadili na Viwango Vinavyofaa

Kwa kusikitisha, inaonekana kwamba sayansi inayopendwa na watu fulani leo inapotosha maadili, viwango, na kanuni zinazofaa. Mtaalamu wa biolojia Richard Dawkins, anayepinga wazo la kuwapo kwa Mungu, alisema hivi: “Katika ulimwengu unaoongozwa na nguvu za asili na unaofanyiza chembe pacha za urithi, watu fulani wataumia, wengine watabahatika, na hakutakuwa na sababu yoyote inayopatana na akili ya kueleza jambo hilo wala haki yoyote.” Je, unaona maelezo hayo kuwa maoni yasiyofaa kuhusu ulimwengu? Je, hudhani kwamba wanadamu wanahitaji kanuni za maadili ambazo huwanufaisha watu wenye mwenendo unaofaa na kuwaadhibu wale wanaokosea?

Hapa kuna tofauti kuu kati ya maoni ya Biblia kuhusu wanadamu na maoni ya nadharia ya mageuzi. Neno la Mungu linakazia kwamba wanadamu ni sehemu muhimu ya uumbaji; nadharia ya mageuzi inadai kwamba wanadamu walitokea tu bila mpango. Biblia inaeleza kwamba wanadamu wameumbwa kwa mfano wa Mungu mwenye haki na upendo na kwamba wanaweza kuishi maisha safi kiadili na yenye kufurahisha; kwa kuwa nadharia ya mageuzi hudai kwamba viumbe hupigania kuendelea kuishi, haiwezi kueleza ni kwa nini wanadamu wana sifa ya upendo na ya kuwajali wengine.

Nadharia ya mageuzi haiwezi kuwapa wanadamu tumaini au kusudi lolote halisi. Biblia hueleza kusudi kuu la Muumba kwa ajili ya wakati wetu ujao. Anaeleza nia yake waziwazi anaposema hivi: “Nia niliyowawekea . . . ya kuwajalia matumaini mengi kwa siku za mbele.”—Yeremia 29:11, Verbum Bible.

Jifunze Kumhusu Muumba

Mtunga-zaburi mwenye hekima alikubali hivi kwa unyenyekevu: “Jueni kwamba Yehova ni Mungu. Yeye ndiye aliyetufanya, wala si sisi wenyewe.” (Zaburi 100:3) Kwa watu wengi wanaotumia akili, maneno hayo sahili ya mtunga-zaburi yana maana sana kuliko nadharia nyingi za leo zinazodai kwamba uhai wa mwanadamu ulitokea wenyewe tu.

Nyakati nyingine, sayansi ya leo huunga mkono dhana yenye kiburi ya kwamba mwanadamu anapaswa kuongozwa na akili na ujuzi wake mwenyewe. Inasikitisha kwamba dini mashuhuri zimefanya kosa hilohilo mara nyingi. Hata hivyo, akili ya mwanadamu imepungukiwa na itaendelea kupungukiwa. Ingawa mtume Paulo alikuwa na ujuzi mwingi katika mambo ya kiroho, alikuwa mnyenyekevu. Alisema hivi: “Maana sasa twaona kwa kioo, ginsi isiyo wazi; . . . Sasa najua kwa upungufu.”—1 Wakorintho 13:12, VB.

Bila shaka, imani ya kweli katika Mungu haitegemei sayansi ya kisasa. Lakini sayansi inaweza kuimarisha imani ya mtu anayechunguza mambo kwa makini. Imani ya kweli na hali ya kiroho ni muhimu ili kuwa na maisha yenye kuridhisha na yenye furaha. (Mathayo 5:3) Ukiitumia Biblia kupata kumjua Yehova kwa undani na kusudi lake kwa ajili ya wanadamu na dunia, utapata maana halisi ya maisha na msingi imara wa kuwa na tumaini.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Maoni ya wanasayansi wenyewe

Wanasayansi wengi wanatangaza waziwazi imani yao katika Muumba. Ingawa baadhi yao wana maoni yasiyo wazi kabisa kumhusu Mungu, bado wanakubali kwamba uthibitisho unaonyesha kuna Mbuni mwenye akili. Hebu fikiria maelezo yanayofuata:

“Nikiwa mwanasayansi, mimi huutazama ulimwengu, na kuona utaratibu wenye utata sana hivi kwamba ninachochewa kukata kauli kwamba utaratibu huo tata ulibuniwa kwa akili.”—ANDREW MCINTOSH, MWANAHISABATI, HUKO WALES, UINGEREZA

“Utata wa mambo ya asili huonyesha wazi kwamba kuna Muumba. Mifumo yote ya kibiolojia na kifizikia, inapoeleweka, inaonyesha utata wa ajabu.”—JOHN K. G. KRAMER, MTAALAMU WA BIOKEMIA, HUKO KANADA

“Ni wazi kwamba kuna utaratibu katika viumbe ulimwenguni. Vilitokana na Nguvu kuu zaidi ambazo mimi mwenyewe ninaziita Mungu. Hapa ndipo imani inapopatana na kweli ya kisayansi. Badala ya kuipinga sayansi, imani inaikamilisha, ikitoa maelezo sahili kuhusu ulimwengu wetu.”—JEAN DORST, MWANABIOLOJIA, HUKO UFARANSA

“Siwezi kuwazia kwamba ulimwengu na uhai wa wanadamu haukutokana na mtu fulani mwenye akili, au chanzo kingine cha kiroho chenye hisia, kisichohusisha mata na sheria zake.”—ANDREY DMITRIYEVICH SAKHAROV, MWANAFIZIKIA WA NYUKLIA, HUKO URUSI

“Kila mnyama amebuniwa kwa njia ya pekee ili aweze kuishi katika mazingira yake, nami sina budi kusema kwamba utata wa ubuni huo umetokana na Muumba, wala si nguvu za mageuzi zisizo na mpango.”—BOB HOSKEN, MTAALAMU WA BIOKEMIA, HUKO AUSTRALIA

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

Masimulizi ya Mwanzo yaungwa mkono

Gerald Schroeder, aliyekuwa profesa wa fizikia ya nyuklia, anaandika hivi: “Katika mistari 31, na kwa mamia machache ya maneno, Biblia inaeleza mambo yaliyotukia kwa zaidi ya miaka bilioni 16. Hayo ni matukio ambayo wanasayansi wameandika juu yake kwa kutumia mamilioni ya maneno. Muhtasari wa kutokea kwa uhai wa wanyama unapatikana katika sentensi nane za Biblia. Unapozingatia ufupi wa masimulizi hayo ya Biblia, maelezo na wakati wa matukio ya Mwanzo sura ya 1 yanapatana kwa njia ya ajabu sana na mavumbuzi ya sayansi ya leo, hasa tunapofikiria kwamba maelezo hayo yaliandikwa karne nyingi, au hata maelfu ya miaka iliyopita, na kwa hiyo hayakuathiriwa na mavumbuzi ya sayansi ya leo. Kwa hiyo, sayansi ya leo ndiyo imekuja kukubaliana na masimulizi ya Biblia kuhusu mwanzo wetu.”—THE SCIENCE OF GOD—THE CONVERGENCE OF SCIENTIFIC AND BIBLICAL WISDOM.

[Picha]

Biblia inafafanua vipindi sita vya uumbaji

[Picha katika ukurasa wa 12]

Biblia ina uthibitisho wenye nguvu unaoonyesha kwamba iliandikwa kwa mwongozo wa Mungu