Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mkumbuke Muumba Wako”

“Mkumbuke Muumba Wako”

“Mkumbuke Muumba Wako”

“Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako, kabla hazijaja siku zilizo mbaya, wala haijakaribia miaka utakaposema, Mimi sina furaha katika hiyo.” —Mhubiri 12:1,“Union Version.”

ANDIKO hilo lina hoja nzito sana. Utakuwa kijana mara moja tu maishani. Baadaye, utakumbuka miaka ya ujana kwa shangwe nyingi au majuto makubwa. Itakuwaje kwako? Unaweza kufanya nini ili uwe na maisha mazuri?

Kama ilivyonukuliwa juu, Biblia inasihi, “Mkumbuke Muumba wako.” Unawezaje kufanya hivyo? Kwa kutii sheria na kanuni za Mungu zinazopatikana katika Neno lake, Biblia. Hilo halimaanishi kwamba unapaswa kuishi maisha ya kidini yasiyopendeza ya kujinyima raha kabisa. Tofauti na hilo, kumkumbuka Muumba wako kutakuletea furaha nyingi sana. Hilo linawezekanaje?

Hebu fikiria umepewa gari na leseni ya kuliendesha. Sasa unakuwa na uhuru ambao unaweza kukuletea furaha nyingi. Hebu wazia sehemu mbalimbali unazoweza kutembelea! Hata hivyo, uhuru huo uliopata unahusisha daraka zito. Unapoendesha gari, ni lazima ufuate sheria na ishara za barabarani, na pia mwendo unaoruhusiwa na sheria. Je, sheria hizo zitakuzuia usifurahie kuendesha gari? La hasha! Badala yake, zinakulinda. Bila shaka, hutafurahia kupata msiba wa barabarani, sivyo?

Ndivyo ilivyo na uhuru ambao Muumba wako, Yehova Mungu, amekupa. Unapoendelea kufikia kuwa mtu mzima, anakuruhusu uchague jinsi utakavyotumia maisha yako. (Kumbukumbu la Torati 30:19; Methali 27:11) Ni pendeleo la ajabu kama nini! Lakini uhuru huo unaambatana na daraka zito. Katika Neno lake, Yehova ameweka ‘sheria za barabarani,’ yaani, viwango ambavyo anataka ufuate maishani. Je, viwango hivyo hukuzuia usiwe na furaha? Sivyo! Badala yake, vinakulinda kutokana na mfadhaiko na maumivu yanayowapata vijana wengi sana leo.

Federico, ambaye sasa ana umri wa miaka 30 na kitu, anajua ukweli wa hilo. Akiwa kijana, aliwaona wanashule wenzake wakijihusisha na mambo mengi ambayo alijua alipaswa kuyaepuka. Anasema: “Ilionekana kana kwamba wanafurahia maisha, lakini sikudhani walikuwa na furaha ya kweli.” Anapokumbuka wakati huo, Federico anafurahi kwamba kulikuwa na viwango vya Biblia vya kumwongoza alipokuwa akibalehe. Anasema: “Bila shaka, nilikabili matatizo sawa na vijana wengine. Lakini Biblia ilinilinda sana. Na nyakati zote nilipata msaada kutoka kwa Wakristo wenzangu. Nimepata furaha nyingi sana kwa kufuata viwango vya Biblia!”

Yehova Mungu anataka ufurahi—ufurahi sana. Hiyo si furaha bandia inayofunika taabu ya moyoni. Biblia inasema: “Furahia ujana wako, moyo wako, uchangamke wakati ungali kijana.” Lakini mstari huohuo wa Biblia unaongeza onyo hili: “Kumbuka kwamba Mungu atakuhukumu kadiri ya hayo yote.”—Mhubiri 11:9, Biblia Habari Njema.

Mkumbuke Muumba wako kwa kutumia kwa hekima uhuru aliokupa. Ukifanya hivyo, unaweza kuwa na hakika kwamba Muumba wako atakukumbuka na kukuwezesha ufurahi sana. Biblia inasema: “Baraka ya Yehova—hiyo ndiyo hutajirisha, naye haongezi maumivu pamoja nayo.”—Methali 10:22.

Ili kuwasaidia vijana kukabiliana na magumu ya kipindi cha kubalehe, Mashahidi wa Yehova wamechapisha kitabu chenye kurasa 320 kinachoitwa Maswali Ambayo Vijana Huuliza . . . Majibu Yafanyayo Kazi. Kufikia sasa, nakala milioni 34 hivi za kitabu hicho zimechapishwa katika lugha 77. Unaweza kupata kitabu hicho kwa kuwasiliana na Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Ili Ufanikiwe Unapobalehe

Tenga wakati wa kusoma Neno la Mungu

Shiriki kwa bidii katika huduma

Epuka mashirika mabaya

Dumisha mawasiliano mazuri na wazazi wako

[Hisani]

Brochure cover: Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.