Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuhangaikia Sura Kupita Kiasi

Kuhangaikia Sura Kupita Kiasi

Kuhangaikia Sura Kupita Kiasi

WENGI wetu tunapojiangalia kwenye kioo, tunatambua sehemu tunazohitaji kuboresha. Kwa hiyo, tunatengeneza mavazi au nywele zetu au kujipaka vipodozi kisha tunaendelea na shughuli zetu. Ni jambo la kawaida na linalofaa kuhangaikia sura yetu. Lakini watu wengine huhangaikia sura yao kupita kiasi na madaktari wanasema huo ni ugonjwa.

Kampuni ya The Merck Manual of Diagnosis and Therapy hufafanua ugonjwa huo kuwa “kuhangaikia kupita kiasi kasoro fulani katika sura ambako husababisha mfadhaiko mwingi au kumfanya mtu ajitenge na wengine, kuathiri kazi yake, au shughuli nyingine muhimu.” * Kwa kuwa watu wenye ugonjwa huo wanaweza kuwazia kwamba wana kasoro fulani au kuhangaikia sana kasoro ndogo, wao hudhani kwamba wana sura mbaya.

Profesa J. Kevin Thompson wa Chuo Kikuu cha South Florida, Marekani, anasema kwamba labda si wengi walio na ugonjwa huu, kwani “huenda kati ya asilimia 1 hadi 2 ya watu wa kawaida na asilimia 10 hadi 15 ya wagonjwa wa akili wanaotibiwa bila kulazwa hospitalini ndio wanaokumbwa na ugonjwa huo.” Hata hivyo, anaongeza hivi: “Watafiti fulani wanaamini kuwa idadi ya wanaougua ugonjwa huo inaongezeka kadiri njia mpya za kuugundua zinavyovumbuliwa na watu wanavyozidi kuhangaikia sura.” Ingawa hali hiyo inaweza kuwapata watu wa umri wowote, kwa kawaida inawakumba vijana hasa. Kwa watu wazima, idadi ya wanaume na wanawake wanaougua ugonjwa huo ni sawa. Ni tofauti sana na magonjwa ya kula ambayo huwapata hasa wanawake.

Kwa kawaida ugonjwa wa kuhangaikia sura kupita kiasi huwafanya watu wajitazame kwenye kioo mara nyingi sana na nyakati nyingine kujitenga sana na wengine. Kampuni ya Merck Manual inasema kwamba “mfadhaiko na kutofanya kazi vizuri kunakosababishwa na ugonjwa huo kunaweza kumfanya mtu alazwe hospitalini mara nyingi na atamani kujiua.” Si ajabu kwamba wagonjwa fulani huamua kufanyiwa upasuaji wa kubadili sura. Dakt. Katharine Phillips, ambaye ameandika kitabu kinachozungumzia ugonjwa huo anasema: “Mimi huwashauri watu wasifanyiwe upasuaji huo. Matokeo ya upasuaji hudumu, na watu wengi wenye ugonjwa huo huona kwamba haukurekebisha chochote.” *

Wakati mwingine, hata watoto wadogo hupata ugonjwa huo. Jarida George Street Journal * linaripoti kuhusu mvulana mwenye umri wa miaka sita “ambaye aliamini kwamba meno yake yana rangi ya manjano, tumbo lake ni ‘kubwa,’ na nywele zake ni mbaya. Hakuna aliyeona ‘kasoro’ hizo. Alikuwa akitumia karibu muda wa saa moja kila asubuhi kuchana nywele, na kama hangefurahia jinsi zilivyoonekana, angekitia kichwa chake ndani ya maji na kuanza kuzichana tena jambo ambalo mara nyingi lilimfanya achelewe kwenda shuleni.” Siku moja alipofika kwa daktari, hata alipiga magoti ili ajitazame kwenye sehemu inayong’aa ya kiti cha chuma.

Usiruhusu Ulimwengu Uathiri Mtazamo Wako

Majarida, magazeti, na matangazo ya biashara kwenye televisheni huonyesha picha nyingi za wanamitindo wenye maumbo bora. Watangazaji hao husema hivi: Ukiwaonyesha watu umbo wanalopaswa kuwa nalo, watatumia pesa wanazochuma kwa jasho ili wapate umbo kama hilo. Pia uvutano wa marika na mazungumzo yenye kuumiza ya washiriki wa familia au marafiki, yanaweza kuwafanya watu wawe na maoni yasiyofaa kuhusu sura yao. * Bila shaka haimaanishi kwamba mtu mwenye maoni yasiyofaa ana ugonjwa wa akili.

Ni jambo lisilofaa na lisilo la kweli kufikiri kwamba ikiwa huna sura yenye kuvutia, watu hawatapendezwa nawe. Kwa kawaida watu hawachagui marafiki kwa sababu ya sura yao. Ni kweli kwamba huenda watu kwanza wakaangalia sura, lakini utu na maadili ndiyo hufanya urafiki udumu. Kwa njia fulani kila mmoja wetu ni kama kitabu. Kinaweza kuwa na jalada lenye kuvutia, lakini ikiwa habari zilizomo hazipendezi, wasomaji wataacha kukisoma. Hata hivyo, ikiwa kitabu kinapendeza, wasomaji watakisoma hata kiwe na jalada la aina gani. Kwa hiyo, kwa nini usihangaikie sifa zako? Neno la Mungu, Biblia, linakutia moyo ufanye hivyo.—Methali 11:22; Wakolosai 3:8; 1 Petro 3:3, 4.

Kwa hakika, sura yetu hubadilika tunapoendelea kuzeeka. Ikiwa maisha, urafiki, na furaha zingetegemea sura nzuri ya ujana, wakati wetu ujao ungekuwa wenye kuhuzunisha! Hata hivyo, tunaweza kuwa na wakati ujao wenye kufurahisha. Inawezekanaje?

Urembo Utakaodumu

Methali 16:31 husema: “Kichwa chenye mvi ni taji la uzuri kinapopatikana katika njia ya uadilifu.” Machoni pa Yehova Mungu na machoni pa watu wote walio na maoni kama yake, watu wanaoendelea kumtumikia hadi wanapozeeka huendelea kuvutia. Kwa hakika, kwa sababu ya bidii yao na ujitoaji-kimungu, mvi zao zinafananishwa na taji la uzuri. Watu hao wa pekee wanastahili upendo na heshima nyingi kutoka kwetu.—Mambo ya Walawi 19:32.

Isitoshe, Yehova ameahidi kwamba katika ulimwengu mpya unaokuja, ataondoa madhara ambayo dhambi imewaletea waaminifu wake wote, wazee kwa vijana. Siku baada ya siku wataona na kuhisi miili yao ikiboreka hadi watakapofikia ukamilifu wa kimwili. (Ayubu 33:25; Ufunuo 21:3, 4) Hilo ni taraja zuri kama nini! Je, ungependa kuwa miongoni mwao? Ikiwa ndivyo, jitahidi kukazia fikira urembo ulio bora zaidi, na usiruhusu maoni ya kijuujuu na ya kikatili ya ulimwengu yaathiri mtazamo wako. Ukifanya hivyo, utakuwa mwenye furaha na mwenye kuvutia zaidi.—Methali 31:30.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Jarida la The Medical Journal of Australia linasema: “Kuhangaikia sura kupita kiasi ni dalili ya kawaida ya magonjwa kadhaa ya kiakili.” Magonjwa hayo yanatia ndani kushuka moyo, ugonjwa wa kushindwa kudhibiti mawazo au misukumo, na ugonjwa wa kuhofu kunenepa. Hivyo ni vigumu kuutambua ugonjwa huo.

^ fu. 5 Tafadhali ona makala “Vijana Huuliza . . . Je, Nifanyiwe Upasuaji wa Kubadili Sura?” katika toleo letu la Agosti 22, 2002. Bila shaka, huenda mtu mwenye ugonjwa wa akili akahitaji msaada wa daktari wa magonjwa ya akili.

^ fu. 6 Jarida la Chuo Kikuu cha Brown, Rhode Island, Marekani.

^ fu. 8 Kwa habari zaidi, tafadhali soma sura yenye kichwa “Sura Ni ya Maana Kadiri Gani?” katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.