Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna Ubaya Gani Kufanya Ngono Kabla ya Ndoa?

Kuna Ubaya Gani Kufanya Ngono Kabla ya Ndoa?

Vijana Huuliza . . .

Kuna Ubaya Gani Kufanya Ngono Kabla ya Ndoa?

“Nyakati nyingine mimi hujiuliza ikiwa ni vibaya kufanya ngono kabla ya ndoa, hasa ninapojihisi kuwa tofauti na wengine kwa sababu mimi ni bikira.”—Jordon. *

Kelly anasema: “Mimi hushawishiwa sana kufanya ngono. Nadhani hiyo ni asili yetu sote. Kila mahali unapoenda unasikia kuhusu ngono!”

JE, UNAHISI kama Jordon na Kelly? Desturi na maadili ya kale ambayo yaliwakataza watu kufanya ngono kabla ya ndoa yamezorota sana. (Waebrania 13:4) Uchunguzi mmoja uliofanywa katika nchi moja ya Asia ulifunua kwamba wavulana wengi kati ya umri wa miaka 15 na 24 wanahisi kwamba kufanya ngono kabla ya ndoa si jambo linalokubalika tu bali pia linatazamiwa. Haishangazi kwamba vijana wengi ulimwenguni pote hufanya ngono kabla ya kufikia umri wa miaka 19.

Pia, vijana wengine huepuka ngono lakini wanajihusisha katika matendo mengine yanayohusiana na ngono kama vile kupapasana viungo vya uzazi. Ripoti moja yenye kushtua katika gazeti la The New York Times ilionyesha kwamba “mara nyingi ngono ya kinywa huongoza kwenye ngono, na vijana wengi huiona kuwa salama kuliko ngono ya kawaida . . . na njia ya kuepuka kupata mimba na kudumisha ubikira wao.”

Mkristo anapaswa kuonaje ngono kabla ya ndoa? Na vipi matendo mengine yanayohusiana na ngono? Je, Mungu anayakubali? Je, ni salama? Na je, kweli yanadumisha ubikira?

Maana ya Uasherati

Muumba wetu, Yehova Mungu, ndiye anayeweza kuweka viwango kuhusiana na mambo hayo. Katika Neno lake anatuambia ‘tuukimbie uasherati.’ (1 Wakorintho 6:18) Hilo linamaanisha nini? Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “uasherati” halihusu tu ngono bali linatia ndani matendo mengine machafu yanayohusiana na ngono. Kwa hiyo, ikiwa watu wawili wasiooana wanajihusisha katika ngono ya kinywa au kupapasana viungo vya uzazi, wanafanya uasherati.

Je, bado Mungu atawaona kuwa mabikira? Neno “bikira” hutumiwa katika Biblia kuonyesha usafi wa maadili. (2 Wakorintho 11:2-6) Lakini linatumiwa kihalisi pia. Biblia inazungumzia msichana mmoja aliyeitwa Rebeka. Inasema kwamba alikuwa “bikira, wala hakuna mwanamume aliyekuwa amelala naye.” (Mwanzo 24:16) Katika Kiebrania cha awali, neno “ngono” lilihusisha matendo mengine zaidi ya ngono ya kawaida kati ya mwanamume na mwanamke. (Mwanzo 19:5) Kwa hiyo, kulingana na Biblia, kijana akijihusisha katika aina yoyote ya uasherati, hataonwa kuwa bikira.

Zaidi ya kuwahimiza Wakristo wajiepushe na uasherati, Biblia huwahimiza wajiepushe na matendo machafu ya aina zote ambayo yanaweza kuongoza kwenye uasherati. * (Wakolosai 3:5) Huenda ukadhihakiwa kwa kuchukua msimamo huo. Kijana mmoja Mkristo anayeitwa Kelly anasema: “Nilipokuwa katika shule ya sekondari, sikuzote niliambiwa, ‘Hujui kile unachokosa!’” Hata hivyo, ngono kabla ya ndoa ni “kufurahia dhambi kwa muda.” (Waebrania 11:25) Inaweza kusababisha madhara ya kudumu ya kimwili, kihisia, na kiroho.

Madhara Makubwa

Biblia inatueleza kwamba wakati mmoja Mfalme Sulemani alimwona kijana akishawishiwa kufanya ngono kabla ya ndoa. Sulemani alimlinganisha kijana huyo na “ng’ombe-dume anayeenda machinjoni.” Ng’ombe-dume anayeenda kuchinjwa hajui kitakachompata. Mara nyingi vijana wanaojihusisha na ngono kabla ya ndoa hutenda vivyo hivyo, kana kwamba hawajui madhara makubwa yatakayowapata! Sulemani alisema hivi kuhusu kijana huyo: “Hajajua kwamba nafsi yake mwenyewe inahusika.” (Methali 7:22, 23) Naam, “nafsi” yako, yaani, uhai wako umo hatarini.

Kwa mfano, kila mwaka mamilioni ya vijana hupata magonjwa ya zinaa. Lydia anasema: “Nilipojua kwamba nina ugonjwa fulani wa zinaa ambao husababisha vidonda, nilitaka kutoroka.” Anajuta hivi: “Ni ugonjwa unaosababisha maumivu makali sana na hauwezi kuponywa.” Zaidi ya nusu ya watu wanaoambukizwa virusi vya UKIMWI ulimwenguni pote (6,000 kwa siku) wana umri wa kati ya miaka 15 na 24.

Wanawake hasa ndio wanaokumbwa zaidi na matatizo yanayosababishwa na ngono kabla ya ndoa. Kwa kweli, wanawake ndio wanaokabili uwezekano mkubwa wa kupata magonjwa ya zinaa (kutia ndani virusi vya UKIMWI) kuliko wanaume. Msichana mdogo akipata mimba, yeye pamoja na mtoto wake aliye tumboni wamo hatarini. Kwa nini? Kwa kuwa mwili wa msichana huyo haujakomaa vya kutosha kuweza kujifungua bila matatizo yoyote.

Hata msichana huyo akiepuka matatizo makubwa ya afya, bado atakabili madaraka makubwa ya kuwa mzazi. Wasichana wengi huona kwamba kujiruzuku na kumtunza mtoto ni kazi ngumu sana kuliko walivyofikiri.

Kisha kuna madhara ya kiroho na kihisia. Dhambi ya uzinzi ya Mfalme Daudi ilihatarisha uhusiano wake pamoja na Mungu na alikuwa karibu kuangamia kiroho. (Zaburi 51) Ingawa Daudi alipona kiroho, alipata madhara ya dhambi yake muda wote wa maisha yake.

Vijana wanaweza kupatwa na madhara yayo hayo leo. Kwa mfano, Cherie alifanya ngono na mvulana fulani alipokuwa na umri wa miaka 17. Alifikiri kwamba mvulana huyo alimpenda. Miaka kadhaa imepita lakini bado anajutia matendo yake. Anasema hivi kwa masikitiko: “Nilipuuza kweli za Biblia na kupata madhara. Nilipoteza kibali cha Yehova, na hilo liliniumiza sana.” Kijana anayeitwa Trish anakubali hivi pia: “Kosa kubwa nililofanya maishani ni kufanya ngono kabla ya ndoa. Ninatamani sana kuwa bikira tena.” Naam, madhara ya kihisia yanaweza kudumu kwa miaka mingi na kusababisha mfadhaiko na huzuni.

Kujifunza Kujizuia

Msichana anayeitwa Shanda anazusha swali hili muhimu, “Kwa nini Mungu awape vijana tamaa ya ngono, akijua kwamba hawapaswi kuitosheleza kabla ya ndoa?” Ni kweli kwamba tamaa ya ngono inaweza kuwa yenye nguvu sana wakati wa “upeo wa ujana.” (1 Wakorintho 7:36) Kwa hakika, vijana wanaweza kupata tamaa ya ngono ghafula bila sababu yoyote. Lakini hiyo si dhambi. Hilo ni jambo la kawaida katika ukuzi wa viungo vya uzazi. *

Pia ni kweli kwamba Yehova alikusudia mahusiano ya ngono yafurahishe. Hilo linapatana na kusudi lake la awali kwamba wanadamu waijaze dunia. (Mwanzo 1:28) Hata hivyo, Mungu hakukusudia tutumie vibaya nguvu zetu za uzazi. Biblia inasema: “Kila mmoja wenu ajue jinsi ya kukiweza chombo chake mwenyewe katika utakaso na heshima.” (1 Wathesalonike 4:4) Ni upumbavu kutosheleza kila tamaa ya ngono kwani ni kama kumpiga mtu kila unapokasirika.

Mahusiano ya ngono ni zawadi kutoka kwa Mungu ambayo inapaswa kufurahiwa wakati unaofaa, yaani, baada ya mtu kufunga ndoa. Mungu anahisije tunapojaribu kufurahia ngono kabla ya ndoa? Wazia umemnunulia rafiki yako zawadi, lakini kabla ya kumpa anaiiba! Je, hungekasirika? Fikiria jinsi Mungu anavyohisi mtu anapofanya ngono kabla ya ndoa na kutumia vibaya zawadi ambayo Mungu ametoa.

Ufanyeje kuhusu hisia zako za ngono? Jifunze kuzizuia. Kumbuka kwamba “Yehova mwenyewe hatawanyima jambo lolote jema wale wanaotembea bila kosa.” (Zaburi 84:11) Kijana anayeitwa Gordon anasema: “Ninapoanza kufikiri kwamba si vibaya kufanya ngono kabla ya ndoa, mimi hutafakari kuhusu madhara ya kiroho na kutambua kwamba sipaswi kuruhusu dhambi yoyote iharibu uhusiano wangu na Yehova.” Huenda isiwe rahisi kujizuia. Lakini kama vile kijana anayeitwa Adrian anavyotukumbusha, “kujizuia hukuwezesha kuwa na dhamiri safi na uhusiano mzuri na Yehova, na kukazia fikira mambo ya maana zaidi bila majuto wala masikitiko yoyote.”—Zaburi 16:11.

Kuna sababu nyingi nzuri za ‘kujiepusha na uasherati’ wa aina yoyote. (1 Wathesalonike 4:3) Ni kweli kwamba si rahisi kufanya hivyo nyakati zote. Makala ya wakati ujao itazungumzia jinsi unavyoweza ‘kujihifadhi ukiwa safi kiadili.’—1 Timotheo 5:22.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 11 Kwa mazungumzo kuhusu uasherati, uchafu, na mwenendo mlegevu, ona makala ya “Vijana Huuliza . . . ‘Kupita Kiasi’ Kwafikia Wapi?” katika gazeti la Amkeni! la Oktoba 22, 1993.

^ fu. 20 Ona makala ya “Vijana Wanauliza . . . Kwa Nini Hili Linaupata Mwili Wangu?” katika toleo letu la Januari 8, 1991.

[Blabu katika ukurasa wa 13]

Kijana akifanya aina yoyote ya uasherati, je, Mungu ataendelea kumwona kuwa bikira?

[Picha katika ukurasa wa 13]

Kufanya ngono kabla ya ndoa kunaweza kuharibu dhamiri ya kijana anayemwogopa Mungu

[Picha katika ukurasa wa 14]

Wale wanaofanya ngono kabla ya ndoa hukabili uwezekano wa kupata ugonjwa wa zinaa