Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Viini Sugu Mimi hufurahia sana kusoma gazeti lenu. Nilipendezwa hasa na mfululizo wenye kichwa “Viini Sugu—Tatizo la Ulimwenguni Pote.” (Oktoba 22, 2003) Wakati ujao ningependa kupata magazeti yenu na kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova.

Y. G., Urusi

Kuwategemea Wazazi Asa- nteni sana kwa makala “Vijana Huuliza . . . Ninawezaje Kutambuliwa Bila Kuwategemea Wazazi?” (Oktoba 22, 2003) Baba yangu ni mzee katika kutaniko moja la Mashahidi wa Yehova na sikuzote mimi huonwa kuwa mfano wa kuigwa na wengine. Nilifikiria kuasi ili nitambuliwe. Nashukuru kwa makala hiyo iliyonisaidia kuona kwamba ningejuta ikiwa ningechukua hatua hiyo. Sasa ninafahamu kwamba ninapaswa kusitawisha sifa nzuri kutanikoni.

L. D., Ufaransa

Ninaelewa hisia za vijana wanaotajwa katika makala hiyo. Zamani nilihisi kwamba kutaniko lilitazamia mengi kutoka kwangu kwa sababu ya umaarufu wa baba yangu na ndugu yake. Popote nilipoenda nilitambuliwa kwa jina la familia yetu. Niliposhindwa kutimiza matarajio ya watu, nilihisi sifai kitu. Lakini sasa nimejifunza kwamba jambo muhimu zaidi ni jinsi Yehova anavyotuona.

S. S., Japani

Jina la Mungu Katika mwaka wa 1983, niliwanunulia watoto wangu kitabu kilichozungumza kuhusu Hawaii. Kilieleza jinsi mke wa mkuu fulani alivyohubiri kuhusu Mungu wake, Yehova, wapata mwaka wa 1800. Wakati huo haikuwa rahisi huku Slovakia, iliyokuwa nchi ya kisoshialisti, kusoma jina la Mungu katika vitabu. Na kwa miaka mingi hatukujua jinsi mke wa mkuu huyo alivyoweza kujua jina la Mungu zamani hizo. Hivyo, tulipokuwa tukisoma makala “Jina la Yehova Huko Pasifiki” (Oktoba 22, 2003), tulifurahia kupata maelezo kuhusu jambo hilo.

E. G., Slovakia

Mishonari Huko Afrika Nilifurahia simulizi la maisha la Ernest Pandachuk, lenye kichwa “Malezi Yangu Yalinisaidia Niishi Maisha Yenye Kusudi.” (Oktoba 22, 2003) Nina matatizo mbalimbali, kutia ndani ugonjwa na kumlea mwana wangu nikiwa peke yangu. Lakini matatizo yangu hayawezi kulinganishwa na mambo ambayo baadhi ya ndugu zetu Wakristo katika Afrika wamekabiliana nayo. Makala hiyo ilinigusa moyo na kunichochea nitafakari ahadi ya Yesu katika Mathayo 6:33, inayosema kwamba Yehova atawatunza wale wanaotafuta kwanza Ufalme.

M. C., Urusi

Kuutazama Ulimwengu Ninataka kuwashukuru kwa sehemu inayoitwa “Kuutazama Ulimwengu.” Hiyo ndiyo sehemu ya kwanza ninayosoma katika gazeti hili, na sikuzote mimi hutazamia kwa hamu kuona michoro yake. Michoro hiyo hunichochea nisome habari ambazo kwa kawaida hazinivutii. Mfano mmoja ni ile sehemu kuhusu “Samaki Wenye Makelele,” katika toleo la Oktoba 22, 2003. Ilinichekesha sana!

N. N., Marekani

Katika sehemu yenye kichwa “Kujikinga na Mbu” katika makala ya “Kuutazama Ulimwengu” (Agosti 8, 2003), mnataja ripoti moja inayopendekeza kutumia “miligramu 300 za vitamini B1 kila siku.” Kutumia kiasi hicho kila siku kunaweza kudhuru mwili.

H. M., Japani

“Amkeni!” linajibu: Wataalamu hawakubaliani kuhusu kiasi cha vitamini B1 (thiamini) kinachoweza kusababisha madhara. Baadhi yao wanapendekeza kutumia miligramu 1.1 tu kila siku. Hata hivyo, ripoti iliyochapishwa na Shirika la Afya Ulimwenguni inasema kwamba kulingana na ripoti fulani, “iligunduliwa kwamba kumeza tembe za miligramu 500 kila siku kwa mwezi mmoja hakudhuru.” Kwa vyovyote vile, habari hii inahitaji kufanyiwa utafiti zaidi.