Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Familia Zisizo na Baba Ni Tatizo Linaloongezeka

Familia Zisizo na Baba Ni Tatizo Linaloongezeka

Familia Zisizo na Baba Ni Tatizo Linaloongezeka

AKINA baba wengi wanaziacha familia zao. Katika miaka ya mwisho-mwisho ya 1990, gazeti USA Today lilisema kwamba Marekani ndiyo “nchi iliyo na idadi kubwa zaidi ya familia zisizo na baba.” Hata hivyo, familia zisizo na baba ni tatizo la ulimwenguni pote.

Ripoti ya idadi ya watu ya mwaka wa 2000 huko Brazili ilionyesha kwamba familia milioni 11.2 kati ya familia milioni 44.7, zinaongozwa na wanawake. Nchini Nikaragua, asilimia 25 ya watoto huishi na mama zao tu. Katika miaka ya 1990 huko Kosta Rika, idadi ya watoto wasiotambuliwa kisheria na baba zao iliongezeka kutoka asilimia 21.1 hadi asilimia 30.4.

Idadi hizo kutoka nchi tatu ni mfano tu wa hali ulimwenguni. Fikiria sehemu nyingine ya tatizo la familia zisizo na baba.

Akina Baba Wasiotimiza Madaraka Yao

Tafadhali ona sanduku “Baba, Utarudi Lini?” Nao, ambaye sasa ana umri wa miaka 23, anakubali hivi: “Nilimwona Baba mara chache sana kabla ya kuingia shule ya msingi. Siku moja alipokuwa akiondoka nyumbani, nilimsihi hivi, ‘Tafadhali usikose kurudi.’”

Mahusiano ya familia kama yale ya Nao na baba yake ndiyo yaliyomchochea Piotr Szczukiewicz, mwandishi kutoka Poland, kusema hivi: “Yaelekea baba ndiye mtu muhimu anayekosekana katika familia.” Ni kweli kwamba baba wengi huishi na familia zao na kuzitegemeza kiuchumi. Hata hivyo, kama vile gazeti Capital la Ufaransa lilivyoeleza, “baba wengi huridhika tu na kuandalia familia zao chakula huku wakipuuza kuwafundisha watoto wao.”

Mara nyingi kuna baba katika familia, lakini hajihusishi na maisha ya watoto wake. Anahangaikia mambo mengine. Jarida Famille chrétienne la Ufaransa linasema hivi: “[Baba] anaweza kuwepo kihalisi, lakini huenda asiwepo kiakili.” Kwa nini leo baba wengi wamejitenga na familia zao kiakili na kihisia?

Kulingana na jarida hilo, sababu kuu ni kwamba “yeye hukosa kuelewa daraka lake akiwa baba au mume.” Kulingana na maoni ya baba wengi, daraka la baba mzuri ni kuleta mshahara mnono. Kama alivyosema mwandishi Józef Augustyn, kutoka Poland, “baba wengi hufikiri wao ni wazazi bora kwa sababu wanachuma pesa kwa ajili ya familia.” Lakini hilo ni mojawapo tu ya madaraka ya baba.

Ukweli ni kwamba watoto hawawathamini baba zao kulingana na kiasi cha pesa wanazochuma au thamani ya zawadi wanazowapatia. Badala yake, watoto hutaka hasa upendo, wakati, na uangalifu kutoka kwa baba wala si zawadi. Hayo ndiyo mambo muhimu kwao.

Baba Wanahitaji Kujichunguza

Kulingana na ripoti ya Baraza Kuu la Elimu la Japani, “akina baba wanapaswa kuchunguza maisha yao kwa sababu wanatumia wakati mwingi kazini.” Swali ni, Je, baba yuko tayari kufanya marekebisho kwa faida ya watoto wake? Gazeti la Ujerumani Gießener Allgemeine, liliripoti uchunguzi fulani ulioonyesha kwamba baba wengi walikataa kuwatanguliza watoto wao badala ya kazi yao.

Watoto wanaweza kuumia sana kihisia wanapoona kwamba baba hawajali. Lidia, ambaye sasa ana umri wa miaka 21, anakumbuka vizuri jinsi baba yake alivyokuwa akifanya alipokuwa msichana mdogo huko Poland. Anasema: “Hakuzungumza nasi hata kidogo. Maisha yetu yalitofautiana kabisa. Hakujua kwamba nilikuwa nikienda disko.” Vilevile Macarena, msichana mwenye umri wa miaka 21 huko Hispania, anasema kwamba alipokuwa mtoto, baba yake “alizoea kwenda kujifurahisha na marafiki zake mwishoni mwa juma, na mara kwa mara hakurudi nyumbani kwa siku kadhaa.”

Kutanguliza Mambo Yanayofaa

Huenda baba wengi wakatambua kwamba hawatumii wakati wa kutosha pamoja na watoto wao. Baba ya kijana mmoja huko Japani alisema: “Ninatumaini kwamba mtoto wangu ataelewa hali yangu. Nyakati zote mimi humfikiria, hata ninapokuwa na shughuli nyingi.” Lakini je, tatizo hilo litasuluhishwa kwa kufikiri tu kwamba mtoto ataelewa kwa nini baba yake hapatikani?

Bila shaka, jitihada nyingi na kujinyima kunahitajiwa ili kutosheleza mahitaji ya mtoto. Ni kweli kwamba si rahisi kuwapa watoto kile wanachohitaji hasa, yaani upendo, wakati, na uangalifu. Yesu Kristo alisema: “Mwanadamu ataishi, si kwa mkate [au, chakula cha kimwili] tu.” (Mathayo 4:4) Pia, ni kweli kwamba watoto hawawezi kufanikiwa maishani kwa sababu tu ya vitu vya kimwili. Je, akina baba, mko tayari kudhabihu kitu chenye thamani zaidi kwenu, yaani, wakati au mafanikio yenu kazini ili kuwa pamoja na watoto wenu?

Gazeti Mainichi Daily News la Februari 10, 1986, lilieleza kuhusu baba mmoja aliyetambua kwamba watoto wake ni wenye thamani sana. Liliripoti hivi: ‘Ofisa mmoja wa cheo cha juu katika Shirika la Reli la Japani aliamua kuacha kazi badala ya kutenganishwa na familia yake.’ Kisha gazeti hilo likamnukuu ofisa huyo akisema: “Kazi ya mkurugenzi-mkuu inaweza kuchukuliwa na mtu yeyote. Lakini mimi peke yangu ndiye baba ya watoto wangu.”

Hatua ya kwanza ya kuwa baba mzuri ni kutambua mambo ambayo watoto wanahitaji kutoka kwa baba yao. Hebu tuchunguze kinachomaanishwa na kuwa baba mzuri.

[Sanduku katika ukurasa wa 3]

“Baba, Utarudi Lini?”

Hilo ndilo swali ambalo Nao, msichana Mjapani mwenye umri wa miaka mitano, alimwuliza baba yake alipokuwa akienda kazini siku moja. Ingawa aliishi nyumbani, Nao alimwona mara chache sana. Kwa kawaida alifika nyumbani Nao akiwa amelala na kwenda kazini kabla hajaamka.