Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Geneva Bible Tafsiri ya Biblia Iliyosahauliwa

Geneva Bible Tafsiri ya Biblia Iliyosahauliwa

Geneva Bible Tafsiri ya Biblia Iliyosahauliwa

Na mwandishi wa Amkeni! nchini New Zealand

JE, UNA Biblia ndogo iliyo na maandishi yanayosomeka kwa urahisi? Je, muundo wake unakuwezesha kupata habari unayotafuta kwa urahisi? Ikiwa ndivyo, basi ni kwa sababu ya tafsiri ya Geneva Bible ya mwaka wa 1560.

Si watu wengi leo ambao wamesikia kuhusu tafsiri ya Geneva Bible. Hata hivyo, ilipochapishwa, watu wengi sana waliinunua. Usahihi wa maandishi, muundo na mpangilio wake bora, ulifanya watu waliojua kusoma waipende sana. Shakespeare na Marlowe, waandishi wa tamthilia Waingereza, waliinukuu Biblia hiyo.

Ilikuwaje kwamba Biblia hiyo ya Kiingereza iliyopendwa sana ya karne ya 16 ikaanza kuchapishwa katika jiji lenye watu wanaozungumza Kifaransa la Geneva huko Uswisi? Ilikuwa na mambo gani ya pekee? Kwa nini iliacha kutumiwa? Inatufaidije leo?

Biblia Iliyo na Mambo Mapya

Tafsiri ya Geneva Bible ilichapishwa na kikundi cha wakimbizi wa kidini waliokimbia kutoka Uingereza kwa sababu ya mnyanyaso na kuhofia kuuawa wakati Mary Tudor alipoanza kutawala mwaka wa 1553. Wasomi hao walikaribishwa na Waprotestanti huko Geneva. Kutafsiriwa na kuchapishwa kwa Biblia kulisitawi sana huko Geneva kwa sababu kulikuwa na viwanda bora vya uchapishaji na wakazi wa jiji hilo walipenda kusoma Biblia.

Biblia hiyo, iliyotafsiriwa na William Whittingham na wasaidizi wake, ilikamilika mwaka wa 1560. Muda si muda, watu wakaanza kuisoma kwa hamu huko Uingereza. Biblia hiyo iliyosomeka kwa urahisi kuliko Biblia nyingine zilizoitangulia, ilikuwa Biblia ya kwanza katika Kiingereza kuwa na mistari iliyogawanywa kwa nambari, na utaratibu huo unatumiwa katika Biblia zote leo. Pia, juu ya kila ukurasa kulikuwa na maelezo mafupi yaliyowasaidia wasomaji kupata mafungu hususa kwenye ukurasa huo. Isitoshe, badala ya kutumia mtindo wa herufi nzito za Kigothi zilizonakiliwa katika hati, walitumia mtindo wa herufi zinazosomeka kwa urahisi sawa na ule unaotumiwa katika Biblia nyingi za Kiingereza leo.

Biblia za awali zilizokusudiwa kusomwa kanisani zilikuwa kubwa sana kwa sababu zilichapishwa kwenye kurasa kubwa zilizokunjwa mara moja. Tafsiri ya Geneva Bible ilibebeka kwa urahisi kwani ukubwa wake ulikuwa karibu nusu ya ukubwa wa Biblia zilizosomwa kanisani. Zaidi ya kusaidia katika usomaji wa kibinafsi na kujifunza, Biblia hiyo ndogo iliuzwa kwa bei nafuu pia.

Jitihada ya Kutokeza Tafsiri Sahihi

Watafsiri wa Geneva Bible walijitahidi hasa kudumisha mtindo na maana ya Kiebrania cha awali. Jina la Mungu, Yehova, lilipatikana katika sehemu kadhaa, kama vile kwenye kitabu cha Kutoka 6:3; 17:5; na Zaburi 83:18. Maneno ambayo watafsiri waliona yalifaa kuongezwa yaliandikwa kwa italiki, na maandishi yaliyoongezwa ili kukamilisha sarufi yalitiwa kwenye mabano ya mraba.

Biblia hiyo ikawa tafsiri rasmi huko Scotland. Pia ilitumiwa sana katika Uingereza na inadhaniwa kuwa ndiyo iliyobebwa na wakoloni Waingereza mwaka wa 1620 katika safari yao inayojulikana sana ya kwenda kwenye eneo ambalo sasa linaitwa Marekani. Tafsiri hiyo ilipelekwa kwenye koloni nyingine za Uingereza, hata kufikia koloni ya mbali zaidi ya New Zealand. Katika mwaka wa 1845, Gavana wa New Zealand aliyeitwa Sir George Grey, akapata nakala moja.

Maelezo ya Pambizoni Yanayobishaniwa

Wasomaji wa Geneva Bible waliendelea kuitumia kwa muda mrefu kwa sababu ya maelezo yake mengi ya pambizoni. Watafsiri waliongeza maelezo hayo kwa sababu walitambua kwamba Biblia ina sehemu fulani zilizo ngumu kuelewa. Hilo halikuwa jambo jipya. Tyndale alikuwa amefanya vivyo hivyo katika tafsiri yake ya “Agano Jipya” ya mwaka wa 1534. Zaidi ya maelezo ya pambizoni, Geneva Bible ilikuwa na picha, maelezo ya utangulizi, na ramani zilizokusudiwa kumsaidia msomaji aelewe mambo vizuri zaidi. Ilikuwa na orodha za vizazi, mihtasari, na hata sehemu iliyowatia watu moyo kuisoma Biblia kila siku.

Ingawa walikubali ubora wa tafsiri hiyo faraghani, viongozi wa Kanisa la Anglikana waliipinga hadharani kwa sababu waliyaona maelezo yake ya pambizoni kuwa ya ukaidi. Aliyekuwa Askofu Mkuu wa Canterbury, Matthew Parker, alisema kwamba maelezo hayo ni “hatari.” Mfalme James wa Kwanza aliyaona kuwa “yenye upendeleo sana, yasiyo ya kweli, na yenye kuchochea maasi.” Haishangazi kwamba walikuwa na maoni hayo kwani baadhi ya maelezo hayo ya pambizoni yalipinga wazo la kwamba watawala wanamwakilisha Mungu na mamlaka yao imetoka kwake!

Geneva Bible Yaacha Kutumiwa

Katika mwaka wa 1604, Mfalme James aliamuru tafsiri mpya ya Biblia ifanyizwe akitumaini kukomesha matumizi ya Geneva Bible huko Uingereza. Mwanahistoria wa theolojia, Alister McGrath anasema kwamba “sababu kubwa iliyofanya tafsiri ya King James Version isikubaliwe kwa urahisi katika karne ya 17 ni kwamba Geneva Bible ilikuwa ikitumiwa sana.” Kwa miaka mingi Geneva Bible ilipendwa na umma, na iliendelea kuwa Biblia rasmi huko Scotland. Chapa mpya ziliendelea kutolewa mpaka mwaka wa 1644.

Chama cha Biblia cha Uingereza na cha Lugha za Kigeni kilisema kwamba “uchunguzi wa Biblia ya King James ya mwaka wa 1611 unaonyesha kwamba watafsiri wake . . . walitegemea zaidi Biblia ya Geneva kuliko tafsiri nyingine yoyote ya Kiingereza.” Mitindo mipya ya kuwasilisha habari na maelezo ya Geneva Bible yalitumiwa katika King James Version.

Uvutano Unaodumu

Ijapokuwa iliacha kutumiwa na mahali pake pakachukuliwa na tafsiri ya Authorized Version au King James Version, tafsiri ya Geneva Bible ingali inakumbukwa. Zaidi ya kuweka viwango vipya vya utafsiri na utaratibu, imetumiwa sana kusahihisha tafsiri mbalimbali za Biblia za Kiingereza. Ilikuwa vigumu kwa watu wengi kuisoma Biblia, lakini Geneva Bible iliwawezesha kuisoma na kujifunza.

Kwa kuwa ilitumiwa kutafsiri Biblia ya King James, tafsiri ya Geneva Bible ilifanya baadhi ya taarifa za Biblia zitumiwe katika fasihi na ziingizwe pia katika lugha ya Kiingereza. Kwa hiyo, ingawa huenda watu wengi leo hawaijui Geneva Bible, ni wazi kwamba imekuwa na uvutano mkubwa na wa kudumu.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kutoka 6:3, mahali ambapo jina la Mungu linapatikana

[Picha katika ukurasa wa 13]

Maelezo yaliyo juu ya ukurasa

Picha

Maelezo ya pambizoni

[Hisani]

All photos: Courtesy American Bible Society

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 12]

All photos: Courtesy American Bible Society