Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuwa Baba Mzuri

Jinsi ya Kuwa Baba Mzuri

Jinsi ya Kuwa Baba Mzuri

MAKALA moja katika gazeti la Economist kuhusu kuzorota kwa maisha ya familia ilianza kwa taarifa hii yenye kuvuta fikira: “Kupata watoto ni rahisi, lakini kuwa baba mzuri si rahisi.”

Ijapokuwa ni vigumu kufanya mambo mengi maishani, mojawapo ya mambo magumu zaidi na muhimu zaidi maishani ni kuwa baba mzuri. Kila baba anapaswa kutamani kuwa baba mzuri, kwani hali njema na furaha ya familia yake inategemea jambo hilo.

Kwa Nini Si Rahisi Kuwa Baba Mzuri?

Kwa ufupi, mojawapo ya sababu kuu zinazofanya isiwe rahisi kuwa baba mzuri ni hali ya kutokamilika iliyorithiwa na wazazi na watoto wao pia. Biblia inasema: “Mwelekeo wa moyo wa mwanadamu ni mbaya tangu ujana wake na kuendelea.” (Mwanzo 8:21) Ndiyo sababu mwandikaji mmoja wa Biblia alikubali hivi: “Mama yangu alinichukua mimba katika dhambi.” (Zaburi 51:5; Waroma 5:12) Lakini mwelekeo wa kufanya mabaya kwa sababu ya dhambi iliyorithiwa ni kizuizi kimoja tu kinachofanya iwe vigumu kuwa baba mzuri.

Kizuizi kingine kikubwa ni ulimwengu huu, yaani, mfumo wa mambo. Kwa nini? Kwa sababu kama vile Biblia inavyoeleza, “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu,” anayetambulishwa kuwa “yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani.” Vilevile Biblia inamwita Shetani “mungu wa mfumo huu wa mambo.” Si ajabu kwamba Yesu alisema wanafunzi wake hawapaswi kuwa “sehemu ya ulimwengu” kama vile ambavyo yeye si sehemu ya ulimwengu!—1 Yohana 5:19; Ufunuo 12:9; 2 Wakorintho 4:4; Yohana 17:16.

Ili kuwa baba mzuri ni muhimu sikuzote kutambua mambo haya: kutokamilika kwetu, Shetani Ibilisi, na ulimwengu huu unaoongozwa naye. Vizuizi hivyo si vya kuwaziwa. Ni halisi! Lakini mtu anaweza kujifunza wapi jinsi ya kuvishinda na jinsi ya kuwa baba mzuri?

Mfano wa Yehova na Yesu

Akina baba wanaweza kuichunguza Biblia ili kupata msaada wa kushinda vizuizi hivyo vilivyotajwa juu. Kuna mifano bora inayozungumziwa humo. Yesu alionyesha mfano bora zaidi alipowafundisha wanafunzi wake kusali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni.” Biblia humfafanua Baba yetu wa mbinguni kwa njia rahisi, inaposema: “Mungu ni upendo.” Baba ambaye ni mwanadamu anapaswa kutendaje anapofikiria mfano huo wenye upendo? Mtume Paulo alihimiza hivi: “Iweni waigaji wa Mungu . . . na endeleeni kutembea katika upendo.”—Mathayo 6:9, 10; 1 Yohana 4:8; Waefeso 5:1, 2.

Ikiwa wewe ni baba, fikiria jambo unaloweza kujifunza kutokana na tukio hili moja linaloonyesha jinsi Mungu alivyoshughulika na Mwana wake, Yesu. Andiko la Mathayo 3:17 linatueleza kwamba Yesu alipobatizwa katika maji, sauti ya Mungu ilisikika kutoka mbinguni, ikisema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” Tunaweza kujifunza nini kutokana na hilo?

Kwanza, fikiria jinsi mtoto anavyohisi wakati baba yake anapomwambia mtu fulani kwa furaha, ‘Huyu ni mwanangu’ au ‘Huyu ni binti yangu.’ Watoto hufanya maendeleo mazuri wazazi wanapowahangaikia na hasa wanapowapongeza. Yaelekea mtoto atachochewa kujitahidi zaidi ili apongezwe.

Pili, Mungu alieleza jinsi alivyohisi kumhusu Yesu alipomwita “mpendwa.” Bila shaka, taarifa hiyo ya upendo kutoka kwa baba yake ilimfurahisha Yesu sana. Watoto wako watatiwa moyo pia iwapo utawaonyesha kwamba unawapenda sana kwa maneno yako, na vilevile kwa kutumia wakati pamoja nao, kuwapa uangalifu, na kuwahangaikia.

Tatu, Mungu alimwambia Mwana wake: “Nimekukubali wewe.” (Marko 1:11) Hilo pia ni jambo muhimu ambalo mzazi anapaswa kufanya, yaani, kuwaambia watoto wake kwamba anapendezwa nao. Ni kweli kwamba mara nyingi mtoto atafanya makosa. Sisi sote hukosea. Lakini ukiwa baba, je, wewe hutafuta nafasi za kuwapongeza watoto wako kwa mambo wanayofanya na kusema?

Yesu alijifunza kwelikweli kutokana na Baba yake wa mbinguni. Akiwa duniani alionyesha waziwazi kwa maneno na matendo jinsi Baba yake anavyohisi kuwaelekea watoto Wake walio duniani. (Yohana 14:9) Hata Yesu alipokuwa na shughuli na mkazo mwingi, alitenga wakati wa kuketi na kuzungumza na watoto. Aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwazuia.” (Marko 10:14) Je, ninyi akina baba mnaweza kuiga mfano wa Yehova Mungu na wa Mwana wake kwa ukamili zaidi?

Ni Muhimu Kuwa Mfano Mzuri

Ni muhimu sana kuwa mfano mzuri kwa watoto wako. Yaelekea jitihada zako za ‘kuendelea kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova’ hazitafanikiwa usipokubali nidhamu kutoka kwa Mungu na kuiruhusu iongoze maisha yako. (Waefeso 6:4) Lakini kwa msaada wa Mungu, unaweza kushinda jambo lolote linalokuzuia kutii amri yake ya kuwatunza watoto wako.

Fikiria mfano wa Viktor Gutschmidt, Shahidi wa Yehova aliyeishi katika ule uliokuwa Muungano wa Sovieti. Mnamo Oktoba 1957, alihukumiwa kifungo cha miaka kumi kwa sababu ya kuhubiri kuhusu imani yake. Aliwaacha binti wawili wadogo na mke wake, Polina. Akiwa gerezani, aliruhusiwa kuandikia familia yake barua bila kutaja jambo lolote kumhusu Mungu au dini. Hata katika hali hiyo ngumu, Viktor aliazimia kuwa baba mzuri na alifahamu kwamba kuwafundisha watoto wake kumhusu Mungu ni jambo muhimu sana. Basi alifanya nini?

Viktor anaeleza hivi: “Nilipata habari za kuandika katika magazeti ya Young Naturalist na Nature ya Sovieti. Kisha nikachora picha za wanyama na watu kwenye kadi zinazotumwa kupitia posta na kuandika hadithi au simulizi kuhusu viumbe vya asili.”

Polina anasema hivi: “Mara tu tulipopokea kadi hizo tulizihusianisha na habari za Biblia. Kwa mfano, kadi hizo zilipoonyesha uzuri wa uumbaji, misitu, au mito, nilisoma Isaya sura ya 65,” inayozungumzia ahadi za Mungu za kufanya dunia kuwa paradiso.

Binti ya Viktor anayeitwa Yulia anasema: “Kisha Mama alisali pamoja nasi, na tulilia. Kadi hizo zilikuwa muhimu sana katika malezi yetu.” Polina anasema kwamba kutokana na kadi hizo “wasichana wangu walimpenda Mungu sana tangu utotoni.” Familia hiyo inaendeleaje sasa?

Viktor anaeleza hivi, “Sasa binti zangu wawili wameolewa na wazee Wakristo na wote wana familia zilizo imara kiroho pamoja na watoto wanaomtumikia Yehova kwa uaminifu.”

Zaidi ya ustadi, jitihada nyingi zinahitajiwa ili kuwa mfano mzuri. Yaelekea watoto watachochewa wanapoona baba yao akijitahidi sana kuwa mfano mzuri. Mwana mmoja aliyetumikia kwa miaka mingi katika utumishi wa wakati wote alisema hivi kwa uthamini kuhusu baba yake, “Nyakati nyingine baba alirudi nyumbani kutoka kazini akiwa amechoka sana hivi kwamba haikuwa rahisi kwake kukaa macho, lakini bado tulifanya funzo letu la Biblia, na hilo lilitusaidia kuchukua funzo hilo kwa uzito.”

Ni wazi kwamba kuwa mfano mzuri, katika maneno na matendo, ni muhimu sana ili uwe baba mzuri. Unahitaji kufanya hivyo ili uone ukweli wa methali hii ya Biblia inayosema: “Mlee mvulana kulingana na njia inayomfaa; hata atakapozeeka hatageuka kando na kuiacha.”—Methali 22:6.

Kwa hiyo, kumbuka kwamba jambo muhimu si yale unayosema tu, bali kilicho muhimu zaidi ni kile unachofanya, yaani, mfano wako. Mtaalamu Mkanada wa elimu ya watoto aliandika hivi: “Njia bora zaidi ya kuwachochea watoto wetu wajiendeshe [jinsi tutakavyo] ni kuweka mfano mzuri sisi wenyewe.” Kwa hakika, ukitaka watoto wako wathamini mambo ya kiroho ni lazima wewe mwenyewe uyathamini.

Tumia Wakati Pamoja na Watoto!

Watoto wako wanapaswa kuona mfano wako mzuri. Hilo linamaanisha kwamba unapaswa kutumia wakati mwingi sana pamoja nao wala si vipindi vifupi-vifupi tu. Kwa hekima, tii shauri la Biblia la ‘kujinunulia wakati,’ kwa kupuuza mambo yasiyo muhimu sana ili kuwa pamoja na watoto wako. (Waefeso 5:15, 16) Je, kweli kuna jambo muhimu kuliko watoto wako? Je, ni televisheni kubwa, michezo, nyumba nzuri, au kazi yako?

Akina baba wasipotumia wakati kuwashughulikia watoto wakiwa wachanga, watapata matokeo mabaya baadaye. Mara nyingi akina baba walio na watoto wenye mwenendo mpotovu au wasiojali mambo ya kiroho hujuta sana. Wao husikitika kwamba walishindwa kutumia wakati pamoja na watoto wao wachanga wakati walipowahitaji sana.

Kumbuka kwamba unahitaji kufikiria matokeo ya maamuzi yako watoto wakiwa wachanga. Biblia huwaita watoto wako “urithi kutoka kwa Yehova,” urithi ambao Mungu mwenyewe amekupa. (Zaburi 127:3) Hivyo, usisahau kamwe kwamba unawajibika mbele za Mungu kuhusiana na vile unavyowatendea!

Kuna Msaada

Baba mzuri hutamani kupata msaada utakaowafaidi watoto wake. Baada ya malaika kumwambia mke wa Manoa kwamba angepata mtoto, Manoa alimwomba Mungu hivi: “Tafadhali, . . . na arudi kwetu tena, atufundishe yale tunayopaswa kumtendea huyo mtoto atakayezaliwa.” (Waamuzi 13:8, 9) Manoa alihitaji msaada gani unaohitajiwa pia na wazazi leo? Hebu tuone.

Brent Burgoyne, mwalimu katika Chuo Kikuu cha Cape Town, Afrika Kusini, alisema: “Mojawapo ya zawadi kubwa ambazo mtu anaweza kumpa mtoto ni kumfundisha maadili bora.” Ukweli wa jambo hilo unaonyeshwa na ripoti moja katika gazeti Daily Yomiuri la Japani, iliyosema: “Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba asilimia 71 ya watoto Wajapani hawajawahi kukatazwa na baba zao wasiseme uwongo.” Jambo hilo linasikitisha, sivyo?

Ni nani anayeweza kufundisha maadili bora yenye kutegemeka? Ni yule aliyempa Manoa mwongozo, yaani, Mungu mwenyewe! Ili kutusaidia, Mungu alimtuma Mwana wake mpendwa, Yesu, akiwa Mwalimu—kama vile alivyoitwa na wengi. Kwa sasa, kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu, ambacho kina masomo yanayotegemea mafundisho ya Yesu, kinapatikana katika lugha nyingi ili kikusaidie kuwafundisha watoto.

Zaidi ya kufundisha kanuni zinazopatikana katika Neno la Mungu, kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu kina picha zaidi ya 160 zenye maswali muhimu. Kwa mfano, picha inayopatikana katika sura ya 22 yenye kichwa “Kwa Nini Hatupaswi Kusema Uwongo?” imeonyeshwa kwenye ukurasa wa 32 wa gazeti hili. Maelezo yaliyo kwenye ukurasa wenye picha hii yanasema hivi: “Labda mvulana anamwambia baba yake hivi: ‘La, sikupiga mpira ndani ya nyumba.’ Lakini namna gani ikiwa kwa kweli alifanya hivyo? Je, ni vibaya kusema kwamba hakupiga mpira?”

Pia kuna habari zenye kuchochea katika sura hizi: “Utii Unakulinda Wewe,” “Tuepuke Vishawishi,” “Jinsi ya Kuwa Mwenye Fadhili,” “Usiwe Mwizi Kamwe!,” “Je, Karamu Zote Zinampendeza Mungu?,” “Jinsi ya Kumfurahisha Mungu,” na “Kwa Nini Tufanye Kazi?” Hizo ni sura chache tu kati ya sura 48 za kitabu hicho.

Utangulizi wa kitabu hicho unamalizia kwa maneno haya: “Watoto wanahitaji zaidi kuelekezwa kwa Chanzo cha hekima yote, Baba yetu wa mbinguni, Yehova Mungu. Kila wakati Mwalimu Mkuu, Yesu, aliwaelekeza watu kwenye chanzo cha hekima yote, Muumba wetu. Kitabu hiki na kikusaidie sana pamoja na familia yako kumpendeza Yehova ili mpokee baraka za milele.” *

Hapana shaka kwamba kuwa baba mzuri kunatia ndani kuwa mfano mzuri kwa watoto wako, kutumia wakati mwingi pamoja nao, na kuwasaidia waishi kulingana na kanuni za Mungu ambazo ameonyesha katika Biblia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 35 Vitabu vingine ambavyo vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova ili kusaidia familia ni Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, Maswali Ambayo Vijana Huuliza−Majibu Yafanyayo Kazi, na Siri ya Kupata Furaha ya Familia.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Ajapokuwa gerezani, Viktor Gutschmidt alifanikiwa kuwa baba mzuri

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Alipofungwa gerezani kwa sababu ya imani yake, Viktor aliwachorea watoto wake picha hizi ili kuwafundisha

[Picha katika ukurasa wa 9]

Binti za Viktor katika mwaka wa 1965

[Picha katika ukurasa wa 10]

Akina baba wanapaswa kujitahidi sana kuwafundisha watoto wao