Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kitu Bora Kuliko Umashuhuri wa Ulimwengu

Kitu Bora Kuliko Umashuhuri wa Ulimwengu

Kitu Bora Kuliko Umashuhuri wa Ulimwengu

SIMULIZI LA CHARLES SINUTKO

Katika mwaka wa 1957, nilipewa kandarasi ya kuimba kwa majuma 13 huko Las Vegas, Nevada, Marekani, kwa mshahara wa dola elfu moja kwa juma, na kulikuwa na uwezekano wa kuendelea na kazi hiyo kwa majuma mengine 50 iwapo maonyesho yangu yangefanikiwa. Hiyo ingemaanisha kwamba ningepata dola 50,000 zaidi, na hicho kilikuwa kiasi kikubwa sana cha pesa wakati huo. Acha nieleze jinsi nilivyopata kandarasi hiyo yenye pesa nyingi na jinsi ilivyokuwa vigumu kufanya uamuzi wa kuikubali au kutoikubali.

BABA, ambaye ana asili ya Ukrainia, alizaliwa Ulaya Mashariki mnamo mwaka wa 1910. Katika mwaka wa 1913, mama yake alipohamia Marekani ili kuishi na mume wake, alienda pamoja naye. Katika mwaka wa 1935, Baba alioa nami nikazaliwa mwaka mmoja baadaye huko Ambridge, Pennsylvania. Karibu wakati huohuo, ndugu zake wawili wakubwa wakawa Mashahidi wa Yehova.

Wakati mimi na ndugu zangu watatu tulipokuwa wadogo tuliishi karibu na New Castle, Pennsylvania, na mama yetu alijifunza Biblia kwa muda na Mashahidi. Wazazi wangu hawakuwa Mashahidi wakati huo, lakini Baba alionelea kwamba ndugu zake walikuwa na haki ya kuamini walichotaka. Ingawa Baba alitaka tuwe wazalendo, sikuzote alitetea haki ya wengine ya kuabudu wapendavyo.

Kazi ya Kuimba

Wazazi wangu waliamini kwamba nilikuwa na kipawa cha kuimba, hivyo walinisaidia kuwa mwimbaji bora. Nilipokuwa na miaka sita au saba, Baba alinisimamisha juu ya meza katika klabu cha usiku ili niimbe na kucheza gita. Niliimba wimbo ulioitwa “Mama.” Wimbo huo hufafanua sifa za mama mwenye upendo na unamalizika kwa njia yenye kuvutia. Watu waliokuwa wamekunywa kupindukia, walikuwa wakipiga kelele na kutumbukiza pesa ndani ya kofia ya Baba.

Niliimba wimbo wa country katika kipindi changu cha kwanza cha redio kwenye kituo cha redio cha WKST huko New Castle mwaka wa 1945. Baadaye nilianza kuimba nyimbo zilizopendwa ambazo zilichezwa katika kipindi cha redio cha Hit Parade kilichocheza nyimbo kumi bora za kila juma. Katika mwaka wa 1950, nilionekana kwa mara ya kwanza kwenye televisheni katika kipindi cha Paul Whiteman. Bado watu wanakumbuka jinsi George Gershwin alivyoimba wimbo wa “Rhapsody in Blue” alipoalikwa na Paul Whiteman. Muda mfupi baadaye Baba aliuza nyumba yetu huko Pennsylvania, nasi tukahamia Los Angeles, California, ili kuendeleza kazi yangu.

Kwa sababu ya kuhimizwa na Baba, nilianzisha kipindi cha redio cha kila juma huko Pasadena na maonyesho ya kila juma ya nusu saa kwenye televisheni huko Hollywood. Nilirekodi muziki katika kampuni ya kurekodi muziki ya Capitol Records pamoja na okestra ya watu 100 ya Ted Dale, na vilevile nikawa mwimbaji katika shirika la redio la CBS. Katika mwaka wa 1955 nilifanya maonyesho ya muziki huko Lake Tahoe, kaskazini mwa California. Miradi yangu ilibadilika sana nikiwa huko.

Miradi Mipya

Karibu na wakati huo, John, ndugu mkubwa wa Baba aliyekuwa pia amehamia California kutoka Pennsylvania, alinipa kitabu “Let God Be True.” * * Nilienda nacho Lake Tahoe. Maonyesho yetu ya mwisho yaliisha usiku wa manane, kisha nilipokuwa nikipumzika nikaanza kusoma kitabu hicho kabla ya kulala. Nilifurahi kupata majibu ya Biblia kwa maswali niliyokuwa nimejiuliza kwa muda mrefu.

Muda si muda, nilianza kubaki klabuni baada ya kazi nikizungumza na waimbaji wenzangu, na mara nyingi tuliendelea kuzungumza mpaka alfajiri. Tulizungumzia mambo kama vile uhai baada ya kifo, kinachofanya Mungu aruhusu uovu, na ikiwa mwanadamu atajiangamiza na kuiangamiza dunia. Miezi michache baadaye, katika kusanyiko la wilaya la Mashahidi wa Yehova lililofanywa katika uwanja wa Wrigley Field, Los Angeles, mnamo Julai 9, 1955, nilibatizwa ili kuonyesha kwamba nimejiweka wakfu nimtumikie Yehova Mungu.

Karibu miezi sita baadaye, asubuhi ya Krismasi ya mwaka wa 1955, Shahidi mwenzangu aliyeitwa Henry Russell alinialika tumtembelee Jack McCoy, aliyefanya kazi katika fani ya burudani. Henry alikuwa msimamizi wa muziki katika Shirika la Utangazaji la Kitaifa (NBC). Ingawa Jack na watoto wake watatu pamoja na mke wake walikuwa wametoka tu kufungua zawadi zao za Krismasi, waliketi na kutusikiliza. Muda si muda, Jack na familia yake wakawa Mashahidi.

Wakati huohuo, nilijifunza na Mama, naye akaikubali kweli ya Biblia. Hatimaye akawa Shahidi wa Yehova na pia painia, yaani, mweneza-injili wa wakati wote. Muda si muda, ndugu zangu watatu walibatizwa pia na kuwa mapainia kwa muda. Mnamo Septemba 1956, nikiwa na umri wa miaka 20, nilianza upainia.

Maamuzi Kuhusu Kazi ya Kuajiriwa

Wakati huohuo, George Murphy, rafiki wa meneja wangu alitaka kunisaidia nifanye maendeleo katika uimbaji. George aliigiza katika sinema nyingi kati ya miaka ya 1930 na 1940. Kwa sababu Murphy alikuwa mtu mashuhuri, katika Desemba 1956 nilishiriki katika maonyesho ya Jackie Gleason katika televisheni ya CBS huko New York. Ilikuwa hatua muhimu katika kazi yangu kwani ilikadiriwa kwamba watu milioni 20 walihudhuria maonyesho hayo. Nikiwa New York, nilitembelea makao makuu ya Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza huko Brooklyn.

Baada ya kushiriki katika maonyesho ya Gleason, nilitia sahihi kandarasi ya miaka saba na shirika moja la sinema la Metro-Goldwyn-Mayer (MGM). Nilipewa sehemu katika mfululizo mmoja wa vipindi vya televisheni. Hata hivyo, baada ya muda, dhamiri yangu ilianza kunisumbua kwani nilipaswa kuigiza sehemu ya mchezaji wa kamari na mfyatuaji stadi wa risasi—sehemu zilizoonyesha ukosefu wa adili na mwenendo mwingine usio wa Kikristo. Hivyo nikajiuzulu. Wafanyakazi wenzangu walifikiri kwamba nimerukwa akili.

Huo ndio wakati ambapo nilipata ile kandarasi huko Las Vegas, niliyoizungumzia mwanzoni. Nilipaswa kuanza kazi wakati wa juma la ziara ya mwangalizi asafiriye. Ikiwa singeanza kazi wakati huo, ningepoteza kandarasi hiyo. Nilichanganyikiwa, hasa kwa sababu Baba alitazamia nichume pesa nyingi! Nilihisi kwamba alistahili malipo kwa ajili ya jitihada zake za kunisaidia kufanya maendeleo katika kazi yangu.

Hivyo nilimwendea Carl Park, mwangalizi-msimamizi wa kutaniko letu. Yeye pia alikuwa mwanamuziki na alipiga fidla katika kituo cha redio cha WBBR huko New York katika miaka ya 1920. Nilimweleza kwamba ikiwa ningekubali kandarasi hiyo ningeweza kufanya upainia maisha yangu yote bila kuhangaika kuhusu pesa. Akaniambia, “Siwezi kukuambia la kufanya, lakini ninaweza kukusaidia ufanye uamuzi.” Kisha akaniuliza, “Je, ungeondoka iwapo mtume Paulo angetembelea kutaniko letu juma hili?” Naye akaongezea, “Unafikiri Yesu angetaka ufanye nini?”

Ilikuwa wazi kabisa. Nilipomwambia Baba kwamba nimeamua kutofanya kazi hiyo huko Las Vegas, alisema kwamba ninaharibu maisha yake. Usiku huo aliningoja akiwa na bunduki. Alikusudia kuniua, lakini kwa sababu alikuwa amelewa sana, alisinzia na kulala. Kisha akajaribu kujiua akiwa ndani ya gereji kwa kuvuta moshi wa gari. Niliwaita waokoaji, nao wakamwokoa.

Ingawa wengi kutanikoni walimwogopa Baba kwa sababu ya hasira yake, Roy Dowell, mwangalizi wetu wa mzunguko hakumwogopa. Roy alipomtembelea, Baba alimwambia kwamba nilipozaliwa kulikuwa na uwezekano mkubwa kwamba ningekufa. Baba alikuwa amemwahidi Mungu kwamba iwapo nitaishi, atanitoa nimtumikie. Roy akamuuliza iwapo aliwahi kufikiri kwamba Mungu anamtazamia atimize ahadi hiyo. Jambo hilo lilimshangaza Baba. Kisha Roy akamuuliza, “Ikiwa utumishi wa wakati wote ulimfaa Mwana wa Mungu, kwa nini usimfae mwana wako?” Baada ya mazungumzo hayo ilionekana kwamba Baba amekubali uamuzi niliofanya.

Wakati huohuo, katika Januari 1957, Shirley Large pamoja na painia mwenzake walitoka Kanada kuja kutembelea marafiki wao. Tulifahamiana na Shirley nilipohubiri nyumba kwa nyumba pamoja naye na painia mwenzake. Baadaye Shirley aliambatana nami kwenda Hollywood Bowl, ambapo niliimba na Pearl Bailey.

Kushikamana na Uamuzi Wangu

Katika Septemba 1957, nilipokea mgawo wa kutumikia nikiwa painia wa pekee katika jimbo la Iowa. Nilipomwambia Baba kwamba nilikuwa nimekubali mgawo huo, alilia sana. Hakuelewa maoni yangu kuhusu mambo yaliyo muhimu. Nilienda Hollywood na kukatiza kandarasi zangu zote. Mmoja wa watu niliowafanyia kazi ni Fred Waring, kiongozi mashuhuri wa okestra na kwaya. Aliniambia kwamba sitaweza kufanya kazi ya uimbaji tena iwapo sitatimiza mapatano yangu. Hivyo, nikamweleza kwamba nilikuwa nikiacha kazi hiyo ili nimtumikie Yehova Mungu zaidi.

Bwana Waring alinisikiliza kwa makini nilipokuwa nikizungumza, kisha akanishangaza aliposema hivi kwa upole: “Mwanangu, ninasikitika kwamba unaacha kazi nzuri jinsi hii, lakini nimefanya kazi hii maisha yangu yote na nimeona kwamba kuna mambo mengine yaliyo muhimu maishani kuliko muziki. Mungu na akubariki.” Bado ninakumbuka nikienda nyumbani huku nikitokwa na machozi ya shangwe, nikijua kwamba sasa nilikuwa huru kutumia maisha yangu kumtumikia Yehova.

“Imani Yako Iko Wapi?”

Nilianza kutumikia huko Strawberry Point, mji wenye wakazi 1,200 hivi huko Iowa, pamoja na painia mwenzangu Joe Triff. Shirley alitutembelea, nasi tukazungumzia kufunga ndoa. Hatukuwa na pesa. Pesa zangu zote zilikuwa na Baba. Hivyo, nikamwambia: “Ninataka kukuoa, lakini tutaishije? Nikiwa painia wa pekee mimi hupata dola 40 tu kila mwezi.” Naye akaniuliza hivi kwa njia yake ya kawaida ya moja kwa moja na ya upole: “Lakini Charles, imani yako iko wapi? Yesu alisema kwamba tukiutafuta kwanza Ufalme na uadilifu wake, atatuongezea vyote tunavyohitaji.” (Mathayo 6:33) Basi tukafanya uamuzi na kufunga ndoa Novemba 16, 1957.

Nilijifunza Biblia na mkulima mmoja nje ya mji wa Strawberry Point ambaye alikuwa na nyumba ndogo ya mbao katika msitu karibu na nyumba yake. Haikuwa na umeme, maji, wala choo. Lakini iwapo tuliitaka tungeishi humo bila malipo. Ilikuwa nzee, lakini tuliamua kwamba kwa kuwa tulitumia siku nzima kuhubiri, tulihitaji tu mahali pa kulala.

Niliteka maji katika chemchemi iliyokuwa karibu. Tuliipasha nyumba joto kwa kuni na tulitumia taa ya mafuta kusoma; Shirley alitumia jiko la mafuta kupika. Tulioga katika bafu iliyochakaa. Tuliwasikia mbweha wakipiga kelele usiku na tulihisi kuwa ni pendeleo kuwa pamoja, na kumtumikia Yehova tukiwa pamoja mahali ambapo pana uhitaji mkubwa wa wahudumu Wakristo. Bill Malenfant na mke wake Sandra, ambao sasa wanatumikia katika makao makuu huko Brooklyn, walikuwa mapainia wa pekee huko Decorah, Iowa, kilometa 100 hivi kutoka katika eneo letu. Mara kwa mara walikuja kuhubiri nasi. Hatimaye, kulikuwa na kutaniko dogo la watu 25 hivi huko Strawberry Point.

Kutembelea Makutaniko

Katika Mei 1960, tulipata mgawo wa kutembelea makutaniko, yaani kazi ya kuzunguka. Mzunguko wetu wa kwanza ulikuwa North Carolina, na ulitia ndani majiji ya Raleigh, Greensboro, na Durham, na vilevile miji mingi midogo ya mashambani. Hali yetu ya maisha iliboreka kwani tuliishi na familia nyingi zilizoishi katika nyumba zenye umeme na hata vyoo. Hata hivyo, tulipata wasiwasi tulipoonywa na wale waliokuwa na vyoo nje ya nyumba. Walituonya tujihadhari na nyoka njiani!

Mapema katika mwaka wa 1963 tulipelekwa kwenye mzunguko mwingine huko Florida, ambapo nilipata ugonjwa fulani hatari wa moyo na nilikuwa karibu kufa. Huenda ningekufa ikiwa singesaidiwa na Bob na Ginny Mackey wa Tampa. * Walinipeleka kwa daktari wao na hata kulipia matibabu yangu yote.

Nilitumia Mambo Niliyokuwa Nimejifunza

Katikati ya mwaka wa 1963, nilialikwa New York kupangia kusanyiko kubwa la Mashahidi wa Yehova ambalo lingefanywa huko. Niliandamana na Milton Henschel, msemaji wa Mashahidi wa Yehova, ili kushiriki kipindi cha mahojiano kwenye redio, kilichosimamiwa na Larry King. Bwana King angali msimamizi wa kipindi maarufu cha mahojiano kwenye televisheni. Alikuwa mwenye heshima sana na kwa muda wa saa moja hivi baada ya kipindi hicho, alituuliza maswali mengi kuhusu kazi yetu.

Wakati huohuo, Harold King, mishonari aliyekuwa ameachiliwa kutoka gerezani huko China wakati wa utawala wa Ukomunisti, alitembelea makao makuu ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni. Jioni moja alihutubia umati wa watu 700 hivi na kusimulia baadhi ya mambo aliyojionea na kueleza jinsi imani yake ilivyoimarishwa alipofungwa gerezani akiwa peke yake kwa zaidi ya miaka minne. Akiwa gerezani aliandika nyimbo zilizotegemea Biblia na huduma ya Kikristo.

Jioni hiyo isiyosahaulika, niliungana na Audrey Knorr, Karl Klein, na Fred Franz, Shahidi wa muda mrefu aliyezoezwa kuimba kwa sauti ya tenor, kuimba wimbo wenye kichwa “Nyumba kwa Nyumba” ambao baadaye uliingizwa kwenye kitabu cha nyimbo cha Mashahidi wa Yehova. Nathan Knorr, ambaye alisimamia kazi ya Mashahidi wakati huo, aliniomba niuimbe wimbo huo katika Kusanyiko la “Habari Njema za Milele” ambalo lilifanywa juma lililofuata huko Yankee Stadium, na nilifanya hivyo.

Mambo Yaliyoonwa Katika Kazi ya Mzunguko

Tulipokuwa tukitumikia huko Chicago, Illinois, mambo mawili yasiyosahaulika yalitukia. Kwanza, kwenye kusanyiko la mzunguko, Shirley alimwona Vera Stewart ambaye alikuwa amemhubiria Shirley na mama yake huko Kanada katikati ya miaka ya 1940. Wakati huo Shirley alikuwa na umri wa miaka 11 na alifurahi kusikia kuhusu ahadi za Mungu zilizo katika Biblia. Alimuuliza Vera, “Je, unafikiri ninaweza kuishi katika ulimwengu huo mpya?” Vera akajibu, “Bila shaka, Shirley.” Wote wawili walikumbuka maneno hayo. Kuanzia wakati huo alipokutana na Vera mara ya kwanza, Shirley aliweka mradi wa kumtumikia Yehova.

Pili, Shahidi fulani aliniuliza ikiwa ninakumbuka wakati nilipopata gunia la viazi lenye uzito wa kilo 20 kwenye mlango wa nyumba yetu wakati wa baridi kali mwaka wa 1958. Bila shaka ninakumbuka. Tulipata gunia hilo jioni moja baada ya kurudi nyumbani kwa shida kwa sababu ya dhoruba ya theluji! Ingawa hatukujua lilitoka wapi, tulimshukuru Yehova kwa uandalizi huo. Kwa sababu ya theluji, hatungeweza kutoka nyumbani kwetu kwa siku tano lakini tulifurahia kula chapati za viazi, viazi vilivyookwa, viazi vilivyokaangwa, viazi vilivyopondwa-pondwa, na mchuzi wa viazi! Hatukuwa na chakula kingine. Shahidi huyo hakutujua wala hakujua tulikoishi, lakini alikuwa amesikia kwamba mapainia fulani wanaoishi karibu walikuwa wakikabili hali ngumu. Alisema kwamba jambo fulani lilimchochea kuulizia mahali wenzi hao vijana walikoishi. Wakulima hujua mengi kuhusu majirani zao, hivyo alielekezwa kwenye nyumba yetu na kubeba viazi kupitia kwenye theluji.

Ninafurahia Maamuzi Yangu

Kufikia mwaka wa 1993, baada ya kufanya kazi ya kuzunguka kwa miaka 33, afya yangu ilidhoofika sana hivi kwamba ilinibidi niache utumishi huo. Kwa sababu ya hali, mimi na Shirley tukawa mapainia wa pekee wanaoruhusiwa kutotimiza saa za utumishi, na tunaendelea kutumikia mpaka leo. Ingawa ninasikitika kwamba sina nguvu za kufanya kazi ya kuzunguka, ninafurahi kwamba nilitumia nguvu zangu kufanya utumishi wa wakati wote.

Ndugu zangu watatu waliamua vingine. Hatimaye wote waliamua kufuatia mali na hawamtumikii Yehova kwa sasa. Baba alibatizwa katika mwaka wa 1958. Yeye na Mama waliwasaidia watu wengi wamjue Yehova, wajiweke wakfu Kwake, na kubatizwa. Wote wawili walikufa mwaka wa 1999. Hivyo, yaonekana uamuzi wangu wa kukataa umashuhuri wa ulimwengu na mali ulimwezesha baba yangu na wengi waliojifunza kweli ya Biblia pamoja naye na mama wapate tumaini la uzima wa milele. Mara nyingi mimi hujiuliza, ‘Ikiwa singefanya uamuzi huo, je, ningeendelea kumtumikia Yehova?’

Miaka mitano hivi baada ya kuacha kazi ya kuzunguka nilipata nafuu, hivyo nikaweza kuongeza utumishi wangu. Sasa ninatumikia nikiwa mwangalizi-msimamizi katika kutaniko moja la Desert Hot Springs, California. Pia nina pendeleo la kutumikia kama mwangalizi wa mzunguko wa badala, kutumika kwenye halmashauri za pekee, na wakati mwingine, kufundisha Shule ya Utumishi wa Painia.

Mpaka leo, Shirley ndiye rafiki yangu mkubwa. Ninafurahia sana kuwa naye. Kwa kawaida sisi huwa na mazungumzo ya kiroho yenye kusisimua, nasi hupendezwa na kweli za Biblia tunazozungumzia pamoja. Bado ninashukuru ninapokumbuka jinsi alivyouliza kwa upole zaidi ya miaka 47 iliyopita, “Lakini Charles, imani yako iko wapi?” Wenzi Wakristo vijana wakiulizana swali hilo wanaweza kupata shangwe na baraka ambazo tumepata katika utumishi wa wakati wote.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 John Sinutko alidumisha uaminifu wake akiwa Shahidi wa Yehova mpaka alipokufa mwaka wa 1996 akiwa na umri wa miaka 92.

^ fu. 11 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini hakichapishwi tena.

^ fu. 32 Katika toleo la Amkeni! la Februari 22, 1975 la Kiingereza, ukurasa wa 12-16, Bob Mackey anaeleza jinsi alivyopambana na kupooza.

[Picha katika ukurasa wa 20]

John, ndugu ya baba, katika 1935, mwaka ambao alibatizwa

[Picha katika ukurasa wa 22]

Nyumba yetu ya mbao

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wazazi wangu katika mwaka wa 1975. Waliendelea kuwa waaminifu hadi kifo

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa na Shirley leo