Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninawezaje Kuepuka Kufanya Ngono Kabla ya Ndoa?

Ninawezaje Kuepuka Kufanya Ngono Kabla ya Ndoa?

Vijana Huuliza  . . .

Ninawezaje Kuepuka Kufanya Ngono Kabla ya Ndoa?

“Nikiwa na umri wa miaka 19, nilifanya ngono na mvulana mmoja shuleni. Hilo lilinifanya niaibike na kufadhaika sana. Baadaye nilihisi kuwa sifai kitu.”—Laci. *

BIBLIA inaamuru hivi: “Ukimbieni uasherati.” (1 Wakorintho 6:18) Hata hivyo, inaonekana ni vijana wachache tu wanaotaka kutii maneno hayo ya Biblia na kuepuka kufanya ngono kabla ya ndoa. Baadhi ya vijana, kama vile Laci wametenda kupatana na tamaa zao nao wamefadhaika na kusumbuliwa na dhamiri.

Ni kweli kwamba si rahisi kuzuia tamaa za ngono. Kitabu Adolescent Development kinasema kwamba mabadiliko ya homoni wakati wa kubalehe “huongeza tamaa ya ngono.” Paul anakubali hivi, “Wakati mwingine, mimi hufikiri juu ya ngono bila sababu yoyote.”

Hata hivyo, profesa wa magonjwa ya watoto, Howard Kulin anasema: ‘Ni kosa kubwa kusema kwamba tamaa ya ngono [wakati wa kubalehe] inasababishwa na homoni.’ Anaeleza kwamba marafiki pia huchangia hali hiyo. Kwa kweli, uvutano wa marika unaweza kumwathiri mtu sana.

Katika kitabu chake A Tribe Apart, Patricia Hersch anasema kwamba “vijana wamejitenga katika ulimwengu wao wenyewe. . . . Mbali na kuwa marafiki tu, vijana hao hujitenga na watu wazima, na hufuata viwango, kanuni, na sheria zao wenyewe.” Hata hivyo, “viwango” na “sheria” hizo huwachochea kutosheleza tamaa za ngono badala ya kujizuia. Hivyo, huenda vijana wengi wakashawishiwa sana kufanya ngono kabla ya ndoa.

Hata hivyo, vijana Wakristo wameazimia kwa hekima kuepuka aina zote za uasherati, wakitambua kwamba Mungu huushutumu kwani ni mojawapo ya “matendo ya mwili.” * (Wagalatia 5:19) Lakini unawezaje kudumu ukiwa safi kiadili unapokabili mkazo mkubwa jinsi hiyo?

Tafuta Marafiki Wenye Hekima

Ingawa marafiki wabaya wanaweza kukuathiri vibaya, marafiki wazuri wanaweza kukufaidi. Biblia inasema: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima.” (Methali 13:20; 1 Wakorintho 15:33) Ripoti ya Shirika la Afya Ulimwenguni ilisema kwamba “vijana waliobalehe ambao wana uhusiano mzuri pamoja na wazazi wao, watu wazima wanaojali, na marika” na “ambao wamewekewa viwango na mipaka maishani . . . huona ni vigumu kuwachochea wengine kufanya ngono.”

Kuwa na uhusiano mzuri na wazazi wako kunaweza kuwa na matokeo mazuri sana. Joseph anakumbuka hivi: “Wazazi wangu walinisaidia sana kuepuka kufanya ngono.” Bila shaka, wazazi wanaomwogopa Mungu wanaweza kukuwekea viwango na mipaka inayotegemea Neno la Mungu. (Waefeso 6:2, 3) Wanaweza kukusaidia katika jitihada zako za kubaki safi kiadili.

Naam, huenda mwanzoni ikawa vigumu kuzungumza na wazazi wako kuhusu ngono. Lakini utatambua kwamba wanaelewa sana hisia zako. Kumbuka kwamba wakati mmoja wao pia walikuwa vijana. Hivyo, Sonja anawashauri vijana wengine hivi, “Ongea na wazazi wako, na usiaibike kuzungumza nao kuhusu ngono.”

Vipi ikiwa wazazi wako hawafuati viwango vya Biblia? Huku ukiendelea kuwaheshimu, huenda ukahitaji kutafuta msaada wa mtu mwingine. Paul aliyetangulia kutajwa anasema, “Mimi hupata msaada kutoka kwa wenzi wa ndoa Wakristo walio wakomavu.” Vilevile, msichana anayeitwa Kenji ambaye mama yake si mwamini anasema, “Ili kupata shauri mimi huwaendea watu wakomavu wanaoweza kunijenga kiroho.” Hata hivyo yeye anatoa tahadhari hii, “Mimi huwaepuka watu wasio na viwango vya juu vya maadili, hata wakidai kuwa waamini wenzangu.”

Wakati mwingine huenda ukahitaji kuwa mwangalifu kuhusu mashirika katika kutaniko la Kikristo. Biblia hutukumbusha kwamba kwa kawaida katika kikundi kikubwa kutakuwa watu fulani wasiojiendesha kwa heshima. (2 Timotheo 2:20) Utafanyaje ukigundua kwamba baadhi ya vijana katika kutaniko lenu ‘wanaficha jinsi walivyo’? (Zaburi 26:4) Epuka kushirikiana kwa ukaribu na vijana hao, na utafute marafiki watakaokusaidia kutimiza azimio lako la kubaki safi kiadili.

Kataa Habari Zinazodhuru

Pia epuka kutazama picha zinazoonyesha au kupendekeza ngono ambazo hupatikana kwenye vitabu, magazeti, video za muziki, michezo ya kompyuta, sinema, na Intaneti. Vyombo vya habari huonyesha kwamba kufanya ngono kabla ya ndoa kunavutia, kunafurahisha, na hakuna hatari yoyote. Habari hizo zina madhara gani? Kenji, aliyetajwa juu anakubali hivi: “Nilitazama kipindi fulani cha televisheni ambacho kilitukuza ngono na kupendekeza kwa njia isiyo ya moja kwa moja ngono kati ya watu wa jinsia moja. Basi, nikaanza kusahau jinsi Yehova anavyoyaona matendo hayo.”

Burudani inayopendwa sana inaficha madhara ya kufanya ngono kabla ya ndoa, yaani, mimba zisizotakiwa, ndoa za mapema, na magonjwa ya zinaa. Hivyo, usidanganywe na wale “wanaosema kwamba wema ni ubaya na ubaya ni wema.”—Isaya 5:20.

Yakumbuke maneno ya Methali 14:15: “Mtu asiye na uzoefu huamini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.” Ukiona picha chafu au habari zinazoeleza kuhusu ngono kwa njia isiyo ya moja kwa moja kwenye vitabu, kwenye Intaneti, au unapotazama televisheni, chukua hatua mara moja! Funga kitabu hicho, zima kompyuta, au badilisha stesheni ya televisheni! Kisha elekeza uangalifu wako kwa jambo lingine linalofaa. (Wafilipi 4:8) Kwa kufanya hivyo unaweza kukomesha tamaa mbaya kabla hazijasitawi.—Yakobo 1:14, 15.

Epuka Hali Zenye Kushawishi

Je, unamchumbia mtu fulani? Ikiwa ndivyo, unahitaji kuwa mwangalifu. Biblia inatuonya hivi: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” (Yeremia 17:9) Ni rahisi kuruhusu hisia za mahaba zikuongoze kwenye mwenendo mpotovu kingono. Hivyo, chukua hatua zinazofaa, kama vile kuwa na mtu wa tatu au kuwa miongoni mwa kikundi cha watu wenye mwenendo mzuri. Epukeni kuwa peke yenu mahali pasipofaa.

Lakini, huenda tayari mmekubaliana kufunga ndoa na unahisi si vibaya kuonyeshana hisia waziwazi. Hata hivyo, ripoti moja ya Shirika la Afya Ulimwenguni ilionya: “Inaonekana kwamba hata katika jamii ambazo hupinga kufanya ngono kabla ya ndoa, wanawake wengi hufanya hivyo wanapokaribia kufunga ndoa.” * Hivyo, jiwekeeni mipaka ili mjilinde dhidi ya kuumizwa hisia bila sababu.

Ni jambo lenye kushtua kwamba vijana wengi—hasa wasichana wadogo—hulazimishwa kufanya ngono. Kulingana na uchunguzi mmoja, “asilimia 60 ya wasichana huko Marekani waliokuwa wamefanya ngono kabla ya kufikia umri wa miaka 15 walifanya hivyo kwa kulazimishwa.” Mara nyingi, watu wanaowalazimisha hutumia nguvu ili kufanya ngono nao. (Mhubiri 4:1) Kwa mfano, Biblia hutuambia kwamba Amnoni, mwana wa mfalme Daudi, ‘alimpenda’ Tamari dada yake wa kambo na kwa kutumia ujanja akamlazimisha kufanya ngono naye.—2 Samweli 13:1, 10-16.

Hilo halimaanishi kwamba mtu hawezi kuepuka kubakwa au kulazimishwa kufanya ngono. Ukiwa macho kuona hatari, ukiepuka hali zenye kushawishi, na kuchukua hatua haraka kunapokuwa hatari, unaweza kufanikiwa kujilinda. *

“Unganisha” Moyo Wako

Tunatumaini kwamba madokezo tuliyoyazungumzia hapa yatakusaidia katika azimio lako la kubaki safi kiadili. Lakini hatimaye matendo yako yatategemea kilicho moyoni mwako. Yesu alisema uasherati “hutoka moyoni.” (Mathayo 15:19) Hivyo, unapaswa kuepuka kuwa na “moyo nusu nusu” (uvuguvugu) au kuwa na “mioyo miwili” (unafiki) kuhusu jambo hili muhimu.—Zaburi 12:2; 119:113.

Ukiona kuwa azimio lako linadhoofika au hujui la kufanya, sali kama Daudi, aliyesihi hivi: “Unganisha moyo wangu ili kuliogopa jina lako.” (Zaburi 86:11) Kisha, tenda kulingana na sala yako kwa kujifunza Biblia na vichapo vinavyoitegemea na kutumia mambo unayojifunza. (Yakobo 1:22) Lydia anasema: “Mimi huchochewa kuepuka vishawishi vya kufanya ngono kwa kukumbuka sikuzote kwamba ‘hakuna mwasherati au mtu asiye safi aliye na urithi wowote katika ufalme wa Mungu.’”—Waefeso 5:5.

Si rahisi kuepuka kufanya ngono kabla ya ndoa. Lakini kwa msaada wa Yehova unaweza kubaki safi kiadili na kuepuka kujiumiza au kuwaumiza wengine.—Methali 5:8-12.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 8 Ona makala “Vijana Huuliza . . . Kuna Ubaya Gani Kufanya Ngono Kabla ya Ndoa?” katika toleo letu la Julai 22, 2004.

^ fu. 21 Ona sura ya 29 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 23 Madokezo kama hayo yalitolewa katika makala za “Vijana Huuliza . . . ” kama vile “Kuudhiwa Kingono—Naweza Kujilindaje?” na “Nifanyeje Mpenzi Wangu Aache Kunitesa?” katika matoleo yetu ya Agosti 22, 1995, na Juni 22, 2004.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kuzungumza na wazazi wako kuhusu hisia zako kunaweza kukusaidia kubaki safi kiadili

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kuchumbiana mkiwa katika kikundi cha watu wenye mwenendo mzuri ni ulinzi