Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Talaka Ndilo Suluhisho?

Je, Talaka Ndilo Suluhisho?

Maoni ya Biblia

Je, Talaka Ndilo Suluhisho?

NCHINI Uingereza kasisi mmoja anawakaribisha watu waliokusanyika kwa ajili ya sherehe fulani. Mbele yake kuna wenzi wawili wa ndoa pamoja na marafiki na watoto. Je, hiyo ni sherehe ya arusi? Hata kidogo! Hiyo ni sherehe ya kuvunja ndoa yao. Naam, talaka zimekuwa za kawaida sana hivi kwamba makanisa fulani yameanzisha sherehe za talaka!

Je, unafikiria kumtaliki mwenzi wako? Ikiwa ndivyo, je, hilo litakuletea furaha zaidi maishani? Je, kuna hatua zozote unazoweza kuchukua ili kuishi kwa furaha na mwenzi wako?

“Nao Watakuwa Mwili Mmoja”

Wanadamu wawili wa kwanza walipounganishwa katika ndoa, Mungu alisema kwamba mwanamume “atashikamana na mke wake nao watakuwa mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Hivyo, ndoa ilipaswa kuwa kifungo cha kudumu. Hiyo ndiyo sababu iliyomfanya Yesu aseme kwamba “uasherati” ndio msingi pekee wa Kimaandiko unaoruhusu talaka kukiwa na uwezekano wa kufunga ndoa tena.—Mathayo 19:3-9. *

Hilo linakazia umuhimu wa kuwa mwaminifu katika ndoa. Lakini vipi ikiwa matatizo ya ndoa yako ni mazito sana?

Je, Ni Jambo la Hekima Kutalikiana?

Yesu alitupatia kanuni inayoweza kutusaidia kuchanganua maamuzi yetu aliposema hivi: “Hekima huonyeshwa kuwa yenye uadilifu kwa matendo yake.” (Mathayo 11:19) Talaka nyingi za leo zisizo na msingi unaofaa zimekuwa na matokeo gani?

Linda Waite, Profesa wa elimu ya kijamii wa Chuo Kikuu cha Chicago, aliyeongoza kikundi cha wataalamu kuchunguza ndoa zisizo na furaha anasema: “Faida za talaka zimetiliwa chumvi kupita kiasi.” Vivyo hivyo, baada ya kuchunguza maelezo ya maelfu ya watu kwa miaka 11, Profesa Michael Argyle wa Chuo Kikuu cha Oxford aligundua kwamba “watu wasio na furaha zaidi katika jamii ni wale waliotalikiana au kutengana.” Kwa nini inakuwa hivyo?

Ingawa huenda talaka ikatatua matatizo fulani, inaweza pia kutokeza matukio mengi yenye kuhuzunisha usiyoweza kuyadhibiti. Kwa kweli, uchunguzi umeonyesha kwamba talaka haipunguzi dalili za kushuka moyo wala kumfanya mtu ajiheshimu zaidi.

Hata ikiwa ndoa yako si “nzuri,” kuendelea kuishi na mwenzi wako kunaweza kukunufaisha. Wengi wanaojitahidi kufanya hivyo hupata furaha. Profesa Waite anasema: “Baada ya muda, matatizo mengi husuluhishwa na yaelekea wenzi wa ndoa hupata furaha zaidi.” Uchunguzi mmoja unaonyesha kwamba karibu watu 8 kati ya 10 ambao “hawakufurahia kabisa” ndoa yao lakini wakaepuka kutalikiana, “walifurahia ndoa” miaka mitano baadaye. Kwa hiyo, hata kunapokuwa na matatizo makubwa, wenzi wa ndoa wanashauriwa wasitalikiane upesi.

Hatua Unazoweza Kuchukua

Wale wanaofikiria kutalikiana wanapaswa kujiuliza ikiwa matarajio yao kuhusu ndoa yanafaa. Vyombo vya habari vimeonyesha kwa njia yenye kupotosha uhusiano wa kimahaba kati ya watu wawili ambao huongoza kwenye arusi yenye madoido mengi inayoishia katika maisha ya raha mustarehe. Mtu anapokuwa na matarajio kama hayo, baada ya arusi anaweza kuvunjika moyo na kusababisha mgogoro iwapo matarajio yake hayatimizwi. Hali ya kutoelewana inapozidi, wenzi hao huumia kihisia. Upendo hufifia na baada ya muda wanakuwa na hasira na chuki. Katika hali hizo, huenda watu fulani wakaona kwamba talaka tu ndilo suluhisho.—Methali 13:12.

Badala ya kuruhusu hisia zisizofaa ziathiri maoni yako, shirikiana na watu wanaoshikamana na ndoa zao. Wakristo wanahimizwa ‘waendelee kufarijiana na kujengana.’ (1 Wathesalonike 5:11) Bila shaka, wale walio na ndoa zenye matatizo wanahitaji kutiwa moyo na waamini wenzao.

Umuhimu wa Kuwa na Sifa Kama za Mungu

Mtume Paulo alishauri hivi: “Jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu.” (Wakolosai 3:12) Kuiga sifa za Mungu kunaweza kudumisha umoja katika ndoa wakati wa magumu.

Kwa mfano, Paulo aliandika: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine.” (Wakolosai 3:13) Mwanasaikolojia Christopher Peterson wa Chuo Kikuu cha Michigan anasema: “Kusamehe ndiyo sifa inayohusiana sana na kuwa na furaha.”

Fadhili, upole, na kusameheana hutokeza upendo, ambao ni “kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:14) Bila shaka, wakati fulani mlipendana sana. Je, mnaweza kupendana kama zamani? Hata mambo yawe magumu jinsi gani, jipe moyo. Kuna tumaini. Kwa kweli, kuendelea kuishi pamoja na kutumia kanuni za Biblia kunaweza kutokeza furaha nyingi kuliko unavyoweza kufikiri. Bila shaka, ukijitahidi kufanya hivyo utamfanya Yehova Mungu, aliye Mwanzilishi wa ndoa, ashangilie.—Methali 15:20.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova huheshimu haki ya mwenzi asiye na hatia ya kuamua kumtaliki au kutomtaliki mwenzi wake aliyefanya uzinzi. Ona toleo la Amkeni! la Aprili 22, 1999, ukurasa wa 5-9.