Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwisho wa Ubaguzi

Mwisho wa Ubaguzi

Mwisho wa Ubaguzi

JE, TUNAWEZA kutambua ikiwa tuna mielekeo ya kuwa wenye ubaguzi? Kwa mfano, je, sisi hukata kauli kuhusu sifa za mtu kwa kutegemea rangi ya ngozi yake, taifa lake, jamii yake, au kabila lake ingawa hatumjui? Au, je, tunaweza kumthamini kila mtu kwa sababu ya sifa zake za pekee?

Katika siku za Yesu, watu walioishi Yudea na Galilaya ‘hawakuwa na shughuli na Wasamaria.’ (Yohana 4:9) Msemo huu ulio katika Talmud unaonyesha wazi hisia za Wayahudi wengi: “Nisimwone Msamaria kamwe.”

Yaelekea hata mitume wa Yesu waliwabagua Wasamaria kwa kiasi fulani. Pindi moja, hawakukaribishwa kwa fadhili katika kijiji kimoja cha Wasamaria. Yakobo na Yohana waliuliza ikiwa wanaweza kuomba moto ushuke juu ya watu hao wasioitikia. Yesu aliwakemea, hivyo akawaonyesha kwamba maoni yao hayakufaa.—Luka 9:52-56.

Baadaye, Yesu alisimulia mfano wa mtu aliyeshambuliwa na wanyang’anyi alipokuwa akisafiri kutoka Yerusalemu akielekea Yeriko. Wayahudi wawili waliofuata dini hawakutaka kumsaidia. Lakini, Msamaria mmoja alisimama na kumfunga majeraha yake. Kisha akapanga mtu huyo atunzwe ili majeraha yake yapone. Msamaria huyo alionyesha kwamba alikuwa jirani kwelikweli. (Luka 10:29-37) Yaelekea mfano wa Yesu uliwasaidia wasikilizaji wake kutambua kwamba ubaguzi wao uliwazuia kuona sifa nzuri za wengine. Miaka michache baadaye, Yohana alirudi Samaria na kuhubiri katika vijiji vyake vingi, huenda hata katika kijiji alichokuwa ameomba kiharibiwe.—Matendo 8:14-17, 25.

Pia mtume Petro alihitaji kutenda bila upendeleo wakati malaika alipomwelekeza amhubirie Kornelio, ofisa wa jeshi la Roma, kumhusu Yesu. Petro hakuwa amezoea kushughulika na Wasio Wayahudi, na Wayahudi wengi hawakupenda askari-jeshi Waroma. (Matendo 10:28) Lakini Petro alipotambua kwamba Mungu alikuwa akielekeza mambo, alisema hivi: “Kwa hakika ninaona kwamba Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”—Matendo 10:34, 35.

Sababu ya Kushinda Ubaguzi

Ubaguzi haupatani na kanuni hii ya msingi ambayo Yesu alifundisha: “Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Ni nani ambaye angependa kudharauliwa kwa sababu tu ya mahali alipozaliwa, rangi ya ngozi yake, au malezi yake? Ubaguzi pia haupatani na kanuni za Mungu za kutoonyesha upendeleo. Biblia inafundisha kwamba Yehova “alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu, ili wakae juu ya uso wa dunia nzima.” (Matendo 17:26) Hivyo, watu wote ni ndugu.

Isitoshe, Mungu hushughulika na kila mtu mmoja-mmoja. Yeye hamshutumu mtu kwa sababu ya matendo ya wazazi wake au ya mababu zake. (Ezekieli 18:20; Waroma 2:6) Hata taifa fulani linapotudhulumu, hiyo si sababu ya kuwachukia watu mmoja-mmoja wa taifa hilo, ambao hawahusiki kibinafsi na dhuluma hiyo. Yesu aliwafundisha wafuasi wake ‘kuwapenda adui zao na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa.’—Mathayo 5:44, 45.

Mafundisho hayo yaliwasaidia Wakristo wa karne ya kwanza kushinda ubaguzi wao na kufanyiza udugu wa pekee wa kimataifa. Walijiona kuwa ndugu na dada na waliitana hivyo, ingawa walitoka katika tamaduni tofauti-tofauti. (Wakolosai 3:9-11; Yakobo 2:5; 4:11) Kanuni zilizowasaidia kufanya mabadiliko hayo, zinaweza kuwa na matokeo kama hayo leo.

Kushinda Ubaguzi Leo

Karibu sisi sote huwa na maoni fulani kuhusu watu tusiowajua, hata hivyo si lazima maoni hayo yatokeze ubaguzi. Kitabu The Nature of Prejudice kinasema: “Maoni yetu kuhusu mambo tusiyoyajua hutokeza ubaguzi tusipoyabadilisha baada ya kupata ujuzi zaidi.” Mara nyingi, ubaguzi unaweza kushindwa watu wanapojuana. Hata hivyo, kitabu hicho kinasema, “maoni yanaweza kubadilishwa ikiwa tu watu wanachangamana na kufanya mambo pamoja.”

Hivyo ndivyo John, wa kabila la Ibo huko Nigeria, alivyoacha kuwabagua Wahausa. Yeye anasema hivi: “Nilipokuwa katika chuo kikuu, nilikutana na wanafunzi Wahausa nasi tukawa marafiki, nami nikagundua kwamba wana sifa nzuri. Tulifanya kazi fulani pamoja na mwanafunzi mmoja Mhausa, nasi tulielewana, hali mwanafunzi niliyeshirikiana naye awali, ambaye ni wa kabila la Ibo, alikuwa mvivu.”

Njia ya Kushinda Ubaguzi

Kulingana na ripoti ya UNESCO Against Racism, “huenda elimu ikawa njia muhimu ya kupambana na aina mpya za ubaguzi wa rangi, upendeleo, na kuwatenga watu wa jamii nyingine.” Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba elimu ya Biblia ndiyo msaada bora zaidi wa kushinda ubaguzi. (Isaya 48:17, 18) Watu wanapotumia mafundisho ya Biblia, wao huwaheshimu wengine badala ya kuwashuku, na upendo humaliza chuki.

Mashahidi wa Yehova wametambua kwamba Biblia inawasaidia kushinda ubaguzi. Kwa hakika, Biblia huwachochea na kuwapa nafasi ya kushirikiana na watu wa tamaduni na jamii tofauti-tofauti. Christina, aliyenukuliwa katika makala ya utangulizi ya mfululizo huu, ni Shahidi wa Yehova. Anasema: “Mikutano yetu katika Jumba la Ufalme hunisaidia kujiamini. Nikiwa huko mimi hujihisi nikiwa salama kwa kuwa hakuna anayenibagua.”

Jasmin, ambaye pia ni Shahidi, anakumbuka jinsi alivyobaguliwa kwa mara ya kwanza akiwa na umri wa miaka tisa. Anasema: “Alhamisi ndiyo siku bora kwangu kwa sababu jioni mimi huenda kwenye Jumba la Ufalme. Huko, watu huonyesha kwamba wananipenda. Wao hunifanya nijihisi kuwa mtu wa maana badala ya kunidharau.”

Miradi ya kujitolea inayotegemezwa na Mashahidi wa Yehova huwawezesha pia watu wa malezi tofauti-tofauti kushirikiana. Simon alizaliwa Uingereza, ingawa familia yake ilitoka Karibea. Alibaguliwa sana alipokuwa akifanya kazi ya uashi katika kampuni za ujenzi. Lakini hilo halikutukia miaka yote aliyojitolea kutumikia katika miradi mbalimbali pamoja na ndugu zake wa imani moja naye. Simon anasema: “Nimefanya kazi pamoja na Mashahidi wenzangu wanaotoka katika nchi nyingi mbalimbali, lakini tumejifunza kuishi pamoja kwa amani. Baadhi ya marafiki zangu wa karibu walitoka katika nchi nyingine na malezi yao yalitofautiana na yangu.”

Bila shaka, Mashahidi wa Yehova hawajakamilika. Hivyo, huenda wanapambana na mielekeo ya ubaguzi. Lakini, wao huchochewa sana kufanya hivyo kwa sababu wanajua kwamba Mungu hana ubaguzi.—Waefeso 5:1, 2.

Kuna faida nyingi za kushinda ubaguzi. Tunaposhirikiana na watu wa malezi mbalimbali, maisha yetu huboreshwa. Zaidi ya hilo, kupitia Ufalme wake, hivi karibuni Mungu atafanyiza jamii ya kibinadamu yenye uadilifu. (2 Petro 3:13) Wakati huo ubaguzi utakomeshwa kabisa.

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

Je, Nina Ubaguzi?

Jiulize maswali yafuatayo ili uone ikiwa una ubaguzi:

1. Je, mimi huona kwamba watu wa jamii, eneo, au taifa fulani wana sifa mbaya kama vile ujinga, uvivu, au uchoyo? (Mizaha mingi huendeleza maoni hayo ya ubaguzi.)

2. Je, mimi huwalaumu wahamiaji au watu wa jamii nyingine ninapokuwa na matatizo ya kiuchumi au ya kijamii?

3. Je, nimeruhusu uadui wa muda mrefu kati ya jamii yetu na watu wa taifa lingine unifanye niwachukie watu wa taifa hilo?

4. Je, ninaweza kuona sifa za kibinafsi za kila mtu ninayekutana naye bila kujali rangi ya ngozi yake, utamaduni wake, au jamii yake?

5. Je, mimi hutaka kuwajua watu wa tamaduni nyingine? Je, mimi hujitahidi kufanya hivyo?

[Picha katika ukurasa wa 8]

Katika mfano wake wa Msamaria mwema, Yesu alitufundisha jinsi ya kushinda ubaguzi

[Picha katika ukurasa wa 8]

Alipokuwa katika nyumba ya Kornelio, Petro alisema: “Kwa hakika ninaona kwamba Mungu hana ubaguzi”

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mafundisho ya Biblia huwaunganisha watu wa malezi tofauti

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mashahidi wa Yehova hutumia mambo ambayo wamejifunza

[Picha katika ukurasa wa 10]

Christina—“Mikutano yetu katika Jumba la Ufalme hunisaidia kujiamini”

[Picha katika ukurasa wa 10]

Jasmin—“Watu huonyesha kwamba wananipenda. Wao hunifanya nijihisi kuwa mtu wa maana badala ya kunidharau”

[Picha katika ukurasa wa 10]

Simon, mfanyakazi wa kujitolea wa ujenzi—“Tumejifunza kuishi pamoja kwa amani”