Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana Wanaotetea Imani Yao

Vijana Wanaotetea Imani Yao

Vijana Wanaotetea Imani Yao

KUNA vijana wengi Mashahidi wa Yehova. Wanampenda Mungu nao hujitahidi kuishi kulingana na kanuni zake zilizoonyeshwa katika Biblia. Vijana hao hujivunia imani yao, nao huwaeleza wengine yale wanayoamini bila woga wakiwa shuleni. Fikiria mifano kadhaa.

Holly alipokuwa katika darasa la sita, yeye na wanafunzi wenzake darasani walipewa mgawo wa kuandika insha kuhusu swali hili: “Unawezaje kutatua tatizo la ugaidi bila kutumia jeuri?” Holly alitumia nafasi hiyo kuandika kuhusu tumaini lake la wakati ujao linalotegemea Biblia. Alieleza kwamba katika historia yote “mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.” (Mhubiri 8:9) Kisha akaonyesha kwamba tumaini la pekee la wanadamu ni Ufalme wa Mungu. Aliandika hivi: “Kwa kuwa Yesu ndiye Mfalme aliyetawazwa wa Ufalme huo, matatizo yote kutia ndani ugaidi yataondolewa.” Holly alieleza jinsi Yesu atakavyotimiza mambo yasiyoweza kutimizwa na mtawala yeyote wa kibinadamu. Aliandika hivi: “Yesu alionyesha angekuwa mtawala wa aina gani alipokuwa duniani. Aliwapenda na kuwajali watu. Alionyesha nguvu alizokuwa nazo kwa kuponya magonjwa na kufufua wafu. Hakuna serikali yoyote ya wanadamu inayoweza kuwafufua wafu. Lakini Ufalme wa Mungu utafanya hivyo.” Holly alimalizia insha yake kwa taarifa hii, “Mungu ndiye atakayesuluhisha mambo, si wanadamu.”

Mwishoni mwa insha hiyo, mwalimu aliandika hivi: “Lo! Umetumia hoja zenye nguvu sana, Holly. Na ulizifikiria vizuri.” Pia mwalimu huyo alifurahi kwamba Holly alionyesha marejeo ya Maandiko katika insha yake. Holly alitumia nafasi hiyo kumweleza mwalimu wake kuhusu Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ambayo ni programu ya kila juma ya kujifunza kutoa hotuba na kufundisha inayofanywa na Mashahidi wa Yehova. Mwalimu wake alifurahia kupata kitabu kinachotumiwa katika Shule ya Huduma.

Jessica pia amepata nafasi ya kuzungumza kuhusu imani yake anapoandika insha shuleni. Anasema hivi: “Nimeandika insha tatu kuhusu yale ninayoamini. Insha moja ilihusu Mashahidi wa Yehova na haki za kidini. Mwalimu aliiweka katika maktaba ili wale wanaotaka waisome. Hivi karibuni niliandika insha kuhusu ubatizo wangu na jinsi siku hiyo ilivyokuwa muhimu kwangu. Wanafunzi huwapa wanafunzi wenzao nakala za insha zao, kwa hiyo wanafunzi wenzangu darasani walisoma insha yangu. Msichana mmoja alisema: ‘Umeandika insha nzuri. Nimefurahi kujua mambo ambayo kila Shahidi wa Yehova anapaswa kufanya. Pongezi kwa ubatizo wako!’ Msichana mwingine alisema hivi: ‘Insha yako ilipendeza sana! Ninafurahi kwamba imani yako ni yenye nguvu sana!’ Mvulana mmoja aliandika hivi kwa ufupi: ‘Wewe ni mwenye busara. Pongezi.’”

Melissa alipokuwa na umri wa miaka 11, alipata nafasi ya pekee ya kutetea imani yake. “Muuguzi wa shule yetu alikuja darasani wakati wa somo la sayansi ili kutufundisha kuhusu mfumo wa kinga. Suala la kutiwa damu mishipani lilitokea. Baada ya somo hilo, nilimweleza mwalimu wangu wa sayansi juu ya video yetu kuhusu damu. Nilikuja nayo shuleni siku iliyofuata, na mwalimu akaenda nayo nyumbani na kuitazama pamoja na familia yake. Siku iliyofuata, alikuja nayo shuleni na kuionyesha kwa madarasa mawili, kutia ndani darasa letu. Kisha akatoa maelezo mazuri kuhusu Mashahidi wa Yehova na kuwaambia wanafunzi kwamba ikiwa si jitihada zetu, haingekuwa rahisi kupata matibabu mengine badala ya damu. Aliponirudishia video hiyo, aliniuliza hivi, ‘Ninawezaje kupata video hii kwa ajili ya maktaba ya shule?’ Basi, nilimpa video moja. Alisisimuka sana, nami pia nikasisimuka!”

Holly, Jessica, na Melissa ni baadhi ya vijana wengi Mashahidi wa Yehova ambao hutii himizo la Biblia la kumkumbuka Muumba wao. (Mhubiri 12:1) Je, wewe unafanya hivyo pia? Ikiwa ndivyo, uwe na hakika kwamba unafanya moyo wa Yehova ushangilie.—Methali 27:11; Waebrania 6:10.

Nyinyi vijana mnapowaeleza wanafunzi wenzenu na walimu wenu kuhusu imani yenu, mnatoa ushahidi wenye nguvu kumhusu Yehova Mungu na makusudi yake. Vilevile, hilo huimarisha imani yenu na kuwafanya mjivunie pendeleo la kuwa watumishi wake. (Yeremia 9:24) Pia mnapata ulinzi mnapotoa ushahidi shuleni. Jessica anaeleza hivi: “Faida moja ya kuzungumza kuhusu imani yangu ni kwamba wanafunzi wenzangu hawajaribu kunishawishi kufanya mambo yanayopingana na Biblia.”

[Picha katika ukurasa wa 12]

Holly

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Jessica

[Picha katika ukurasa wa 13]

Melissa