Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna Ubaya Gani Kunywa Kupita Kiasi?

Kuna Ubaya Gani Kunywa Kupita Kiasi?

Vijana Huuliza . . .

Kuna Ubaya Gani Kunywa Kupita Kiasi?

“Ijapokuwa tulikuwa tumekunywa kileo (pombe) kwa saa kadhaa, mimi na rafiki yangu tuliondoka kwenye karamu saa saba usiku tukiwa na chupa ya kileo. Tulianza kwenda nyumbani huku tukinywa. Niligutuka wakati jua lilipochomoza, nami nikatambua kwamba tulikuwa tumepotea njia. Kumbe tulikuwa tukitembea kwenye barabara kuu. Ni ajabu kwamba hatukugongwa na gari.”—Clay. *

WENGINE husema kwamba kunywa kupita kiasi ni kunywa kwa kusudi la kulewa. Ripoti moja ya Taasisi ya Marekani Inayoshughulikia Ulevi na Madhara Yake ilitoa maelezo hususa zaidi. Ilisema kwamba kunywa kupita kiasi hutokea wakati “mwanamume anapokunywa chupa tano au zaidi za kileo mfululizo, na mwanamke kunywa chupa nne au zaidi mfululizo.”

Maofisa wa afya nchini Marekani wamesema kwamba kunywa kupita kiasi “ni tatizo kubwa linaloathiri afya ya jamii.” Kulingana na uchunguzi uliofanywa kuhusu watoto wa shule za sekondari nchini Uingereza, Scotland, na Wales, “asilimia 25 hivi ya watoto walio kati ya umri wa miaka 13 na 14 walidai kwamba wamewahi kunywa angalau chupa tano za kileo katika pindi moja.” Karibu nusu ya watoto waliochunguzwa wenye umri wa miaka 15 na 16 walidai kwamba walikuwa wamefanya vivyo hivyo.

Katika uchunguzi mmoja uliofanywa Marekani, wanafunzi 2 kati ya wanafunzi 5 wa vyuo walikuwa wamekunywa kupita kiasi angalau mara moja majuma mawili kabla ya uchunguzi huo. Kulingana na Wizara ya Afya ya Marekani, “vijana milioni 10.4 hivi walio kati ya umri wa miaka 12 na 20 walisema kwamba wao hunywa kileo. Milioni 5.1 kati yao hunywa kupita kiasi na milioni 2.3 hunywa kupita kiasi angalau mara tano kila mwezi.” Uchunguzi uliofanywa nchini Australia ulionyesha kwamba wasichana ndio wanaokunywa kileo zaidi ya wavulana, kwani wao hunywa chupa 13 hadi 30 katika pindi moja!

Wengi hunywa kupita kiasi kwa sababu ya kuchochewa na vijana wenzao. Mtafiti Carol Falkowski anasema: “Michezo mipya ya kunywa kileo imeongezeka, nayo ni hatari: inahusisha kufanya mambo katika kikundi ili kulewa. Kwa mfano, katika michezo fulani washiriki hutakiwa wanywe kileo kidogo wakati hususa unapofika katika maonyesho ya televisheni au wakati wa mazungumzo ya kikundi.”

Hatari za Kunywa Kupita Kiasi

Ijapokuwa watu fulani huona kunywa kupita kiasi kuwa mchezo, huo ni mchezo hatari sana! Kunywa kileo kingi sana huzuia oksijeni isifike kwenye ubongo; na mifumo muhimu ya mwili inaweza kuacha kufanya kazi. Dalili zinaweza kutia ndani kutapika, kupoteza fahamu, na kupumua polepole au kwa njia isiyo ya kawaida. Nyakati nyingine, mtu anaweza kufa. Mwezi mmoja hivi baada ya kumaliza shule ya sekondari, kijana mmoja mwenye umri wa miaka 17 anayeitwa Kim alienda katika karamu ambayo iliwaruhusu watu kunywa kileo kingi watakavyo. Kim alikunywa chupa 17 za kileo kabla ya kupoteza fahamu. Dada yake mkubwa alifika huko na kumpeleka Kim nyumbani. Asubuhi iliyofuata, mama yake alimpata Kim akiwa amekufa.

Huenda kunywa kupita kiasi kusisababishe kifo moja kwa moja mara nyingi, lakini kunaweza kuhatarisha afya yako. Jerome Levin, mtaalamu wa afya ya akili, anasema: “Kileo kinaweza kuharibu kiungo chochote cha mwili wako. Viungo vinavyoathiriwa zaidi ni mfumo wa neva, ini, na moyo.” Makala moja katika gazeti Discover inasema: “Uchunguzi wa karibuni unaonyesha kwamba vijana wanaokunywa kileo wanajitafutia matatizo. Kwa kuwa ubongo wa vijana huendelea kukua hata wanapokuwa katika miaka ya ishirini, huenda vijana wanaokunywa kupita kiasi wanaharibu sana uwezo wao wa akili.” Kunywa kupita kiasi kunahusianishwa pia na kuongezeka kwa chunusi, kupata makunyanzi mapema, kunenepa, kuharibika kwa viungo mwilini, kutegemea kileo, na matumizi sugu ya dawa za kulevya.

Kuna hatari nyingine zinazohusiana na kunywa kupita kiasi. Ukilewa, unaweza kudhulumiwa kwa urahisi. Unaweza kushambuliwa au hata kubakwa. Zaidi ya hayo, unaweza kuwahatarisha wengine kwa kufanya mambo ambayo hata hungefikiria kuyafanya ukiwa timamu katika akili. Hivyo, Biblia inaonya kwamba ukinywa kupita kiasi, “macho yako mwenyewe yataona mambo mageni, nao moyo wako mwenyewe utasema mambo yaliyopotoka.” (Methali 23:33) Madhara yanayoumiza yanaweza kutia ndani kupoteza marafiki, kutofanya vizuri shuleni na kazini, kushtakiwa kwa kuhusika katika uhalifu, na umaskini. *Methali 23:21.

Kichocheo cha Kunywa

Licha ya hatari hizo, watu huchochewa sana kunywa kileo, na katika nchi nyingi kinapatikana kwa urahisi. Hata matangazo ya televisheni na magazeti hutukuza unywaji wa kileo. Hata hivyo, mara nyingi vijana hunywa kupita kiasi kwa sababu ya kuchochewa na marafiki zao.

Katika uchunguzi mmoja kuhusu kileo uliofanywa nchini Australia, asilimia 36 ya vijana waliohojiwa walisema kwamba wao hunywa kileo “kwenye karamu ili wakubaliwe na marafiki zao.” Katika karamu ya ulevi yenye fujo, mtu mwenye haya anaweza kuwachangamsha wenzake anapohimizwa nao anywe chupa moja baada ya nyingine. Msichana anayeitwa Katie alipelekwa nyumbani akiwa amepoteza fahamu kwa sababu ya kufanya hivyo. “Rafiki” yake alikuwa amempa kileo na kumwambia: “Katie, wewe ni mtu mzima. Unapaswa kumeza mara moja, si kuonja kidogo-kidogo tu.”

Tamaa ya kujifurahisha na kukubaliwa na wengine ni yenye nguvu sana hivi kwamba ingawa kuna uthibitisho mwingi kwamba kunywa kupita kiasi ni hatari, bado zoea hilo linapendwa na wengi.

Utatendaje?

Basi, utafanya maamuzi gani kuhusu kunywa kileo? Je, utatenda kama vijana wenzako? Kumbuka maneno ya Biblia katika Waroma 6:16: “Je, hamjui kwamba ikiwa mnaendelea kujitoa wenyewe kwa yeyote kuwa watumwa ili kumtii yeye, ninyi ni watumwa wake kwa sababu mnamtii yeye?” Ukiwaruhusu vijana wenzako wakuongoze katika kila jambo, basi utakuwa mtumwa wao. Biblia inakuhimiza ujiamulie mambo. (Methali 1:4) Ina mashauri yanayoweza kukusaidia kuepuka kufanya makosa mazito. Fikiria yale inayosema kuhusu kileo.

Bila shaka, Biblia haiwakatazi watu kunywa kileo, wala haiwazuii vijana wasijifurahishe. Hata hivyo, inaonya dhidi ya kunywa kupita kiasi. Andiko la Methali 20:1 linasema hivi: “Divai ni mdhihaki, kileo husababisha msukosuko, na kila mtu anayepotezwa nacho hana hekima.” Naam, kileo kinaweza kumfanya mtu atende bila akili au kupiga kelele! Ni kweli kwamba kileo kinaweza kukufurahisha kwa muda mfupi, lakini ukinywa kupita kiasi, kinaweza ‘kukuuma kama nyoka’ kwa kukusababishia majeraha ya kimwili na maumivu ya kihisia.—Methali 23:32.

Pia inafaa kukumbuka kwamba katika nchi nyingi watu huruhusiwa kunywa kileo wanapofikia umri fulani. Wakristo hutii sheria kama hizo. (Tito 3:1) Sheria hizo zimewekwa zikulinde.

Mwishowe, jambo la muhimu zaidi ni kufikiria madhara ya kiroho yanayotokana na kunywa kupita kiasi. Yehova Mungu anataka umtumikie “kwa akili yako yote,” wala si kwa akili iliyoathiriwa kwa kunywa kileo kupita kiasi! (Mathayo 22:37) Neno la Mungu linashutumu kunywa “divai kupita kiasi” na pia “mashindano ya kunywa.” (1 Petro 4:3) Kwa hiyo, kunywa kupita kiasi ni kinyume cha mapenzi ya Muumba wetu. Zoea hilo linaweza kumzuia mtu asiwe na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu.

Unapaswa kufanya nini ikiwa wewe hunywa kupita kiasi? Pata msaada upesi kwa kuzungumza na mzazi au Mkristo mkomavu. * Sali kwa Yehova Mungu na umwombe msaada. Bila shaka, yeye ni “msaada unaopatikana kwa utayari wakati wa taabu.” (Zaburi 46:1) Kwa kuwa mara nyingi watu hunywa kupita kiasi na kunywa kileo kabla ya kufikisha umri kwa sababu ya kuchochewa na marafiki, ingefaa utafute marafiki wengine na ufanye mabadiliko makubwa kuhusu burudani unayochagua. Si rahisi kufanya mabadiliko hayo, lakini kwa msaada wa Yehova unaweza kufanikiwa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 11 Kulingana na uchunguzi mmoja nchini Marekani, “vijana ambao mara nyingi hunywa kupita kiasi hukosa kwenda shuleni, hawafanyi vizuri katika masomo yao, huumizwa au kujeruhiwa, na kuharibu mali mara nane zaidi ya wale ambao hawanywi kupita kiasi.”

^ fu. 21 Huenda msaada wa daktari anayestahili ukahitajiwa katika visa fulani.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 15]

Habari za Kushtua Kuhusu Kunywa Kupita Kiasi

Habari zinazofuata zinaonyesha madhara yenye kuhuzunisha ambayo wanafunzi wa vyuo nchini Marekani wanapata kutokana na kunywa kupita kiasi:

Vifo: Wanafunzi 1,400 wa vyuo walio kati ya miaka 18 na 24 hufa kila mwaka kutokana na majeraha wanayopata bila kutarajia wanapokuwa wamelewa, kutia ndani misiba ya barabarani

Majeraha: Wanafunzi 500,000 walio kati ya miaka 18 na 24 hupata majeraha bila kutarajia wanapokuwa wamelewa

Kushambuliwa: Zaidi ya wanafunzi 600,000 walio kati ya miaka 18 na 24 hushambuliwa na mwanafunzi mwenzao aliyelewa

Kutendewa Vibaya Kingono: Zaidi ya wanafunzi 70,000 walio kati ya miaka 18 na 24 hutendewa vibaya kingono au kubakwa na mchumba wao wakiwa wamelewa au mchumba wao akiwa amelewa

[Hisani]

Source: The U.S. National Institute on Alcohol Abuse and Alcoholism

[Picha katika ukurasa wa 13]

Vijana wenzako wanaweza kukuchochea kunywa kileo kupita kiasi