Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maisha Yangu Katika Sarakasi

Maisha Yangu Katika Sarakasi

Maisha Yangu Katika Sarakasi

SIMULIZI LA JOHN SMALLEY

“Mabibi, mabwana, na watoto, karibuni kwenye maonyesho bora zaidi ulimwenguni!” Kwa watu wengi, maneno hayo ya kiongozi wa sarakasi humaanisha kwamba huo ndio mwanzo wa maonyesho yenye kusisimua ya wanyama, wacheshi, na wanasarakasi. Lakini kwa familia yetu maneno hayo yalimaanisha kwamba ni wakati wa kuanza kazi kwenye hema kuu la maonyesho ya sarakasi ya kampuni iliyoitwa Ringling Brothers and Barnum & Bailey Circus.

NILIZALIWA mwaka wa 1951. Huenda ukasema kwamba nilizaliwa nikiwa na “unga wa mbao katika viatu vyangu”—msemo ambao umetokana na zoea la kutandaza unga wa mbao kwenye sakafu ya mahema makubwa ya sarakasi. Tangu mimi na ndugu yangu tulipoanza kutembea, tulishiriki katika maonyesho ya sarakasi.

Wazazi wangu, Harry na Beatriz, walijiunga na kikundi cha sarakasi cha Clyde Beatty Circus kabla sijazaliwa. Mama yangu alikuwa mwimbaji na aliimba nyimbo za Kihispania akiwa amevalia mavazi ya kitamaduni ya Mexico. Baba yangu alikuwa mwanamuziki, naye alishirikiana na John Philip Sousa, kiongozi wa bendi na mtungaji wa muziki wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Kisha, katika miaka ya 1950, baba yangu alipewa kazi ya kucheza tarumbeta kubwa katika bendi mashuhuri ya Ringling Brothers. Huenda alipata kazi hiyo kwa sababu ya kushirikiana na Sousa.

Baadaye tulifanya kazi na vikundi mbalimbali vya sarakasi na hatimaye tukafanya kazi na kikundi cha Al G. Kelly & Miller Brothers Circus, ambacho kilikuwa kikundi mashuhuri sana nchini Marekani. Kikundi hicho kilikuwa na mahema matatu makubwa. Hema moja lilikuwa na simba, simba-milia, tembo, fisi, na wanyama wengine kutoka nchi nyingine.

Hema la pili lilikuwa la maonyesho ya ziada. Kwa kawaida lilikuwa na mtu aliyeonekana kana kwamba anameza upanga, mtu aliyedai kuwa nusu mwanamume na nusu mwanamke, watu wafupi, jitu, na watu wengine wenye maumbile ya ajabu. Tukiwa watoto tulijifunza mambo mengi kwa kuishi na watu tofauti-tofauti. Watu fulani waliwadhihaki, lakini sisi tuliwaona kuwa watu wa familia. Tulifanya kazi nao, tukala nao, na kuishi pamoja nao karibu mwaka mzima.

Hema la tatu ndilo lililokuwa hema kuu la maonyesho nalo lilikuwa na sehemu tatu, na maonyesho yalifanywa wakati uleule katika sehemu zote tatu. Kwa kawaida, maonyesho hatari zaidi au yenye kupendeza zaidi yalifanywa katika sehemu ya katikati.

Maisha ya Mwanasarakasi

Mimi na ndugu yangu tulikuwa wanasarakasi tangu utotoni. Pia tulishiriki Maonyesho ya Wild West, ambapo tuliigiza sehemu ya wavulana wadogo Wahindi. Familia ya Wahindi wa Marekani wa kabila la Choctaw ambao walishiriki katika maonyesho hayo walitufundisha kucheza dansi za Kihindi.

Kwa kawaida tulianza shughuli zetu mwendo wa saa kumi na mbili asubuhi. Tulianza siku kwa kujitayarisha kuhamia mji mwingine. Waigizaji wote walifanya kazi ya kubomoa, kusafirisha, na kuunganisha tena vifaa vya sarakasi. Kwa mfano, ijapokuwa baba yangu alikuwa mwanamuziki, aliendesha pia lori kubwa lenye tembo saba. Nyakati nyingine, mimi, mama yangu, na ndugu yangu tulibebwa na baba katika lori lake.

Kwa kawaida tulihamia eneo jipya kila siku na kufanya maonyesho mawili. Siku ya Jumapili tulifanya onyesho moja tu alasiri, kisha tukapumzika pamoja na familia zetu jioni. Kila Jumapili, baba yangu aliiburudisha familia yetu, kama vile kwa kutupeleka mjini kunywa kinywaji kitamu au kutupeleka kwenye sinema jioni.

Ilikuwa kazi ngumu kuunganisha vifaa vya sarakasi. Hata tembo walisaidia. Jinsi gani? Walitumiwa kuvuta milingoti mirefu ya yale mahema matatu. Ncha moja ya mlingoti iliingizwa ndani ya pete ya hema kisha tembo alivuta ncha ile nyingine hadi mlingoti huo uliposimama wima. Baada ya kusimamisha milingoti yote na kuwasha jenereta za umeme zilizotumiwa kwa ajili ya taa, tulianza kujitayarishia maonyesho ya alasiri.

Kujifunza Mbinu Mpya

Katikati ya maonyesho ya alasiri na ya jioni, watoto wengi waliohusika katika sarakasi walijifunza kupiga samasoti, kutembea juu ya waya, kurusha vitu angani na kuvidaka, na kubembea. Tulifundishwa na wanasarakasi wenye ujuzi wa miaka mingi ambao walitoka katika familia za wanasarakasi. Namkumbuka mwanasarakasi Mwitaliano aliyenifundisha kupiga samasoti mara ya kwanza. Nilianza nikiwa na umri wa miaka minne hivi. Kwanza alinifunga kwa mkanda wa usalama, kisha akanitegemeza kwa mikono yake huku akikimbia kando yangu. Hatimaye, aliacha kunishikilia, nami nikapiga samasoti bila kusaidiwa.

Niliumia mara moja tu wakati wa gwaride iliyofanywa kuzunguka hema kuu. Mimi na ndugu yangu tulikuwa nyuma ya mcheshi aliyekuwa na tumbili wawili na mbele ya kundi la tembo. Nilipokuwa nikitembea na kurusha mikono yangu, yaelekea nilimshtua tumbili mmoja ambaye alishika mkono wangu na kuniuma sana. Uzuri ni kwamba sikuambukizwa ugonjwa wowote. Lakini bado nina alama ndogo kwenye mkono wangu wa kushoto, nayo hunikumbusha niwe mwangalifu nyakati zote ninaposhughulika na wanyama wa mwituni hata wawe wenye kupendeza na wapole jinsi gani.

Nilijifunza Masomo Muhimu

Maisha yetu tukiwa wanasarakasi hayakuathiri maisha yetu ya familia. Nyakati zote wazazi wangu walijitahidi kutenga wakati kutufundisha kanuni na maadili yanayofaa. Ningali nakumbuka baba yangu akinibeba kwenye goti lake na kunishauri nisiwabague watu wa jamii au malezi tofauti na yangu. Hilo lilikuwa somo muhimu kwani niliishi na watu wenye maumbile tofauti na waliotoka katika mataifa mbalimbali.

Mama yangu pia alitufundisha masomo muhimu. Nyakati nyingine hema kuu lilijaa watazamaji, lakini nyakati nyingine walikuwa wachache. Mama alizoea kutuambia hivi: “Mnaigiza ili kuwafurahisha watu (huku akipiga makofi) si kupata pesa. Iwe kuna watazamaji wengi au wachache, nyakati zote fanyeni yote mnayoweza.” Sijasahau maneno hayo. Alimaanisha kwamba tunapaswa kupendezwa na watazamaji, wawe wengi au wachache.

Zaidi ya kuigiza katika maonyesho, mimi na ndugu yangu tulipewa kazi ya kufanya usafi baada ya maonyesho kwa kuokota takataka ndani ya hema kuu. Hayo yalikuwa mazoezi bora.

Kuanzia Aprili hadi Septemba, tulisafiri kutoka sehemu moja hadi nyingine, kwa hiyo hatukuweza kwenda shuleni kama watoto wengine. Wakati wa baridi kali tulikaa kwenye makao yetu makuu huko Hugo, Oklahoma. Wakati huo tulienda shuleni kwa miezi mitano hivi. Pia vikundi vingine vya wanasarakasi vilikaa huko Hugo katika kipindi hicho, hivyo kulikuwa na watoto wengi waliokabili hali hiyo. Wasimamizi wa elimu katika mji huo walipanga ratiba ya pekee kwa ajili yetu.

Siku Ambayo Maisha Yetu Yalibadilika

Asubuhi ya Septemba 16, 1960, baba yangu aliamka mwendo wa saa 11 asubuhi na kuanza kututayarisha kwa ajili ya safari. Siku hiyo, mama yangu aliamua tusafiri pamoja na wanasarakasi wengine badala ya kusafiri na baba katika lori lake la kubeba tembo.

Tulipofika mahali ambapo maonyesho yangefanyiwa, mimi na ndugu yangu tulianza kutazama mazingira. Kisha tukamsikia mtu mmoja akipiga kelele akisema: “Msiba mbaya umetokea. Smalley na kiongozi wa sarakasi wamekufa.” Mwanzoni sikuamini jambo hilo. Nilifikiri kwamba amekosea. Baadaye nilitambua kwamba tayari mama yangu alikuwa ameenda mahali msiba huo ulipotukia. Baba yangu alikuwa akiendesha lori kuteremka barabara ya mlimani karibu na Placerville, California, wakati breki ziliposhindwa kufanya kazi. Inaonekana kwamba uzito wa tembo ulifanya sehemu ya nyuma ya lori kuangukia sehemu ya mbele. Tanki ya mafuta ilifinywa sana na kulipuka, hivyo kumwua baba yangu na kiongozi wa sarakasi papo hapo. Nilihuzunika sana siku hiyo. Nilimpenda baba yangu sana. Tulikuwa marafiki wakubwa.

Baada ya kumzika Baba mahali alikozaliwa huko Rich Hill, Missouri, tulirudi mahali tulipokuwa tukikaa wakati wa baridi kali huko Hugo, Oklahoma, huku kikundi chetu cha sarakasi kikiendelea na safari ili kumaliza maonyesho ya msimu huo. Wakati huo, sisi wavulana tulienda shule kwa ukawaida. Hatukuwa tumezoea kufanya hivyo. Hata hivyo, tulitarajia kwa hamu msimu uliofuata ili tushiriki katika Maonyesho ya Kelly Miller. Lakini maisha yetu yakabadilika kwa njia isiyotarajiwa.

Tunaanza Kujifunza Biblia

Siku moja nilipofika nyumbani baada ya shule, mama yangu alinijulisha kwa mwanamke ambaye alikuwa amekuja kutufundisha Biblia. Aliitwa Jimmie Brown na alikuwa Shahidi wa Yehova. Sikutaka kujifunza Biblia hata kidogo. Kwa miaka mingi nilitamani kurudi kwenye maonyesho ya sarakasi na kujifunza kubembea. Mimi na ndugu yangu tulikuwa tumetengeneza bembea kati ya miti miwili ili kujizoeza. Hata hivyo, sote tulianza kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano katika kikundi cha Mashahidi wanane tu huko Hugo. Baada ya muda, mama yangu aliamua kuacha kazi ya sarakasi na kuendelea kujifunza Biblia. Nilikubali uamuzi wake huku nikitokwa na machozi. Ilikuwa vigumu kushikilia uamuzi wetu wakati wanasarakasi wenzetu walipokuja kututembelea na kutuuliza sababu ya kutojiunga nao.

Sikuwa nimefanya kazi nyingine yoyote ila kushiriki katika sarakasi. Wakati mmoja nilihisi ni kana kwamba tunapuuza mambo ambayo baba yetu alikuwa ametimiza. Lakini jambo la kushangaza ni kwamba kifo chake ndicho kilichonifanya nijifunze Biblia kwa kuwa nilichochewa hasa na tumaini la ufufuo. Bado ninashikilia tumaini hilo sana. Ninataka kuwa miongoni mwa watu wa kwanza watakaomkaribisha baba yangu anapoingia katika Paradiso hapa duniani, kama ilivyoahidiwa.—Ufunuo 20:12-14.

Wenzi wa ndoa Mashahidi wanaoitwa Reeders, walitusaidia kutambua kwamba kuna familia kubwa katika tengenezo la Yehova. Naam, nimeona ukweli wa jambo hilo! Kile kikundi kidogo cha Mashahidi wa Yehova kikawa kutaniko lenye familia kadhaa zinazoabudu pamoja. Pia ni lazima niwataje Robert na Carol Engelhardt, wenzi wa ndoa walionilea kiroho. Walinishauri kwa upendo na kwa uthabiti nilipokuwa kijana.

Upendo huo wa Wakristo wakomavu ulitusaidia kukabiliana na pengo kubwa tulilokuwa nalo maishani. Na nimejionea hilo kwa njia mbalimbali katika maisha yangu nikiwa Mkristo. Kwa miaka mingi niliishi Oklahoma na Texas, na katika kila kutaniko nilikutana na ndugu na dada wengi Wakristo wenye upendo. Baadhi ya akina ndugu wenye umri mkubwa walinipa mwongozo na kunitia moyo kwa upendo. Naam, wao ni baba zangu wa kiroho.

Naanza Kusafiri Tena

Miaka michache iliyopita, mama yangu alikufa. Aliendelea kujifunza Biblia kwa bidii na kubaki akiwa Mkristo mwaminifu hadi kifo. Ninajua kwamba atashangilia wakati Mungu atakapowafufua waaminifu wake. Ninapongojea siku hiyo, mimi hufarijiwa ninapotambua kwamba tengenezo la Yehova limeniwezesha kuwa na familia kwa njia nyingi.

Nilifurahi hasa nilipopata mke, anayeitwa Edna, miongoni mwa watu wa Mungu. Baada ya kufunga ndoa tulifanya mipango ili tushiriki katika kazi ya wakati wote ya kufundisha Biblia. Ili kujiruzuku, nilifanya kazi nikiwa ripota wa televisheni. Sikuwa na ujuzi wowote wala mazoezi yoyote kuhusu kazi hiyo, lakini mazoezi niliyopata nikiwa mwalimu wa Biblia katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova yaliniwezesha kustahili kazi hiyo. Hatimaye nikawa msimamizi wa habari kwenye kituo cha redio. Hata hivyo, sikukusudia kuwa mwandishi-habari mashuhuri. Badala yake, mimi na Edna tulijitolea kufundisha kweli za Biblia mahali popote penye uhitaji.

Katika mwaka wa 1987, niliombwa niwe mwangalizi wa mzunguko ili nitembelee makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Kwa kuwa mimi ni mzee ambaye amejitolea kusafiri, ninatembelea makutaniko mbalimbali kila juma ili kuwatia moyo ndugu na dada zangu wa kiroho na kuwazoeza katika kazi ya kufundisha Biblia. Sasa familia yangu ya kiroho ni kubwa sana. Ingawa mimi na mke wangu hatujawahi kuwa na watoto, tumepata wana na mabinti wengi wa kiroho katika tengenezo la Yehova.

Kwa njia fulani inashangaza kwamba ingawa miaka mingi imepita, bado ninasafiri kutoka mji mmoja hadi mwingine. Niliacha sarakasi na kuanza kazi ya kusafiri! Mara kwa mara mimi hujiuliza ikiwa ningefaulu kujua kubembea. Je, ningetimiza ndoto yangu ya utotoni ya kupiga samasoti mara tatu hewani? Hata hivyo, mawazo hayo hupotea ninapofikiria ahadi ya Mungu ya kufanya dunia kuwa paradiso.—Ufunuo 21:4.

Ni kweli kwamba nilizaliwa nikiwa na “unga wa mbao katika viatu vyangu.” Lakini ninakumbuka maneno haya ya Biblia: “Jinsi ilivyo yenye kupendeza miguu ya wale wanaotangaza habari njema ya mambo mema!” (Waroma 10:15) Pendeleo la kuwasaidia watu kumjua Mungu ni kubwa kuliko mafanikio yoyote ambayo ningepata nikiwa mwanasarakasi. Baraka za Yehova zimenifanya niridhike na maisha yangu!

[Picha katika ukurasa wa 19]

Baadhi ya wanasarakasi wenzetu, na baba yangu akiwa na tarumbeta yake kubwa

[Picha katika ukurasa wa 21]

Sasa, nikiwa na mke wangu, Edna