Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shule za Watoto Zisizo na Vitu vya Kuchezea

Shule za Watoto Zisizo na Vitu vya Kuchezea

Shule za Watoto Zisizo na Vitu vya Kuchezea

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI UJERUMANI

Asubuhi moja watoto walipofika shuleni, hawakuona chochote darasani ila viti na madawati. Walitafuta vitu vya kuchezea na wanyama wa kuchezea, lakini hawakupata chochote. Hakukuwa na vitabu wala vidude vya kujengea vitu. Hata karatasi na makasi hayakuwepo. Vitu vyote vya kuchezea vilikuwa vimeondolewa na havingerudishwa hadi baada ya miezi mitatu. Ni nini kilichokuwa kimetokea?

Shule hiyo ya watoto ni mojawapo ya shule nyingi nchini Austria, Ujerumani, na Uswisi ambazo zinashiriki katika mradi mpya wa pekee wa kuondoa vitu vya kuchezea katika shule za watoto wadogo. Ingawa huenda mradi huo, ambao unasifiwa sana na wataalamu wa afya wa Muungano wa Ulaya, ukaonwa kuwa wa ajabu, kusudi lake ni kuzuia mazoea sugu. Katika miaka ya karibuni, watafiti wamegundua kwamba watu wanaositawisha uwezo wa kuishi na wengine vizuri wakiwa wachanga, hawatumbukii kwa urahisi katika mazoea sugu. Gazeti moja linaripoti kwamba uwezo huo unatia ndani “ustadi wa kuwasiliana, uwezo wa kuanzisha urafiki haraka, kutatua hali ya kutoelewana, kuwajibika, kujiwekea miradi, kutambua matatizo, kutafuta msaada, na kupata masuluhisho.” Watu wanaounga mkono mradi huo wanasema kwamba uwezo huo unapaswa kusitawishwa watoto wakiwa wachanga, na kutokuwa na vitu vya kuchezea huchangia kusudi hilo kwa kuwafanya wawe wabunifu na wajiamini.

Mradi huo wa miezi mitatu wa kuondoa vitu vya kuchezea vya watoto umepangwa vizuri sana, na wazazi na watoto wameelezwa juu yake. Mwanzoni, watoto fulani huhangaika wanapokosa vitu vya kuchezea. Ripoti hiyo inasema kuwa “watoto katika shule fulani huzusha fujo kwa majuma manne ya kwanza” hivi kwamba wapangaji wa mradi huo hushindwa la kufanya. Hata hivyo, watoto hujifunza kuzoea hali hiyo na kubuni mambo. Kwa kuwa hawana vitu vya kuchezea, watoto hushauriana, hupanga, na kucheza pamoja zaidi, na hivyo kuboresha ustadi wao wa lugha na wa kuanzisha urafiki. Wengine ambao zamani walitumia vitu vya kuchezea na hivyo kuepuka kucheza na watoto wengine, sasa wanaanzisha urafiki. Wazazi pia wameona mabadiliko fulani mazuri. Wamesema kwamba sasa watoto wao wanacheza kwa adabu na ni wabunifu zaidi.