Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuwasaidia na Kuwalinda Vijana

Jinsi ya Kuwasaidia na Kuwalinda Vijana

Jinsi ya Kuwasaidia na Kuwalinda Vijana

INAHUZUNISHA sana msichana mchanga anapopata mimba kabla ya kuolewa. Hata hivyo, tatizo la wasichana wachanga kupata mimba limeenea sana, nalo huathiri kila mtu kwa njia fulani. Matokeo mabaya ya tatizo hilo yanathibitisha kwamba amri hii ya Mungu inafaa: “Ukimbieni uasherati.”—1 Wakorintho 6:18.

Hata hivyo, nyakati nyingine msichana ambaye amefundishwa njia za Mungu huchagua kuzipuuza au kuzikataa. Anafanya ngono na kupata mimba. Wakristo wa kweli wanapaswa kutendaje? Kijana huyo aliyefanya dhambi anapotubu, wazazi wake na washiriki wengine wa kutaniko wanapaswa kumsaidia na kumtegemeza kwa upendo.

Fikiria tena kisa cha Nicole. Wazazi wake walikuwa wakimsaidia awe Shahidi wa Yehova. Hivyo, alipopata mimba nje ya ndoa walivunjika moyo sana. Hata hivyo, Nicole anakumbuka hivi: “Wakristo wenzangu walikuwa wakija nyumbani na kunitia moyo nijifunze Biblia na kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova.”

Mashahidi wa Yehova hawakubali kamwe ukosefu wa adili katika ngono. Lakini wanatambua kwamba kwa kutumia kanuni za Biblia, watenda dhambi wanaweza ‘kugeuzwa.’ (Waroma 12:2) Wanaamini kabisa kwamba Mungu huwasamehe watenda-dhambi wanaotubu. (Waefeso 1:7) Pia wanatambua kwamba mtoto hana hatia, hata kama amezaliwa nje ya ndoa. Kwa hiyo, badala ya kumshutumu mtoto huyo, washiriki wa kutaniko la Kikristo humtendea kwa upendo, huruma, na fadhili, sawa na vile wangewatendea watoto wengine.—Wakolosai 3:12.

Mama mmoja asiye na mwenzi wa ndoa alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Alikubali haraka ujumbe wa Biblia na kufanya mabadiliko makubwa maishani mwake. Alisema hivi kuhusu Mashahidi: “Wote walipendezwa na mimi na watoto wangu kikweli. Walinipa chakula, mavazi, na kunitegemeza kifedha ilipohitajika. Walijitolea kuwa yaya wa mtoto wangu nilipoanza kuhubiri na Mashahidi wa Yehova. Walifanya yote wawezayo kunisaidia kumpenda Yehova kikweli.”

Kuzuia

Hata hivyo, ni afadhali zaidi kuwasaidia vijana kuepuka matatizo hayo. Hivyo, Mashahidi wa Yehova hujitahidi sana kufanya familia iwe yenye uchangamfu na upendo kwa ajili ya watoto wao. Mashahidi hujaribu kuwafundisha watoto wao kumpenda Yehova Mungu na sheria zake badala ya kuwatisha kwamba watapata UKIMWI au mimba. (Zaburi 119:97) Wanaamini kwamba watoto wanapaswa kuelezwa habari sahihi kuhusu ngono. Zaidi ya hilo, wanaamini kwamba watoto wanahitaji kufundishwa kanuni za maadili zilizo katika Biblia. (2 Timotheo 3:15) Mafundisho hutolewa kwenye Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova katika maeneo mbalimbali. Hata hivyo, wazazi Mashahidi wanatiwa moyo kuwafundisha watoto wao Biblia, wao wenyewe. Vitabu kama vile Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, vimechapishwa ili kuwasaidia wazazi kuwafundisha watoto wao. *

Watu wanaofuata viwango thabiti vya Biblia huwa tofauti na watu ambao hufanya mambo yaliyopotoka kiadili ambayo yameenea sana ulimwenguni. Lakini kufuata viwango hivyo kunaweza kusaidia mamilioni ya wasichana wachanga waepuke matatizo yanayowapata wasichana wachanga wenye mimba.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Wakristo wa kweli huwatendea kwa upendo na kwa fadhili akina mama wasio na wenzi