Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kukabili Magumu ya Kuwa Mama Mchanga

Kukabili Magumu ya Kuwa Mama Mchanga

Kukabili Magumu ya Kuwa Mama Mchanga

MSICHANA mchanga anapopata mimba, analazimika kukabili maamuzi ambayo watu wazima hukabili. Mama mmoja mchanga alisema hivi: “Ni kana kwamba nina miaka 40. Sikufurahia maisha yangu ya utotoni.” Kwa hakika, msichana mchanga anapogundua kwamba ana mimba anaweza kuogopa na kuhangaika sana.

Ikiwa wewe ni msichana mchanga na una mimba, unaweza kuhisi hivyo. Hata hivyo, hutatimiza chochote ukiruhusu hisia zisizofaa zikulemee. Biblia inasema, “Anayeuangalia upepo hatapanda mbegu; naye anayetazama mawingu hatavuna.” (Mhubiri 7:8; 11:4) Mkulima anayehangaishwa sana na hali ya hewa hatachukua hatua zinazohitajiwa. Usiruhusu mahangaiko yakuzuie kutenda. Muda si muda itakubidi uendelee kufanya shughuli za kawaida na kutimiza madaraka yako.—Wagalatia 6:5.

Utafanyaje? Huenda watu fulani wakakushauri utoe mimba. Lakini watu wanaotaka kumpendeza Mungu hawatoi mimba, kwani Biblia husema kwamba kutoa mimba ni kinyume cha sheria ya Mungu. (Kutoka 20:13; 21:22, 23; Zaburi 139:14-16) Machoni pa Mungu, uhai wa kila kiini-tete—hata ikiwa mimba imetungwa nje ya ndoa—ni wenye thamani.

Vipi kuolewa na baba ya mtoto wako na kumlea mtoto huyo mkiwa pamoja? Huenda ukafikiri kwamba ndoa inaweza kukuondolea aibu. Lakini hata baba mchanga akihisi kwamba ana daraka la kusaidia kumlea mtoto wake, mara nyingi ndoa si suluhisho linalofaa. * Hata ingawa kijana anaweza kutunga mimba, haimaanishi kwamba yuko tayari kihisia na kiakili kuwa mume na baba mzuri. Wala haimaanishi kwamba anaweza kumruzuku mke na mtoto wake. Isitoshe, ikiwa hamko katika dini moja na kijana huyo, kufunga ndoa naye kutakuwa kukiuka shauri la Biblia la kuoa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Imeonekana kwamba kukimbilia ndoa haraka-haraka, ambayo huenda haitadumu, kunaweza kusababisha maumivu na kuteseka zaidi.

Vipi kumkabidhi mtoto atunzwe na wengine? Ijapokuwa hatua hiyo ni afadhali kuliko kutoa mimba, unapaswa kukumbuka kwamba licha ya hali ngumu unazokabili, bado una nafasi ya kumtunza na kumlea mtoto wako.

Kukabili Magumu

Ni kweli kwamba si rahisi kumlea mtoto bila mwenzi. Hata hivyo, kwa kufuata kanuni za Biblia kadiri uwezavyo na kwa kumtegemea Mungu akuimarishe na kukuongoza, unaweza kufanikiwa kukabiliana na magumu mengi. Zifuatazo ni baadhi ya hatua zitakazokusaidia kukabiliana na magumu hayo.

Rekebisha uhusuano wako na Mungu. Tambua kwamba kufanya ngono kabla ya ndoa ni dhambi mbele za Mungu, ni kuvunja viwango vyake vya juu vya adili. (Wagalatia 5:19-21; 1 Wathesalonike 4:3, 4) Hivyo, hatua ya kwanza muhimu ni kutubu na kumwomba Mungu msamaha. (Zaburi 32:5; 1 Yohana 2:1, 2) Ni kweli kwamba huenda ukaona hustahili kupata msaada wake. Hata hivyo, Yehova anaahidi kwamba atatusamehe, naye huwasaidia wale wanaotubu dhambi zao. (Isaya 55:6, 7) Kwenye Isaya 1:18, Yehova anasema: “Hata dhambi zenu zikiwa nyekundu [nzito sana], zitafanywa kuwa nyeupe kama theluji [zitasafishwa kabisa].” Biblia hutia moyo watenda-dhambi wawaendee wazee waliowekwa rasmi kutanikoni ili kupata msaada wa kiroho.—Yakobo 5:14, 15.

Acha kufanya ngono kabla ya ndoa. Huenda hiyo ikamaanisha kuvunja uhusiano kati yako na baba ya mtoto wako. Kuendeleza uhusiano huo kabla ya kufunga ndoa kunaweza kukufanya uendelee kujihusisha na mambo yanayomchukiza Mungu. Usisahau kamwe kwamba ingawa sheria za Mungu ni thabiti, zinatulinda. Nicole aliyenukuliwa mapema katika mfululizo huu anakiri hivi: “Nimetambua kwamba Mungu husema kweli. Anataka tufaidike.”—Isaya 48:17, 18.

Waambei wazazi wako. Huenda ukaogopa kwamba wazazi wako watakukasirikia. Ni kweli kwamba watakasirika na kuhangaika wanapojua una mimba. Huenda wakahisi kwamba wameshindwa kutimiza madaraka yao na hata wanaweza kujilaumu kwa sababu ya mwenendo wako mbaya. Hata hivyo, ikiwa kwa kweli wazazi wako wanamcha Mungu, muda si muda wataacha kuhuzunika. Wao ni wazazi wako na wanakupenda licha ya makosa yako. Wanapoona kwamba umetubu, bila shaka watamwiga baba ya mwana mpotevu na watakusamehe kwa upendo.—Luka 15:11-32.

Toa shukrani. Mara nyingi wazazi, watu wa ukoo, na marafiki husaidia sana. Kwa mfano, wazazi wako wanaweza kuhakikisha kwamba unapata matibabu. Baada ya kupata mtoto, wanaweza kukusaidia kujua jinsi ya kumtunza mtoto mchanga; pia wanaweza kujitolea kuwa yaya wa mtoto wako. Nicole anasema hivi kuhusu mama yake: “Nilipata mtoto, lakini mama yangu ndiye aliyenisaidia sana.” Huenda pia marafiki wakakusaidia. Kwa busara wanaweza kukupatia nguo za mtoto na vitu vingine vinavyoweza kukusaidia. (Methali 17:17) Unapotendewa kwa fadhili, fuata shauri la Biblia la ‘kuonyesha shukrani.’ (Wakolosai 3:15) Ukisema asante, hawatahisi kwamba umepuuza fadhili zao.

Jifunze kuwa mzazi. Bila shaka, hungependa kutegemea familia yenu na marafiki zako daima. Kwa hiyo, jifunze stadi zitakazokusaidia kumtunza mtoto wako na kushughulikia mambo ya nyumbani. Ni kazi ngumu kujifunza jinsi ya kumtunza mwanadamu mwenye mahitaji mengi sana. Kuna mambo mengi unayopaswa kujifunza kuhusu chakula, afya, na mambo mengine yanayohusiana na kumtunza mtoto. Inapendeza kwamba Biblia inawasihi wanawake Wakristo wenye umri mkubwa wawaelimishe wanawake vijana kuwa “wafanyakazi nyumbani.” (Tito 2:5) Bila shaka, mama yako—na labda washiriki wengine wenye umri mkubwa katika kutaniko la Kikristo—wanaweza kukupa mazoezi muhimu ya kushughulikia mambo hayo.

Tumia pesa kwa hekima. Biblia inasema kwamba “pesa ni ulinzi.” (Mhubiri 7:12) Mtoto anapozaliwa, kunakuwa na mahitaji mengi ya kifedha.

Huenda ikafaa utafute msaada unaoandaliwa kwa umma. Hata hivyo, mara nyingi msichana bado atahitaji kutegemea wazazi wake kifedha. Ikiwa ndivyo ilivyo kwako, basi, ni jambo la hekima na upendo kupunguza gharama zako kwa kadiri iwezekanavyo. Ingawa ungependa mtoto wako awe na vitu vipya, unaweza kuokoa pesa kwa kununua bidhaa ambazo tayari zimetumiwa.

Jaribu kupata elimu. Andiko la Methali 10:14 linasema: “Wenye hekima ndio wanaoweka hazina ya ujuzi.” Ingawa maneno hayo yanahusu hasa ujuzi wa Biblia, yanatumika pia kuhusu elimu ya kilimwengu. Unahitaji kupata stadi za kujiruzuku.

Ni kweli kwamba si rahisi kwenda shule huku ukimtunza mtoto. Hata hivyo, kukosa elimu ya msingi kunaweza kukufanya wewe na mtoto wako muishi maisha ya umaskini, kutegemea misaada ya umma, kuwa na mapato madogo, kuishi katika nyumba za hali ya chini, na kukosa chakula kinachofaa. Kwa hiyo, ikiwa inawezekana, endelea kupata elimu. Mama ya Nicole alisisitiza kwamba amalize shule, na hivyo Nicole akapata mazoezi ambayo yalimwezesha kuwa msaidizi wa wakili na kujiruzuku.

Kwa nini usichunguze ikiwa kuna masomo ya ziada unayoweza kupata? Ikiwa ni vigumu kwako kwenda shuleni, chunguza ikiwa unaweza kusomea nyumbani. Kwa mfano, kupata elimu kupitia mawasiliano ya barua kunaweza kukufaa sana.

Unaweza Kufanikiwa

Kumlea mtoto nje ya ndoa si jambo rahisi kwa msichana mchanga. Lakini unaweza kufanikiwa! Ukiwa na subira, nia, na msaada wa Yehova Mungu, unaweza kuwa mzazi mwenye upendo na ustadi, ambaye anatimiza madaraka yake. Na watoto wa akina mama wasio na wenzi wanaweza kukua na kuwa watu wazima wenye sifa nzuri. Ama kwa hakika, utafurahi kuona mtoto wako akikubali msaada na mazoezi unayompa na kumpenda Mungu.—Waefeso 6:4.

Nicole anasema hivi: “Licha ya magumu, kwa msaada wa Mungu, nilifurahia kumsaidia msichana wangu mdogo awe mtu mzima mwenye fadhili na heshima, na anayechukua madaraka kwa uzito. Ninapomtazama, mimi hukumbuka siku nilizokosa usingizi lakini pia mimi hufurahi sana.”

Hata hivyo, watu wazima wanapaswa kuwatendeaje akina mama wachanga pamoja na watoto wao? Je, kuna njia yoyote ya kuwasaidia vijana kuepuka matatizo yanayotokana na kupata mimba wakiwa wachanga?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Unaweza kupata habari zaidi kuhusu madaraka na matatizo yanayowapata akina baba wachanga ambao bado hawajafunga ndoa katika makala za “Vijana Huuliza . . . ” katika matoleo ya Amkeni! ya Aprili 22, 2000, na Mei 22, 2000.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mama wachanga hukabili magumu mengi ya kulea watoto wao

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kukimbilia ndoa kabla ya wakati si suluhisho

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wazee Wakristo wanaweza kuwasaidia vijana waliofanya dhambi kurekebisha uhusiano wao na Mungu

[Picha katika ukurasa wa 11]

Ni jambo la hekima akina mama wasio na wenzi kupata elimu ya msingi