Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Taarifa: Wasomaji wengi walituandikia kuhusu ule mfululizo wenye kichwa “Kuyaelewa Magonjwa ya Kihisia” katika toleo la Januari 8, 2004. Zifuatazo ni baadhi ya barua tulizopokea.

Nimesoma makala nyingi sana ambazo zimenigusa moyo katika magazeti yenu, lakini hakuna makala ambayo imewahi kunigusa moyo kama mfululizo huo. Niliposoma kuhusu ndugu na dada zetu walio na ugonjwa huu, niliwahurumia sana. Ninatumaini kwamba watanisamehe ikiwa nimewahi kuwaambia jambo lolote lenye kuudhi. Tafadhali endeleeni kuchapisha makala kama hizo. Makala hizo hutusaidia kupendana sana na kuwajali wengine.

S. W., Marekani

Ilipogunduliwa kwamba nina ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika, nilihisi kuwa maisha yangu yameharibika. Nililia sana, lakini pia nilisali kwa Yehova. Sala yangu ilijibiwa juma hili nilipopokea gazeti la Amkeni! linalozungumzia magonjwa ya kihisia. Ni kana kwamba Yehova ananipenda mimi binafsi. Makala hizo zimeniimarisha nisonge mbele.

R. T., Kanada

Miaka mitatu iliyopita iligunduliwa kwamba mto- to wetu mwenye umri wa miaka 12 alikuwa na ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika. Mara nyingi yeye huhisi kwamba hakuna mtu anayefahamu hali yake na kwamba Yehova hamjali. Tulimpa gazeti hilo, naye akalisoma mara moja. Alilia huku akisema hivi: “Mama, kuna watu wanaoelewa. Yehova pia anaelewa hali yangu.” Daktari anayemtibu alifurahia kupokea gazeti hilo, nami nikafurahia kuzungumza naye kuhusu Biblia.

L. P., Marekani

Nilimsihi Yehova katika sala na kumwomba makala kuhusu ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika. Nimepokea toleo la Amkeni! la Januari 8, 2004, miezi miwili tu tangu nilipotoa sala yangu. Madokezo mliyotoa yamenisaidia kumtumikia Yehova zaidi.

M. S., Mexico

Nilitumia habari hiyo ya mfululizo kufanya kazi fulani chuoni. Msimamizi wa idara ya wenye mahitaji ya pekee, aliomba nakala ya gazeti hilo ili alitumie kuwafundisha wafanyakazi kuhusu ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika. Endeleeni kuchapisha makala hizo bora. Zinanufaisha watu wengi.

K. R., Marekani

Mlionyesha umuhimu wa kutofautisha mgonjwa na ugonjwa. Makala hizo zinatusaidia tukiwa wazee wa kutaniko kuelewa hali ya ndugu na dada walio na ugonjwa huo na kuwasaidia.

R. P., Italia

Dada yangu ana ugonjwa wa kushuka moyo. Nililia niliposoma makala hizo kwani nilitambua kwamba nilikuwa nikiongea kuhusu hali yake bila kumwelewa. Sasa ninafahamu kwamba badala ya kuchoshwa na dada yangu, ninapaswa kujitahidi kwa subira kuelewa hali yake.

D. P., Marekani

Hali yangu inafanana sana na ile iliyoelezwa katika makala hizo. Nililia na kuacha kujilaumu, na hivyo nikahisi nimefarijiwa. Nilimpa daktari wangu gazeti hilo. Yeye hunitia moyo niendelee kushikamana na imani yangu.

A. L., Ufaransa

Nina umri wa miaka 13. Mara nyingi mimi hutamani kufa. Gazeti la Amkeni! limenisaidia sana kukabili hisia hizo. Sasa najua kwamba Yehova anatujali na kwamba yeye hutusikiliza!

M. S., Marekani

Nimekuwa nikifikiri kwamba kushuka moyo husababishwa na ubinafsi, na kwamba mtu anahitaji tu kuacha kushuka moyo. Lakini niliposoma makala hizo, nilitambua kwamba mimi ndiye niliyekuwa na ubinafsi kwa kutowajali wengine.

R. N., Marekani

Asanteni sana kwa makala hizo zilizoandikwa vizuri. Zina habari zinazoweza kutumiwa katika matibabu ya ugonjwa huo. Niko katika chuo kikuu na ninasomea jinsi ya kutoa ushauri wa kisaikolojia, nami nitawapa wateja wangu habari hiyo.

P. Y., Marekani

Nimekuwa nikipambana na ugonjwa wa kushuka moyo kwa zaidi ya miaka kumi. Makala hizo zilionyesha umuhimu wa mtu kuandika mambo anayofanya, nami nitafanya hivyo. Ninapokosa kufika mikutanoni, rafiki yangu ambaye ni Mkristo hunisaidia sana kwa kurekodi habari inayozungumziwa huko kwa ajili yangu.

M. S., Japani

Nimekuwa na dalili za ugonjwa huo kwa miaka kumi. Mara nyingi mimi na mume wangu tumesoma makala hizo kwa makini. Hivyo, tunaweza kuzungumza kuhusu hisia zangu na kuhangaikiana zaidi.

I. H., Hungaria

Nimefikiria kujiua kwa sababu ya kulaumiwa sana na washiriki wa familia yangu mwenyewe. Hata hivyo, makala hizo zilinipa tumaini kwa kuonyesha kwamba Yehova anaelewa hali yangu. Sasa mimi huhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova na ninahubiri pia.

M. B., Marekani

Nimefarijika kujua kwamba kuna wengine wanaokabili hali kama yangu. Mfululizo huo ulikuwa na madokezo mazuri, nami nitayatumia kadiri niwezavyo. Tafadhali endeleeni kuchapisha makala kama hizo kwa kuwa zinaweza kunufaisha watu wengi.

V. L., Urusi

Mimi ni mzee wa miaka 68, na nimekuwa na ugonjwa wa kushuka moyo kwa miaka kumi hivi. Wazee Wakristo pia wanahitaji msaada, na baadhi yao hushuka moyo sana. Niliguswa moyo sana kusoma kuhusu jinsi watu wengine wanavyokabiliana na ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika.

B. A., Marekani

Habari iliyo katika makala hizo ilinichochea kutafuta matibabu. Imemsaidia pia mke wangu kushughulika vizuri zaidi na ugonjwa wangu wa kushuka moyo. Nyakati zote mimi hufurahi kuona jinsi makala zenu zilivyo sahihi na za wakati unaofaa.

C. B., Ujerumani

Iligunduliwa kwamba nina ugonjwa wa kushuka moyo miezi mitatu kabla ya kusoma mfululizo huu. Itikio langu la kwanza ni sawa na lile lililoonyeshwa katika mfululizo huo, yaani kushtuka na kuogopa kumwambia mtu mwingine juu ya hali yangu. Makala zenu zilinisaidia kujua kwamba wengine wanaelewa hali yangu, nami sihisi upweke.

A. G., Austria

Baba yangu amekuwa na ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika tangu nilipokuwa mchanga. Aliposisimuka kupita kiasi nilichukizwa naye, ingawa nilijua kwamba alikuwa mgonjwa. Lakini niliposoma mfululizo huo, nilifahamu mambo aliyokuwa akikabili. Nililia nilipokuwa nikisoma makala hizo. Nitazungumza naye nitakapoenda nyumbani. Nitajaribu niwezavyo kuvumilia hali yake.

S. S., Japani

Binti ya rafiki yangu ana ugonjwa wa akili, nami nilimwambia kwamba anaweza kupata nafuu kwa kusoma na kusali sana. Habari iliyomo katika ukurasa wa 10 wa gazeti hilo ilionyesha kwamba sikuwa na maoni yanayofaa. Kusali na kujifunza husaidia lakini hakuwezi kuponya magonjwa. Asanteni kwa kunisahihisha.

B. D., Marekani

Nimekuwa nikilia kila mara mtu anaponiambia kwamba tukiwa Wakristo hatuwezi kushuka moyo. Hata hivyo, makala hizo zimenisaidia, nami nimefarijiwa kujua kwamba kuna wengine pia wanaokabili tatizo hilo.

P. B., Uingereza