Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunapaswa Kuwatendeaje Wazee?

Tunapaswa Kuwatendeaje Wazee?

Maoni ya Biblia

Tunapaswa Kuwatendeaje Wazee?

KATIKA majira ya kiangazi ya mwaka wa 2003, maelfu ya watu walikufa barani Ulaya kutokana na mawimbi makali zaidi ya joto kuwahi kutukia huko kwa kipindi cha miaka 60. Wengi wao walikuwa wazee. Wengine walikuwa wameachwa peke yao na watu wao wa ukoo ambao walikuwa wameenda likizo. Pia inasemekana wengine waliachwa au kupuuzwa na wafanyakazi wa hospitali wenye shughuli nyingi au wafanyakazi wa makao ya kuwatunzia wazee. Gazeti Le Parisien liliripoti kwamba huko Paris, maiti 450 hazikuchukuliwa. Gazeti hilo lilizusha swali hili kuhusu hali ya wale waliokufa bila kutambulishwa: “Kwani tunaishi katika hali za aina gani hivi kwamba tunasahau baba zetu, mama zetu, na akina babu na nyanya?”

Kwa kuwa kila mwezi watu 795,000 ulimwenguni hufikia umri wa miaka 65, mojawapo ya mahangaiko makubwa leo ni kushughulikia mahitaji ya wazee. Nancy Gordon, msimamizi-mshirika wa miradi ya kuchunguza idadi ya watu katika Idara ya Sensa ya Marekani, anasema: “Idadi ya watu wazee ulimwenguni imeongezeka sana kuliko wakati mwingine wowote na tunahitaji kuzingatia sana jinsi nchi mbalimbali zinavyoshughulikia matatizo ya kuzeeka.”

Muumba wetu pia anawajali wazee. Hata Neno lake, Biblia, linatuonyesha jinsi wanavyopaswa kutendewa.

Kuwaheshimu Wazee

Sheria ambayo Mungu alimpa Musa iliwahimiza watu wawaheshimu wazee. Sheria hiyo ilisema: “Unapaswa kusimama mbele ya mtu mwenye mvi, nawe umwonyeshe ufikirio mtu mzee.” (Mambo ya Walawi 19:32) Waabudu wa Mungu watiifu walitazamiwa “kusimama” mbele ya wazee ili (1) kuonyesha kwamba wanawaheshimu na (2) kuonyesha kwamba wanamcha Mungu. Hivyo, wazee walipaswa kuheshimiwa na kuonwa kuwa wenye thamani.—Methali 16:31; 23:22.

Ingawa Wakristo leo hawako chini ya Sheria ya Musa, kanuni zake huonyesha maoni ya Yehova na mambo anayotaka yatangulizwe, na hilo linaonyesha wazi kwamba anawathamini sana wazee. Washiriki wa kutaniko la Kikristo katika karne ya kwanza walielewa kanuni hizo. Hilo linaonyeshwa katika kitabu cha Biblia cha Matendo. Kulikuwa na wajane wenye uhitaji miongoni mwa Wakristo waliokuwa Yerusalemu wakati huo. Inaonekana kwamba baadhi yao walikuwa wazee. Mitume waliwaweka rasmi “wanaume saba waliothibitishwa” kuhakikisha kwamba wanawake hao wanapata chakula cha kila siku kwa utaratibu, na waliona daraka hilo kuwa ‘kazi ya lazima’ kwa kutaniko.—Matendo 6:1-7.

Mtume Paulo alitumia kanuni ya “kusimama mbele ya mtu mwenye mvi” katika kutaniko la Kikristo. Alimwambia hivi kijana Timotheo ambaye alikuwa mwangalizi Mkristo: “Usimkemee kwa ukali mwanamume mzee. Badala yake, msihi kama baba, . . . wanawake wazee kama mama.” (1 Timotheo 5:1, 2) Ingawa kijana Timotheo alikuwa na mamlaka fulani juu ya Wakristo wenye umri mkubwa, aliambiwa asimdharau mwanamume mzee. Badala yake, alipaswa kumsihi kwa heshima kama baba. Na alipaswa kuwaheshimu wanawake wazee kutanikoni kwa njia iyo hiyo. Hivyo, mtume Paulo alikuwa akimshauri Timotheo, na washiriki wote wa kutaniko la Kikristo, “kusimama mbele ya mtu mwenye mvi.”

Bila shaka, watu wanaomwogopa Mungu hawahitaji sheria ili kuwaheshimu wazee. Fikiria mfano ambao unatajwa katika Biblia kumhusu Yosefu, ambaye alijitahidi juu chini kumleta baba yake mzee Misri, na hivyo kumwepusha Yakobo mwenye umri wa miaka 130 asife kutokana na njaa iliyokuwa imeenea. Yosefu alipomwona baba yake baada ya zaidi ya miaka 20, ‘alimwangukia shingoni mara moja, akalia shingoni pake tena na tena.’ (Mwanzo 46:29) Naam, miaka mingi kabla ya Waisraeli kuamuriwa wawatendee wazee kwa huruma na kuwaheshimu sana, Yosefu alionyesha maoni ya Mungu kwa kufanya hivyo.

Yesu mwenyewe aliwajali wazee katika huduma yake. Aliwashutumu vikali viongozi wa kidini ambao waliona ni sawa kuwapuuza wazazi wao wazee kwa sababu ya mapokeo ya kidini. (Mathayo 15:3-9) Yesu pia alimjali mama yake kwa upendo. Alipokuwa akipatwa na maumivu makali kwenye mti wa mateso, alihakikisha kwamba mama yake mzee angetunzwa na mtume wake mpendwa, Yohana.—Yohana 19:26, 27.

Mungu Hawaachi Kamwe Washikamanifu Wake

Mtunga-zaburi alisali hivi: “Usinitupe wakati wa uzee; wakati tu nguvu zangu zinapungua, usiniache.” (Zaburi 71:9) Mungu ‘hawatupi’ kamwe watumishi wake waaminifu hata wao wenyewe wanapohisi kwamba wamezeeka sana hivi kwamba hawawezi kutimiza lolote. Mtunga-zaburi hakuhisi kwamba ameachwa na Yehova; badala yake, alitambua kwamba anahitaji kumtegemea Mfanyi wake zaidi kadiri alivyoendelea kuzeeka. Yehova anapoona ushikamanifu huo, yeye humtegemeza mtu katika maisha yake yote. (Zaburi 18:25) Mara nyingi, mtu hutegemezwa na Wakristo wenzake.

Kutokana na yale ambayo yamezungumziwa, ni wazi kwamba wote wanaotaka kumheshimu Mungu wanapaswa pia kuwaheshimu wazee. Ndiyo, Muumba anawathamini sana wazee. Tukiwa viumbe waliofanywa kwa mfano wake, acheni sikuzote tuwe na maoni kama yake kuhusu “kichwa chenye mvi.”—Zaburi 71:18.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wakristo huwatendea wazee kwa heshima