Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wafungwa Walio Huru!

Wafungwa Walio Huru!

Wafungwa Walio Huru!

Na mwandishi wa Amkeni! nchini Mexico

VISIWA vya Islas Marías viko kilometa 90 kutoka pwani ya magharibi ya kati ya Mexico. * Tangu mwaka wa 1905, kisiwa kimoja kati ya hivyo, yaani Kisiwa cha María Madre, kimetumiwa na serikali ya Mexico kama kituo cha kuwaadhibia wafungwa. Wakati fulani, watu waliogopa sana adhabu ya kupelekwa kwenye kituo hicho, lakini sasa wafungwa wenye sifa nzuri wanaweza kuomba wapelekwe huko!

Sababu moja ni kwamba wafungwa fulani huruhusiwa kuishi na familia zao huko. Wafungwa hawawekwi katika jela zilizozuiwa kwa vyuma, bali wanaishi katika nyumba ndogo-ndogo. Kituo hicho kina huduma nyingi ambazo hupatikana katika miji mingi midogo. Wafungwa wanaweza kuwasiliana na watu wengine kwa simu, telegramu, televisheni, au barua. Watoto wanaweza kwenda shule ya msingi huko, ingawa inawabidi kwenda shule ya sekondari barani. Na ingawa si rahisi kuruhusiwa kufika huko, mara moja kwa juma meli moja ya kijeshi huleta bidhaa mbalimbali na wageni.

Tabia za wafungwa hurekebishwaje? Wafungwa hao hujiita colonos, yaani wenyeji, na wanapaswa kufanya kazi kwa saa kadhaa kila siku. Mbali na kuwasaidia kuzoea maisha baada ya kuachiliwa, jambo hilo pia husaidia kugharimia mahitaji yao. Wafungwa hao pia wako huru kufanya shughuli zao, kama vile kutunza bustani na kutengeneza vitu kwa mkono ili kupata pesa. Hiyo haimaanishi kwamba hawana vizuizi. Wafungwa wanapaswa kuwepo majina yao yanaposomwa kila asubuhi na hawapaswi kutoka nje ya nyumba zao baada ya saa tatu usiku.

Wafungwa Wawekwa Huru Kiroho

Wapata mwaka wa 1985, mfungwa mmoja ambaye alitoka katika familia ya Mashahidi wa Yehova, aliomba msaada wa kiroho. Alianza kufundishwa Biblia kwa barua. Baada ya muda, kikundi cha wanafunzi wa Biblia kilianzishwa na mikutano ya Kikristo ikaanza kufanywa. Baada ya kupata ruhusa kutoka kwa serikali, Mashahidi wa Yehova walianza kutembelea kisiwa hicho kwa ukawaida, huku wakisafiri usiku kwa saa 13 kutoka Mazatlán, kwenye nchi kavu. Katika miaka iliyofuata, wafungwa 40 hivi walijifunza kweli ya Neno la Mungu, wakabatizwa, na kufunguliwa baada ya kumaliza kifungo chao. Kufikia sasa, kuna Mashahidi 6 waliobatizwa wanaoishi kwenye kisiwa hicho, na watu 25 kwa wastani huhudhuria mikutano ya Kikristo.

Wenye mamlaka wanawaheshimu Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya jitihada zao, na wafungwa wanaokuwa Mashahidi huheshimiwa na watu wote. Hivi majuzi, msimamizi-msaidizi wa kituo hicho cha wafungwa alimwambia hivi Shahidi aliyetembelea huko: “Ni jambo zuri sana kwamba, kama sisi, nyinyi pia mnajali hali ya kimwili na ya kiadili ya wafungwa, mnawajali sana! Tunawaunga mkono kabisa.” Msimamizi huyo aliahidi kurekebisha jengo ambalo akina ndugu waliruhusiwa kutumia kwa ajili ya mikutano.

Shahidi mmoja aliyebatizwa, ambaye amefungwa kwa miaka kumi, alisema: “Akina ndugu wanaotutembelea wanapouliza ikiwa ninataka kuondoka, mimi huwaambia kwamba ninataka kuendelea kutumikia huku; ninaona kituo hiki kuwa eneo langu, kwani kuna uhitaji mkubwa. Lakini pia ningependa kuhudhuria makusanyiko na kufurahia ushirika wa Kikristo.” Shahidi huyo atafunguliwa mwaka ujao kwa sababu ya mwenendo wake mzuri.

Kituo cha wafungwa katika Islas Marías kimefanikiwa kuwarekebisha wafungwa kwa kadiri fulani. Hata hivyo, ujumbe wa Ufalme umeleta uhuru wa kiroho na marekebisho ya kweli, “kuachiliwa huru kwa mateka” na ‘kufunguliwa kabisa kwa macho ya walio wafungwa.’—Luka 4:18; Isaya 61:1.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kuna visiwa vinne katika eneo hilo, lakini vitatu havina watu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]

Kuacha Dawa za Kulevya na Kuwa Mzee Mkristo

Guillermo alifungwa kwa sababu ya kuuza na kutumia dawa za kulevya. Baada ya kupelekwa kwenye Kisiwa cha Islas Marías, aliendelea kutumia dawa za kulevya. Lakini alitambua kwamba baadhi ya wafungwa waliokuwa na vifungo virefu kwa sababu ya ulanguzi wa dawa za kulevya walikuwa safi, walikuwa na mtazamo mzuri, na walikuwa mfano kwa wafungwa wengine. Alipogundua kwamba wanajifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, alikubali mwaliko wa kuhudhuria mikutano. Baadaye, alianza kufundishwa Biblia kwa ukawaida.

Guillermo alifanya mabadiliko makubwa maishani mwake na kuachiliwa baada ya muda mfupi. Papo hapo aliwatafuta Mashahidi wa Yehova ili aendelee kujifunza. Leo, yeye ni mzee katika kutaniko la Kikristo, na sasa washiriki 17 wa familia yake ni Mashahidi wa Yehova. Anasema hivi: “Ni pendeleo kubwa kumjua Yehova na kuacha maovu hayo. Wengi kati ya marafiki zangu wa zamani sasa wamekufa kwa sababu ya kutumia dawa za kulevya. Dawa za kulevya zimeathiri ubongo wangu hivi kwamba ni vigumu kukumbuka mambo. Lakini njia ambayo Mashahidi walitumia kunifundisha iliboresha akili yangu sana. Madaktari walishangaa kwa kuwa walifikiri kwamba singepona. Mimi na familia yangu tumefaidika sana kutokana na kweli ya Biblia. Hatukuwa tukipendana, lakini sasa tuna umoja.”

[Ramani katika ukurasa wa 20]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Mazatlán

María Madre

Islas Marías

[Picha katika ukurasa wa 20]

Wafungwa na familia zao huhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme la María Madre