Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Faida za Kuwasomea Watoto

Faida za Kuwasomea Watoto

Faida za Kuwasomea Watoto

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI POLAND

Watayarishaji wa kampeni yenye kichwa “Poland Nzima Yawasomea Watoto,” ambayo hufanywa kila mwaka wanasema hivi: “Kusoma ni njia muhimu ya kupata ujuzi na kusitawisha uwezo wa kufikiri. . . . Kunamwezesha mtu atumie ufahamu na ujuzi.” Ikiwa hilo ni kweli, kwa nini watu wazima wengi na watoto huona kusoma kuwa wajibu usiopendeza?

Waanzilishi wa kampeni hiyo wanasema hivi: “Zoea la kusoma na kupendezwa na vitabu lazima lisitawishwe tangu utotoni.” Wanawaambia wazazi hivi: “Mkitaka watoto wenu wawe na hekima na wafanikiwe shuleni na maishani, wasomeeni kwa sauti kwa dakika 20 kila siku.”

Wazazi wanahimizwa pia wasiahirishe kuwasomea watoto wao, bali “waanze mapema iwezekanavyo.” Wanapaswa kuanza lini? Wazazi wanahimizwa hivi: “Acheni tumsomee mtoto mchanga tukiwa tumemkumbatia, tukimtazama kwa upendo, na kuamsha hamu yake kupitia sauti yetu. Kwa kufanya hivyo, daima watoto watavutiwa na kufurahia kusoma. Pia kusoma huchochea ukuzi wa akili zao.”

Wapangaji wa kampeni hiyo wanasisitiza kwamba “sasa kuwasomea watoto ni muhimu sana kuliko ilivyokuwa wakati mwingine wowote,” nao huonyesha faida nyingine za kufanya hivyo. Kusoma kwa sauti huwazoeza watoto kufikiri, “huwasaidia kuwaelewa wengine, kuuelewa ulimwengu, na kujielewa. . . . huwachochea kupendezwa na mambo, huwasaidia kuwa wabunifu, kusitawi kihisia, kuwa wenye huruma na fadhili, kujifunza maadili, . . . na kuwafanya wajiheshimu.” Bila shaka, kama vile wasimamizi wa kampeni hiyo wanavyosema, huo ni “ulinzi dhidi ya uvutano usiofaa . . . ambao huathiri akili na mioyo ya watoto.”

Ili watoto wanufaike zaidi tunapowasomea, ni muhimu kutumia vichapo ambavyo vitawachochea kumkaribia Muumba wao wa mbinguni. Biblia ndicho kitabu bora zaidi kinachoweza kutusaidia kumkaribia Mungu. Biblia husema kwamba kijana Timotheo alifundishwa “maandishi matakatifu” tangu “utoto mchanga.” (2 Timotheo 3:15) Wazazi wanaweza kuwasomea watoto wao vitabu vinavyotegemea Biblia, ambavyo vimeandikwa hasa kwa ajili ya watoto na kuchapishwa na Mashahidi wa Yehova kama vile, Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia na Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu.