Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilifundishwa Kumpenda Mungu Tangu Utotoni

Nilifundishwa Kumpenda Mungu Tangu Utotoni

Nilifundishwa Kumpenda Mungu Tangu Utotoni

SIMULIZI LA ANATOLY MELNIK

Watu wengi hupenda kuniita Babu. Mimi hufurahi sana kuitwa hivyo kwani hilo hunikumbusha babu yangu niliyempenda sana na aliyenisaidia sana. Hebu niwaeleze kumhusu na jinsi yeye na nyanya yangu walivyosaidia familia yao na watu wengine.

NILIZALIWA katika kijiji cha Hlina, kaskazini mwa Moldova. * Katika miaka ya 1920, wahudumu wanaosafiri, ambao waliitwa pilgrimu kutoka mpakani mwa Rumania, walitembelea eneo letu maridadi lenye milima-milima. Bila kusita, wazazi wa mama yangu walikubali habari njema ya Biblia. Mwaka wa 1927, wakawa Wanafunzi wa Biblia kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipoanza mnamo 1939, tayari kulikuwa na kutaniko la Mashahidi wa Yehova katika kijiji chetu kidogo.

Nilizaliwa mwaka wa 1936, na wakati huo kila mtu katika familia yetu alikuwa Shahidi wa Yehova isipokuwa baba yangu ambaye bado alikuwa wa Kanisa Othodoksi. Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipokuwa vikiendelea, baba yangu alianza kufikiria sana kusudi la uhai, na hatimaye akajiweka wakfu kwa Muumba wetu, Yehova Mungu, na kubatizwa. Babu yangu alitusaidia sana kufanya maendeleo ya kiroho. Aliipenda Biblia sana na angekariri maandiko mengi. Angebadilisha mazungumzo yoyote yahusu Biblia.

Mara nyingi Babu alinisimulia hadithi za Biblia nikiwa nimeketi pajani pake. Alinifundisha kumpenda Mungu. Ninamshukuru sana kwa kufanya hivyo! Nikiwa na umri wa miaka minane, nilienda kuhubiri kwa mara ya kwanza pamoja na Babu. Tulitumia Biblia kuwafundisha wanakijiji wenzetu kumhusu Yehova na jinsi ya kumkaribia.

Kunyanyaswa na Wakomunisti

Katika mwaka wa 1947, serikali ya Moldova ikichochewa na sera ya Kikomunisti na Kanisa Othodoksi, ilianza kuwanyanyasa Mashahidi wa Yehova. Polisi na baadhi ya maofisa wa siri wa shirika ambalo baadaye liliitwa KGB, walikuja nyumbani na kutuuliza kuhusu viongozi wa kazi yetu ya kuhubiri, mahali ambapo tulitoa vichapo, na mahali pa ibada. Walidai kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa “wanaharibu maendeleo ya Ukomunisti nchini humo,” na hivyo walitaka kukomesha kazi yao.

Wakati huo, baba yangu aliyekuwa amesoma sana alikuwa ameanza pia kupenda kweli za Biblia. Yeye na Babu walijua jinsi ya kuwajibu wapelelezi bila kuwasaliti Wakristo wenzetu. Walikuwa wajasiri, wenye upendo, na walihangaikia waamini wenzao. Mama vilevile alikuwa mtulivu wakati wote.

Baba alikamatwa mwaka wa 1948. Hatukuambiwa mashtaka yake. Alihukumiwa miaka saba katika gereza lenye ulinzi mkali kisha miaka miwili uhamishoni. Hatimaye, alipelekwa Magadan, eneo lililo kaskazini-mashariki mwa Urusi, umbali wa kilometa 7,000 kutoka nyumbani. Hatukuonana naye kwa miaka tisa. Ilikuwa vigumu kuishi bila baba, lakini Babu alinisaidia sana.

Twapelekwa Uhamishoni

Mnamo usiku wa Juni 6, 1949, askari wawili na ofisa mmoja walituvamia. Walituamuru tuondoke na kuingia ndani ya gari lao kabla ya saa mbili kwisha. Hatukupewa habari zaidi. Walituambia tu kwamba tunapelekwa uhamishoni na hatutarudi kamwe. Basi, sisi sote, yaani, mimi, Mama, Babu, Nyanya, pamoja na waamini wenzetu, tukapelekwa Siberia. Nilikuwa na umri wa miaka 13 tu. Baada ya majuma machache, tulifika katika eneo lenye majimaji katikati ya msitu mkubwa. Eneo hilo lilitofautiana na mazingira ya nyumbani niliyoyapenda sana! Wakati mwingine tulilia. Hata hivyo, tulikuwa na uhakika kwamba Yehova hatatuacha kamwe.

Tulipelekwa katika kijiji kilichokuwa na nyumba kumi ndogo za mbao. Mashahidi wengine walipelekwa katika vijiji tofauti msituni. Wenyeji waliambiwa kwamba Mashahidi hula watu ili watuogope na kutubagua. Hata hivyo, muda si muda, watu waligundua kwamba huo ni uwongo na hivyo hawakupaswa kutuogopa.

Kwa miezi miwili, tuliishi katika nyumba ndogo nzee. Lakini tulihitaji kujenga nyumba bora kabla ya majira ya baridi kali. Babu na Nyanya walitusaidia mimi na Mama kujenga nyumba duni iliyokuwa nusu juu ya ardhi na nusu chini ya ardhi. Tuliishi humo kwa zaidi ya miaka mitatu. Hatukuruhusiwa kuondoka kijijini kamwe.

Baadaye niliruhusiwa kwenda shule. Kwa kuwa imani yangu ilitofautiana na ya walimu na wanafunzi wenzangu, mara nyingi waliniuliza maswali. Niliporudi nyumbani na kumwambia Babu kwamba niliwahubiria, alifurahi sana.

Uhuru Zaidi

Maisha yetu yalikuwa afadhali kidogo baada ya mtawala wa kimabavu, Stalin, kufa mwaka wa 1953. Tulikuwa na uhuru wa kuondoka kijijini. Hilo lilituwezesha kukutana na waamini wenzetu na kuhudhuria mikutano katika vijiji vingine vilivyokuwa na Mashahidi. Tulikutana katika vikundi vidogo-vidogo ili kuepuka kutambuliwa. Ili kufika huko tulitembea umbali wa kilometa 30, wakati mwingine katika theluji iliyofika kwenye magoti kukiwa na baridi kali. Siku iliyofuata, tungetembea kwa muda mrefu kurudi nyumbani. Tukiwa njiani, tulikula matango na peremende. Hata hivyo, tulifurahi sana sawa na alivyofurahi Daudi!—Zaburi 122:1.

Katika mwaka wa 1955 nilijiweka wakfu na kubatizwa. Muda mfupi kabla ya hapo, kwenye mkutano katika kijiji jirani, nilikuwa nimekutana na Lidiya, msichana mpole mwenye nywele nyeusi. Yeye na familia yao walikuwa wamehamishwa kutoka Moldova. Alikuwa na sauti nyororo na alijua akilini karibu nyimbo zote 337 katika kitabu cha nyimbo tulichotumia wakati huo. Nilipendezwa na jambo hilo kwani mimi pia nilipenda nyimbo zetu. Tukaamua kufunga ndoa mwaka wa 1956.

Kwa kuwa tulijua kwamba Baba alikuwa amepelekwa Magadan, tuliahirisha ndoa yetu na hivyo nikamwandikia barua ili tupate kibali chake. Muda mfupi baadaye, Baba aliachiliwa na akajiunga nasi uhamishoni. Alitusimulia jinsi Mungu alivyomsaidia yeye na Wakristo wenzake kukabili hali mbaya gerezani. Masimulizi hayo yaliimarisha imani yetu.

Muda mfupi baada ya Baba kurudi, kulitokea msiba mbaya sana Mama alipokuwa akitayarisha mafuta tuliyotumia kuchanganya rangi na vanishi. Sufuria kubwa aliyotumia kuchemsha mafuta iliteleza na mafuta yakammwagikia. Alifia hospitalini. Tulihuzunika sana. Baadaye, huzuni ya Baba ilipopungua, alimwoa Tatyana, Shahidi kutoka kijiji jirani.

Kupanua Utumishi Wetu

Katika mwaka wa 1958, mimi na Lidiya tulihamia kijiji kikubwa cha Lebyaie, kilometa 100 kutoka Kizak, kijiji tulichokuwa tukiishi. Tulikuwa tumesoma kwamba Wakristo wengine katika nchi nyingine walihubiri nyumba kwa nyumba. Hivyo tukajaribu kufanya hivyo katika eneo letu jipya. Ingawa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yalikuwa yamepigwa marufuku, tuliyapata kisiri kutoka sehemu nyingine. Sasa tulijulishwa kwamba tungepata magazeti katika lugha ya Kirusi tu. Kufikia wakati huo, tulipokea magazeti katika lugha ya Moldavia pia. Hivyo, tulijitahidi sana kujifunza Kirusi. Mpaka leo ninakumbuka vichwa na mambo yaliyozungumziwa katika makala mbalimbali.

Tulifanya kazi ili kujiruzuku. Lidiya alifanya kazi katika ghala ya nafaka nami nikafanya kazi ya kushusha mbao kutoka kwa magari. Ilikuwa kazi yenye kuchosha, na mshahara kidogo. Ingawa Mashahidi walionwa kuwa wafanyakazi wenye bidii, hatukupata msaada wa kifedha tulipouhitaji wala hatukupewa marupurupu. Wasimamizi walisema hivi waziwazi: “Mashahidi wa Yehova si sehemu ya jumuiya ya Kikomunisti.” Hata hivyo, tulifurahi kwamba maneno haya ya Yesu kuhusu wafuasi wake yalitimizwa kwetu: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.”—Yohana 17:16.

Kukabili Magumu Mapya

Binti yetu Valentina alizaliwa mwaka wa 1959. Muda mfupi baadaye, mnyanyaso ulianza tena. Kitabu The Encyclopædia Britannica, kinasema: “Mwaka wa 1959-1964, Waziri Mkuu, Nikita Khrushchev, alianzisha kampeni mpya ya kupinga dini.” Maofisa wa KGB walituambia kwamba lengo la serikali ya Sovieti ni kukomesha dini zote, hasa Mashahidi wa Yehova.

Valentina alipokuwa na umri wa mwaka mmoja hivi, niliamuriwa nijiunge na jeshi. Nilipokataa, nilihukumiwa kifungo cha miaka mitano kwa sababu ya kutounga mkono upande wowote. Pindi moja Lidiya aliponitembelea, ofisa mmoja wa KGB alimwambia hivi: “Tumejulishwa na serikali ya Urusi kwamba kabla ya miaka miwili kwisha, hakuna Shahidi wa Yehova atakuwa katika Muungano wa Sovieti.” Kisha akaonya hivi: “Ni lazima uikane imani yako, au sivyo utatiwa gerezani.” Ofisa huyo alifikiri kwamba akitumia vitisho kama hivyo, atawanyamazisha wanawake, huku akidai: “Wao ni kikundi dhaifu.”

Baada ya muda, ndugu wengi walikuwa gerezani na katika kambi za kazi ngumu. Hata hivyo, akina dada wenye ujasiri waliendelea kuhubiri. Pia, walihatarisha maisha yao ili kuwapelekea vichapo wale waliokuwa gerezani na katika kambi za kazi ngumu. Lidiya alikabili majaribu kama hayo na mara nyingi alitongozwa na wanaume waliojua kwamba sikuwapo. Isitoshe, aliambiwa kwamba sitaachiliwa kamwe. Hata hivyo niliachiliwa!

Naachiliwa na Kuhamia Kazakhstan

Kesi yangu ilisikilizwa tena mwaka wa 1963, kisha nikaachiliwa baada ya kukaa gerezani kwa miaka mitatu. Lakini hatukupata kibali cha kuishi popote, na hivyo sikuweza kupata kazi. Serikali iliamuru hivi: “Ikiwa huna kibali cha kuishi nchini, huruhusiwi kufanya kazi.” Tulimwomba Yehova msaada kwa bidii. Kisha tukaamua kuhamia jiji la Petropavl, lililo kaskazini mwa Kazakhstan. Hata hivyo, wenye mamlaka katika jiji hilo walikuwa tayari wamepata habari kutuhusu na hivyo hawakuturuhusu kuishi wala kufanya kazi huko. Mashahidi 50 hivi katika jiji hilo walikabili mnyanyaso huohuo.

Tukiwa pamoja na wenzi wawili wa ndoa, tulihamia mji mdogo wa Shchuchinsk, ulioko upande wa kusini. Hakukuwa na Shahidi yeyote huko wala wenye mamlaka hawakujua chochote kuhusu kazi yetu ya kuhubiri. Kwa juma moja, mimi na Ivan tuliwaacha wake zetu katika kituo cha gari moshi, mahali ambapo tulilala, na kwenda kutafuta kazi. Hatimaye tulipata kazi katika kiwanda cha glasi. Tulipangisha chumba kidogo kilichotoshea vitanda viwili na vitu vichache tu, hata hivyo tuliridhika.

Waajiri wetu walifurahi sana kwa sababu mimi na Ivan tulifanya kazi kwa bidii. Nilipoitwa nijiunge na jeshi kwa mara nyingine, tayari meneja wa kiwanda alikuwa amejua kwamba kwa sababu ya dhamiri yangu inayoongozwa na Biblia, siwezi kujiunga na jeshi. Inafurahisha kwamba aliwasiliana na mkuu wa jeshi na kumwambia kwamba mimi na Ivan ni wafanyakazi stadi na hivyo tukiondoka, kiwanda hakitaendelea kufanya kazi. Basi tukaruhusiwa kubaki.

Kulea Watoto na Kuwatumikia Wengine

Binti yetu wa pili, Lilya, alizaliwa mwaka wa 1966. Mwaka mmoja baadaye tulihamia mji wa Belyye Vody, kusini mwa Kazakhstan karibu na mpaka wa Uzbekistan, ambapo kulikuwa na kikundi kidogo cha Mashahidi. Punde si punde, kutaniko likaanzishwa na nikawekwa kutumikia nikiwa mwangalizi-msimamizi. Mnamo 1969, tulipata mwana anayeitwa Oleg, na miaka miwili baadaye, Natasha, ambaye ndiye kitinda mimba. Mimi na Lidiya hatukusahau kamwe kwamba watoto ni urithi kutoka kwa Yehova. (Zaburi 127:3) Tulijadiliana kuhusu jinsi ya kuwalea ili wampende Yehova.

Hata katika miaka ya 1970, ndugu wengi walikuwa bado katika kambi za kazi ngumu. Makutaniko mengi yalihitaji Wakristo wakomavu ili wasimamie mambo na kutoa mwongozo. Hivyo, Lidiya alitimiza mengi katika kuwalea watoto wetu, nyakati nyingine akitimiza wajibu wake na wangu, huku nikitumikia nikiwa mwangalizi anayesafiri. Nilitembelea makutaniko huko Kazakhstan, na pia katika jamhuri za Sovieti za Turkmenistan, Tajikistan, na Uzbekistan. Wakati huohuo, nilifanya kazi ili kuruzuku familia, na Lidiya na watoto waliniunga mkono.

Ingawa mara nyingine sikurudi nyumbani kwa majuma kadhaa, nilijitahidi kuwapenda watoto wangu na kuwasaidia kukua kiroho. Mimi na Lidiya tulimwomba Yehova kwa bidii awasaidie watoto wetu, nasi tukazungumza nao kuhusu kushinda tatizo la kuwaogopa wanadamu na kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Kama mke wangu hangenisaidia, singeweza kutimiza mgawo wangu nikiwa mwangalizi anayesafiri. Lidiya na dada wengine hawakuwa “kikundi dhaifu” kama vile yule ofisa wa jeshi alivyokuwa amedai. Walikuwa wenye nguvu sana kiroho!—Wafilipi 4:13.

Katika mwaka wa 1988, baada ya watoto wetu wote kukua, niliwekwa rasmi kuwa mwangalizi anayesafiri wa wakati wote. Mzunguko wangu ulitia ndani nchi nyingi za Asia ya Kati. Baada ya kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova katika ule uliokuwa Muungano wa Sovieti kusajiliwa mwaka wa 1991, ndugu wakomavu kiroho walianza kutumikia jamhuri za Asia zilizokuwa sehemu ya muungano huo. Sasa kuna waangalizi wanaosafiri 14 katika nchi hizo tano zilizotajwa, na mwaka uliopita zaidi ya watu 50,000 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo!

Mwaliko Usiotazamiwa

Mapema mwaka wa 1998 nilipigiwa simu ambayo sikutazamia kutoka kwa ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Urusi. Niliulizwa hivi: “Anatoly, je, wewe na Lidiya mmewahi kufikiria kuingia katika utumishi wa wakati wote?” Bila shaka, tulikuwa tumefikiria kwamba pendeleo hilo linawafaa watoto wetu. Hata mwana wetu Oleg tayari alikuwa ametumikia kwa miaka mitano hivi katika ofisi ya tawi ya Urusi.

Nilipomwambia Lidiya kuhusu jambo hilo, aliniuliza hivi: “Lakini vipi kuhusu nyumba yetu, shamba letu, na vitu vyetu?” Baada ya kusali na kujadiliana, tuliamua kuukubali mgawo huo. Hatimaye tulialikwa kutumikia katika kituo cha kidini cha Mashahidi wa Yehova huko Issyk, Kazakhstan, karibu na jiji kubwa la Alma-Ata. Kazi ya kutafsiri vichapo vyetu vinavyotegemea Biblia katika lugha za eneo hili hufanywa katika kituo hiki.

Familia Yetu Leo

Tunamshukuru Mungu sana kwa kutusaidia kuwafundisha watoto wetu kweli za Biblia! Binti yetu mkubwa Valentina aliolewa, naye na mume wake wakahamia Ingelheim, Ujerumani, mwaka wa 1993. Wana watoto watatu ambao ni Mashahidi wa Yehova waliobatizwa.

Binti yetu wa pili, Lilya, ana familia pia. Yeye pamoja na mume wake ambaye ni mzee wa kutaniko la Belyye Vody, wanawasaidia watoto wao wawili kumpenda Mungu. Oleg alimwoa Natasha, dada kutoka Moscow, nao wanatumikia katika ofisi ya tawi iliyo karibu na St. Petersburg, nchini Urusi. Katika mwaka wa 1995, binti yetu mdogo Natasha aliolewa, naye pamoja na mume wake wanatumikia kutaniko la Kirusi, nchini Ujerumani.

Mara kwa mara familia yetu hupanga kuwa pamoja. Watoto wetu huwaeleza watoto wao jinsi “Mama” na “Baba” walivyomtii Yehova na kuwasaidia watoto wao kumpenda na kumtumikia Mungu wa kweli, Yehova. Mazungumzo hayo huwasaidia wajukuu wetu kukua kiroho. Mjukuu wetu mdogo, anafanana sana na mimi nilipokuwa na umri kama wake. Nyakati nyingine yeye huketi pajani pangu na kuniomba nimsimulie hadithi ya Biblia. Mimi hutokwa na machozi ninapokumbuka jinsi nilivyoketi pajani pa Babu na jinsi alivyonisaidia kumpenda na kumtumikia Muumba wetu Mtukufu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Katika makala hii tutatumia Moldova ambalo ndilo jina la kisasa la nchi hiyo, badala ya majina yake ya zamani, yaani, Moldavia au Jamhuri ya Sovieti ya Moldavia.

[Picha katika ukurasa wa 11]

Nikiwa na wazazi wangu nje ya nyumba yetu huko Moldova muda mfupi kabla ya Baba kufungwa

[Picha katika ukurasa wa 12]

Nikiwa na Lidiya, uhamishoni, mwaka wa 1959

[Picha katika ukurasa wa 13]

Lidiya akiwa na binti yetu Valentina nilipokuwa gerezani

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nikiwa na Lidiya leo

[Picha katika ukurasa wa 15]

Tukiwa na watoto na wajukuu wetu; sote tunamtumikia Yehova!