Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Umuhimu wa Kumfundisha Mtoto Wako

Umuhimu wa Kumfundisha Mtoto Wako

Umuhimu wa Kumfundisha Mtoto Wako

UWEZO wa mtu hutegemea mambo ambayo anajifunza au anakosa kujifunza akiwa mchanga. Hivyo, watoto wanaweza kusaidiwaje na wazazi wao ili wafanikiwe na kuwa watu wazima wenye usawaziko? Fikiria kauli za watu fulani zinazotegemea uchunguzi wa hivi karibuni.

Jinsi Ubongo Unavyohusika

Maendeleo katika mbinu za kuchunguza ubongo yamewasaidia sana wanasayansi wanaochunguza ukuzi wa ubongo. Uchunguzi mbalimbali kama huo umeonyesha kwamba miaka ya mapema ya utoto ni muhimu sana ili kusitawisha uwezo wa ubongo unaohitajiwa kuelewa habari, kuonyesha hisia kwa njia ya kawaida, na kufahamu lugha vizuri. Gazeti Nation linaripoti hivi: “Njia za kupitisha habari kwenye ubongo hufanyizwa haraka sana katika miaka ya mapema ya mtoto, wakati ubongo unapoendelea kusitawishwa na mambo yaliyorithiwa na hali zinazompata mtoto.”

Wanasayansi wanaamini kwamba njia za kupitisha habari katika ubongo husitawi sana katika miaka ya mapema. Dakt. T. Berry Brazelton, ambaye ni mtaalamu wa masuala ya ukuzi wa watoto, anasema kwamba wakati huo ndipo “uwezo wa mtoto wa kuwa mwerevu, kujitambua, kuwatumaini wengine, na kuchochewa kujifunza, unapositawishwa.”

Ukubwa, muundo, na uwezo wa ubongo wa mtoto hukua haraka sana katika miaka yake ya mapema. Mtoto anapochochewa sana na kujifunza mambo mengi, njia za kupitisha habari katika ubongo huongezeka. Hilo humwezesha kufikiri, kujifunza, na kuelewa mambo.

Inawezekana kwamba kadiri ubongo wa mtoto unavyochochewa, ndivyo chembe nyingi zaidi za neva zinavyoanza kufanya kazi na kuunganishwa. Ubongo wa mtoto hauchochewi tu kupitia kufundishwa mambo, nambari, au lugha. Wanasayansi wamegundua kwamba ubongo wa mtoto unahitaji kuchochewa pia kihisia. Utafiti unaonyesha kwamba ubongo wa watoto wachanga ambao hawakumbatiwi, hawaguswi, hawachezi na wengine, wala kuchochewa kihisia hauwezi kusitawi sana.

Je, Uwezo wa Mtoto Hutegemea Kufundishwa?

Hatimaye, mtoto anapoendelea kukua, inaonekana mwili huacha kutumia njia za kupitisha habari ubongoni ambazo hazihitajiki. Hilo linaweza kuathiri sana uwezo wa mtoto. Mtafiti wa ubongo, Max Cynader, anasema hivi: “Ubongo wa mtoto usipochochewa vizuri wakati unaofaa, uwezo wake hautasitawi vizuri.” Kulingana na Dakt. J. Fraser Mustard, hilo linaweza kumfanya mtoto asiwe mwerevu, ashindwe kuwasiliana vizuri na kufanya hesabu, awe na matatizo ya afya anapokuwa mtu mzima, na pia matatizo ya kitabia.

Basi, inaonekana kwamba maisha ya mtu mzima hutegemea sana mambo yanayompata akiwa mchanga. Mambo hayo huamua ikiwa mtu ataweza kukabiliana na hali mbalimbali au kuwa dhaifu, ikiwa ataweza au hataweza kuelewa mambo magumu, na ikiwa atakuwa au hatakuwa mwenye huruma. Hivyo, wazazi hutimiza sehemu muhimu. Daktari mmoja wa watoto anasema hivi: “Mojawapo ya mambo muhimu zaidi ambayo mtoto anahitaji ni mzazi anayejali na anayetimiza madaraka yake.”

Huenda hilo likaonekana kuwa jambo rahisi. Ukiwafundisha na kuwatunza watoto wako, watafanikiwa. Hata hivyo, wazazi wanafahamu kwamba mara nyingi si rahisi kujua jinsi ya kuwatunza watoto wao vizuri. Kwa kawaida, kuwa mzazi mwenye matokeo si jambo linalotokea lenyewe tu.

Kulingana na uchunguzi mmoja, asilimia 25 ya wazazi waliochunguzwa hawakujua kwamba wanaweza kuboresha au kuathiri uwezo wa akili, uhakika, na tamaa ya kujifunza ya watoto wao. Hilo linazusha maswali haya: Ni ipi iliyo njia bora zaidi ya kukuza uwezo wa mtoto wako? Na unaweza kufanya nini ili iwe rahisi kwa mtoto wako kusitawisha uwezo wake? Hebu tuone.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Ubongo wa watoto wachanga usipochochewa hautasitawi vizuri