Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kunenepa Kupita Kiasi ni Tatizo?

Je, Kunenepa Kupita Kiasi ni Tatizo?

Je, Kunenepa Kupita Kiasi ni Tatizo?

“Idadi ya vijana ambao wamenenepa kupita kiasi inaongezeka.”—S. K. Wangnoo, mtaalamu katika Hospitali ya Indraprastha Apollo, huko Delhi, India.

KAMA maelezo yaliyo juu yanavyoonyesha, maisha ya familia nyingi za kawaida nchini India yamebadilika na kuwafanya vijana waliobalehe wanenepe kupita kiasi. Tatizo hilo linazidi kuenea katika nchi nyingi kwa sababu watu wanaacha kufanya mazoezi na kuzoea kula vyakula ambavyo haviboreshi afya. Mtaalamu mmoja wa tiba ya vijana waliobalehe alisema hivi: “Kizazi kitakachofuata [nchini Uingereza] kitakuwa . . . na watu wanene zaidi katika historia ya wanadamu.” Gazeti Guardian Weekly liliripoti hivi: “Hapo zamani, ni watu wazima tu walionenepa kupita kiasi. Kwa sababu ya mazoea mabaya ya kula na kutofanya mazoezi, sasa vijana wa Uingereza wanapata matatizo ambayo yalianzia Marekani. Wakinenepa kupita kiasi kwa muda mrefu wanaweza kupata magonjwa kama vile kisukari, ugonjwa wa moyo, na kansa.”

Waandishi wa kitabu Food Fight wanasema hivi: “Sasa, tatizo kubwa zaidi la lishe ulimwenguni si kukosa chakula kinachofaa, bali ni kula na kunywa kupita kiasi.” Don Peck, aliandika hivi katika jarida The Atlantic Monthly: “Sasa, Wamarekani milioni tisa hivi wanakabili hatari ya kupata magonjwa kwa sababu ya kunenepa kupita kiasi, na hiyo inamaanisha kwamba wanazidi uzito wa kawaida kwa kilo 45 au zaidi.” Kila mwaka, watu wapatao 300,000 nchini humo hufa mapema kutokana na magonjwa yanayohusiana na kunenepa kupita kiasi. Hicho ndicho “kisababishi cha pili kikuu cha vifo baada ya uvutaji wa sigara.” Peck anasema hivi: “Huenda karibuni kunenepa kupita kiasi kutakuwa tatizo kubwa zaidi la afya ulimwenguni kuliko njaa na magonjwa ya kuambukiza.” Basi, hatuna budi kuzingatia tatizo la kunenepa kupita kiasi. Katika kitabu Eat, Drink, and Be Healthy, Dakt. Walter C. Willett anaandika hivi: “Zaidi ya uvutaji wa sigara, uzito wako ndilo jambo kuu zaidi linaloonyesha jinsi afya yako itakavyokuwa wakati ujao.” Tunakazia maneno haya: afya ya wakati ujao.

Kunenepa Kupita Kiasi

Mtu huonwa kuwa amenenepa kupita kiasi wakati gani? Kliniki ya Mayo huko Rochester, Minnesota, Marekani, inasema hivi: “Kwa ufupi, kunenepa kupita kiasi ni kuwa mzito sana kwa sababu ya mafuta mengi mwilini.” Lakini utajuaje uzito unaomfaa kila mtu? Chati zinazoonyesha uzito unaowafaa watu wa kimo fulani zinaweza kutumiwa kukadiria iwapo mtu ni mnene tu au ni mnene kupita kiasi. (Ona chati kwenye ukurasa wa 5.) Hata hivyo, chati hizo hazionyeshi uzito unaowafaa watu wenye hali mbalimbali za mwili. Kliniki ya Mayo inasema hivi: “Afya ya mtu hujulikana vizuri inapopimwa kwa kutegemea kiasi cha mafuta yaliyo mwilini mwake wala si kwa kutegemea uzito wake.” Kwa mfano, mwanariadha anaweza kuwa mzito kwa sababu ya kuwa na misuli au mifupa mikubwa. Ni mambo gani yanayowafanya watu wanenepe kupita kiasi? Makala inayofuata itazungumzia swali hilo.