Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kupambana na Mfadhaiko Baada ya Shambulizi la Magaidi

Kupambana na Mfadhaiko Baada ya Shambulizi la Magaidi

Kupambana na Mfadhaiko Baada ya Shambulizi la Magaidi

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI HISPANIA

MNAMO Machi 11, 2004, jiji la Madrid, nchini Hispania, lilitikiswa na milipuko ya mabomu kumi katika vituo vitatu vya gari-moshi. Magari-moshi manne yalishambuliwa kwa wakati mmoja na watu 190 hivi walikufa na 1,800 wakajeruhiwa.

Kwa kuwa mabomu hayo yalilipuka asubuhi wakati watu wengi walipokuwa wakielekea kazini, magari-moshi yote yalikuwa yamejaa, na uharibifu ulikuwa mbaya sana. Aroa, aliyejionea tukio hilo, anasema hivi: “Mlipuko ulikuwa wenye nguvu hivi kwamba behewa moja lilirushwa meta moja hewani. Niliposhuka katika behewa nilimokuwa, sehemu hiyo yote ilikuwa kama eneo la vita. Inatisha sana kuona mauaji makubwa kama hayo.” Mabehewa kumi katika magari-moshi manne yalishambuliwa kwa njia hiyohiyo yenye kutisha. Magaidi walikuwa wameacha mifuko ya kubebea mgongoni iliyojaa vilipukaji kwenye magari-moshi, kisha wakavilipua kwa kutumia simu za mkononi.

Baadhi ya abiria hawakukumbuka matukio hayo ya kuogofya ambayo yaliwapata. Lakini mamia kati ya abiria, kama vile Aroa, wanalazimika kupambana na majeraha ya kimwili na mfadhaiko wenye kudumu. Aroa anasema: “Mlipuko uliathiri sana uwezo wangu wa kusikia, lakini ninaathiriwa hata zaidi na mambo ya kuogofya niliyoyaona.”

Aroa anaongeza hivi: “Ninashukuru kwamba Mashahidi wenzangu walinitia moyo sana. Ujumbe na simu nilizopata kutoka sehemu zote za dunia zilinikumbusha kwamba sisi ni undugu wa ulimwenguni pote. Isitoshe, Biblia inatusaidia kuelewa ni kwa nini watu ni wakatili hivyo. Niliwaeleza baadhi ya wafanyakazi wenzangu kwamba Maandiko yanasema kwamba katika ‘siku za mwisho,’ watu wangekuwa wakali na bila upendo wa asili. Pia nimetambua kwamba utumishi wangu wa wakati wote umenisaidia sana kupunguza mfadhaiko.”—2 Timotheo 3:1-3.

Pedro ni mmoja wa abiria waliopata majeraha mabaya. Alikuwa amesimama umbali wa meta nne hivi kutoka mahali ambapo bomu lililipuka behewani. Mlipuko huo ulimwangusha chini, naye alijeruhiwa kichwani na kupata matatizo ya kupumua. Baada ya kulazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi kwa siku tano, alianza kupata nafuu. Mashahidi wengi walimtembelea na kumtia moyo, na jambo hilo likawashangaza wauguzi. Muuguzi mmoja alisema hivi: “Kwa miaka 26 sijawahi kumwona yeyote akitembelewa na watu wengi hivyo na kupokea zawadi nyingi sana!” Kwa upande mwingine, Pedro, aliwasifu sana wafanyakazi wa hospitali. Alisema: “Wao ni wazuri sana, na walinisaidia kupona haraka.”

Wengi walioathiriwa walikuwa wamehamia Hispania hivi majuzi. Manuel, kutoka Kuba, alijeruhiwa na mlipuko wa kwanza uliotokea kwenye kituo cha Atocha, kisha mlipuko wa pili ukamfanya apoteze fahamu. Alieleza hivi: “Kwa kuwa nilikuwa nimeanguka, watu walinikanyaga walipokuwa wakikimbia kwa woga. Nilipopata fahamu, niligundua kwamba nilikuwa nimevunjika mbavu mbili, nimejeruhiwa mguu, na vilevile kupoteza uwezo wa kusikia katika sikio moja.”

Manuel aliongeza hivi: “Polisi, magari ya kuwabebea wagonjwa, na wazima-moto, walifika bila kukawia, nao walitusaidia sana. Walifanya kazi yao kwa haraka na kwa ustadi, na hivyo walisaidia kupunguza wasiwasi. Walinitendea kwa fadhili na huruma na pia wakahakikisha kwamba ninapata matibabu.”

Mshtuko Unaosababishwa na Tukio Lenye Kutisha

Kama vile Aroa, Manuel pia ameathiriwa sana kihisia. Anasema: “Nilishtuka sana nilipopanda gari-moshi hivi majuzi. Ilinibidi kushuka mara moja. Na bado mimi humshuku abiria yeyote anayebeba mfuko mgongoni au kitu kama hicho. Lakini nimepata msaada mkubwa kuliko wengine, hata ingawa hakuna yeyote wa familia yetu anayeishi Hispania. Mamia ya Mashahidi walinipigia simu, na familia moja ilinialika kukaa nao kwa siku chache ili nisihisi upweke. Msaada huo mkubwa wa ndugu kutoka sehemu zote za dunia ulinisaidia kutulia.”

Sergio, abiria ambaye hakupata jeraha lolote, bado huteseka kila siku anapokumbuka mambo aliyoona. Bomu moja lililipuka kwenye behewa lililokuwa mbele yake na lingine katika behewa lililokuwa nyuma yake. Kama vile Manuel, yeye anashukuru kwa msaada ambao familia yake na Mashahidi wenzake walimpa. Alisema hivi: “Walionyesha kwamba wananipenda na walinikumbusha kwamba nina ndugu wengi wenye umoja wanaowajali wenzao. Walinitia moyo kila siku, na kwa kuwa wengi walinipigia simu niliweza kueleza jinsi nilivyohisi, jambo ambalo kwa kawaida si rahisi kwangu.”

Abiria wengine wa magari hayo ya moshi waliathiriwa kwa njia tofauti. Diego hakujua kwamba aliketi karibu na mojawapo ya mabomu manne ambayo hayakulipuka. Aliweza kutoka katika gari-moshi bila kujeruhiwa. Anasema: “Sasa ninajilaumu kwa kuwa sikuwasaidia wale waliojeruhiwa. Nilikimbia kwa woga pamoja na watu wengine waliotoka haraka kwenye kituo hicho.”

Mlipuko kwenye gari-moshi alimokuwa Ramón, kijana kutoka Brazili, ulimshtua sana hivi kwamba hakuweza kufanya chochote. Hata hivyo, siku mbili baada ya shambulizi hilo, aliamua kuwahubiria wengine kuhusu Ufalme. Alikutana na mwanamume Mreno aliyemwambia Ramón kwamba anatafuta dini ya kweli. Ramón alianza kumfundisha Biblia, na mara moja akaanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Ramón alisema: “Unasikia vizuri unapoweza kuwasaidia wengine kiroho.”

Bila shaka itachukua muda kwa wote walioathiriwa kupona majeraha ya kimwili na mfadhaiko. Inahuzunisha kwamba tunaishi wakati ambapo jeuri isiyo na sababu inaweza kutokea mahali popote. Ingawa mtazamo mzuri wa kiroho unaweza kuwasaidia walioathiriwa kupambana na mfadhaiko, ni Ufalme wa Mungu tu ambao hatimaye utakomesha misiba yote.—Ufunuo 21:3, 4.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 15]

NGUVU ZA KIROHO ZA KUPAMBANA NA MFADHAIKO

Manuel Suárez

“Nilipokuwa bado nimeshtuka nikingoja kupelekwa hospitalini, nilikuwa nikikumbuka maneno haya ya Methali 18:10: ‘Jina la Yehova ni mnara wenye nguvu. Mwadilifu hukimbilia humo na kupewa ulinzi.’ Maneno hayo yalinitia nguvu.”

Aroa San Juan

“Unapopatwa na jambo kama hilo, inakuwa wazi hata zaidi kwamba hizi ni siku za mwisho na ni lazima kukazia fikira mambo ya kiroho. Utumishi wa wakati wote unanisaidia kupona pole kwa pole.”

Fermín Jesús Mozas

“Licha ya kupata majeraha kichwani, niliweza kuwasaidia na kuwafariji baadhi ya abiria wenzangu waliojeruhiwa. Ninafikiri sikuvurugika kwa sababu ya tumaini la ufufuo ambalo Mungu ametupa. Tumaini hilo hutuimarisha tunapopatwa na misiba kama hiyo.”

Pedro Carrasquilla

“Nilipokuwa nimelazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi nikiwa na maumivu makali kifuani, andiko la 1 Timotheo 6:19 lilikuja akilini mwangu tena na tena. Andiko hilo linatutia moyo tujiwekee msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao, ili tushike imara uzima ulio wa kweli. Mstari huu ulinikumbusha tumaini la Paradiso, ambayo Mungu amewaahidi wanaompenda. Paradiso hiyo ndiyo tunayojitahidi sana kufikia.”

[Picha katika ukurasa wa 13]

Juu: Waokoaji wanawahudumia watu waliojeruhiwa na walio mahututi kwenye reli nje ya kituo cha Atocha

[Hisani]

Top: CORDON PRESS

[Picha katika ukurasa wa 13]

Upande wa kulia: Ukumbusho wa muda