Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Deni la Usingizi Asanteni sana kwa ule mfululizo wenye kichwa “Je, Una Deni la Usingizi?” (Februari 8, 2004) Kwa mara nyingine tena, wasomaji wa Amkeni! walipokea habari nyingi zinazoelimisha na kufariji. Nimeugua ugonjwa wa kuziba koo ninapolala kwa miaka miwili na nusu hivi. Tangu mwanzoni, nilijua kwamba nina tatizo fulani, lakini sikulifahamu. Baada ya kufanyiwa uchunguzi, nilifahamu jinsi kukosa usingizi kunavyoweza kumwathiri mtu. Gazeti hilo litaniwezesha kuwaeleza rafiki zangu kuhusu hali yangu.

W. M., Marekani

Ninatumia kompyuta kufanya kazi na kwa sababu ya ratiba ya kazi yangu, mimi hulala saa tofauti-tofauti kila siku. Muda fulani uliopita, nililala kwa muda mfupi sana kwa siku kadhaa, kwani nilipaswa kumaliza kazi fulani. Baadaye, nilichanganyikiwa kidogo nilipokuwa nikitoa tangazo katika mkutano kwenye Jumba la Ufalme. Nilitoa tangazo tofauti kabisa na lile nililopaswa kutoa! Nilishtuka niliposoma gazeti hilo na kuona matokeo mabaya ya kukosa usingizi. Bila shaka, sasa napaswa kufikiria kwa uzito kuhusu mazoea yangu ya kulala.

T. I., Japani

Ninaugua ugonjwa unaofanya miguu isitulie, ambao ulitajwa katika mfululizo huo. Ijapokuwa nimejitahidi kuchukua hatua za kukabiliana na ugonjwa wangu, ninatumaini ahadi ya Biblia inayopatikana katika kitabu cha Isaya 33:24 inayosema kwamba hivi karibuni “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”

L. O. G., Hispania

Makala yenu haikuwa sahihi kuhusu ugonjwa unaofanya miguu isitulie. Ninaathiriwa sana na ugonjwa huo, na maelezo yenu kuhusu visababishi vya ugonjwa huo hayakuwa sahihi. Ugonjwa huo unahusiana na misuli ya neva.

Y. J., Marekani

“Amkeni!” linajibu: Makala yetu haikutoa maelezo marefu kuhusu mambo yanayosababisha ugonjwa huo. Badala yake ilieleza tu baadhi ya sababu ambazo watafiti wanafikiri zinahusiana na ugonjwa huo. Vyovyote vile, kielezi-chini katika makala yetu kilionyesha kwamba toleo la Novemba 22, 2000, lilizungumzia kwa urefu kuhusu ugonjwa huo. Makala hiyo ilisema hivi: ‘Ingawa wataalamu wanauona ugonjwa wa RLS (yaani ugonjwa wa miguu isiyotulia) kuwa kasoro ya neva, ni vigumu kuwa na uhakika kuhusu chanzo chake.’

Mavazi ya Wamexico Nilisoma kwa hamu sana makala yenye kichwa “Tunapenda Nguo Zetu.” (Februari 8, 2004) Nilifurahi sana nilipotambua kwamba mlieleza kuhusu watu wa kabila la Chontal huko Oaxaca, ijapokuwa idadi yao ni ndogo wanapolinganishwa na makabila yale mengine. Babu yangu na baba ya babu yangu ni wa kabila la Chontal, nami nahisi kwamba makala hiyo iliandikwa kwa staha sana.

A. L., Mexico

Makala kama hizo hutusaidia kufahamu vizuri utamaduni na jamii mbalimbali za watu. Tafadhali endeleeni kuchapisha makala kama hizo kwani kuzisoma hutuwezesha kujifunza kuhusu watu na maeneo tofauti-tofauti ambayo nyakati nyingine hatuwezi kutembelea.

M. L. E., Mexico

Paka wa Mwituni Nina umri wa miaka 13, nami hupenda sana kusoma Amkeni! Niliipenda ile makala yenye kichwa “Paka wa Mwituni.” (Februari 8, 2004) Ninapenda wanyama wote, lakini ninapenda paka hasa. Ninatazamia kwa hamu toleo litakalofuata.

Z. B., Urusi

Mvua Asanteni sana kwa makala yenye kichwa “Yaani Kunanyesha Tena?” (Februari 8, 2004) Kwa muda mrefu nimekuwa nikijiuliza jinsi maji yenye uzito wa mamilioni ya tani yanavyoweza kuelea angani. Amkeni! limejibu swali langu.

G. D., Ufaransa