Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mahakama ya Ulaya Yatetea Haki za Mama Mmoja

Mahakama ya Ulaya Yatetea Haki za Mama Mmoja

Mahakama ya Ulaya Yatetea Haki za Mama Mmoja

Na mwandishi wa Amkeni! nchini Ufaransa

MNAMO Desemba 16, 2003, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu, iliyoko Strasbourg, Ufaransa, ilikata kauli kwamba mahakama za Ufaransa zina hatia ya kumbagua Séraphine Palau-Martínez, ambaye ni Shahidi wa Yehova, kwa msingi wa kidini.

Katika mwaka wa 1996, Séraphine alitalikiana na mume wake, ambaye alikuwa amemwacha miaka miwili mapema. Séraphine alipewa haki ya kuwalea watoto wao wawili. Lakini katika mwaka wa 1997, baada ya watoto hao kuishi na mama yao kwa karibu miaka mitatu na nusu, baba yao alikataa kuwarudisha kwa mama yao walipomtembelea. Séraphine anaeleza hivi: “Nilipoenda kuwachukua watoto kutoka shuleni, mkuu wa shule aliwaita polisi. Niliruhusiwa tu kuwaona watoto wangu polisi wakiwapo ili kuhakikisha kwamba siwaelezi lolote kuhusu imani yangu. Nilikuwa kama mhalifu. Niliambiwa kwamba ningewachukua watoto wangu ikiwa tu ningetia sahihi hati iliyosema kwamba sitawaambia lolote kumhusu Mungu, au kuhusu Biblia, wala kuwapeleka kwenye mikutano ya Kikristo.”

Séraphine aliamua kuwasilisha kesi mahakamani. Hata hivyo, katika mwaka wa 1998, Mahakama ya Rufani ya Nîmes ilimpa baba haki ya kulea watoto. Ilitetea uamuzi wake kwa kuchambua vikali mafundisho ambayo Mashahidi wa Yehova huwapa watoto wao. Séraphine anakumbuka hivi: “Nilihuzunika sana niliposhtakiwa kwa kuwadhuru watoto wangu, kwa kuwa niliona kwamba nilikuwa nikiwapa mafunzo bora kabisa, yaani, kuwalea wawe Wakristo.”

Wakati mahakama kuu ya rufani ya Ufaransa ilipounga mkono uamuzi wa mahakama ya rufani, Séraphine aliamua kuwasilisha kesi hiyo mbele ya Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu. Katika uamuzi wake ulioungwa mkono na mahakimu 6 kati ya 7, mahakama hiyo ilisema hivi: “Kwa maoni ya Mahakama hii, hakuna shaka lolote kuwa uamuzi wa mahakama ya rufani [ya Ufaransa] ulimpendelea mzazi mmoja dhidi ya mwingine kwa sababu za kidini. . . . Huo ni ubaguzi.” Mahakama hiyo ilikata kauli kwamba uamuzi wa mahakama ya Ufaransa haukutilia maanani ikiwa Séraphine anaweza kuwatunza watoto wake, wala haukutegemea uthibitisho hususa bali ulitegemea “maoni ya jumla kuhusu Mashahidi wa Yehova.” Kutokana na ubaguzi huo wa kidini na kuvunjwa kwa haki za kibinadamu za Séraphine, Mahakama hiyo iliagiza Ufaransa ilipe ridhaa na gharama za mahakama.

Mnamo Juni 1993, katika kesi kama hiyo, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu ilikata kauli kwamba Austria ilikuwa imembagua Ingrid Hoffmann, ambaye ni Shahidi wa Yehova, kwa msingi wa dini yake. * Gazeti la Ufaransa la habari za sheria La Semaine juridique lilisema hivi kuhusu uamuzi uliofanywa katika kesi ya Séraphine: “Kupatana na uamuzi uliofanywa katika kesi ya Hoffmann, uamuzi huu unathibitisha kwamba haifai kufanya maamuzi kuhusu haki za wazazi kwa msingi wa kidini tu.” Wakili wa Séraphine alisema hivi: “Uamuzi huu ni muhimu sana, kwa kuwa unapatana na maamuzi mengine ambayo Mahakama hiyo imewahi kufanya kuhakikisha kwamba wazazi ambao ni Mashahidi wa Yehova wana haki ya kutobaguliwa mahakamani.”

Séraphine, ambaye sasa anaishi nchini Hispania, alipoulizwa jinsi alivyohisi kuhusu uamuzi huo alisema: “Nimefurahi sana, na wasiwasi wangu umetoweka. Nilihuzunika sana niliponyang’anywa watoto wangu kwa sababu ya dini yangu na ilikuwa vigumu sana kuishi bila kuwaona kwa miaka mitano, lakini Yehova amenitegemeza sikuzote. Natumaini kwamba uamuzi huo utawasaidia wengine wanaokabili tatizo kama langu.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ona makala yenye kichwa “Mashahidi wa Yehova Watetewa Katika Vita ya Kutunza Watoto,” katika Amkeni! la Oktoba 8, 1993, ukurasa wa 15.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Séraphine