Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nifanyeje Nisipofanikiwa?

Nifanyeje Nisipofanikiwa?

Vijana Huuliza . . .

Nifanyeje Nisipofanikiwa?

“Nimetoka tu kupokea ripoti yangu na kwa mara nyingine nimeanguka masomo yaleyale manne. Nilijaribu lakini nimeanguka tena.”—Lauren, miaka 15.

“Ni vigumu kuvumilia baada ya kushindwa kufanya jambo ambalo ulitaka. Ni rahisi kujiona kuwa hufai.”—Jessica, miaka 19.

KUTOFANIKIWA. Huenda hata hupendi kusikia neno hilo. Lakini mara kwa mara sisi hushindwa kutimiza tunayotaka. Tunaweza kuhuzunika tunapoanguka mtihani wa shule, tunaposema au kufanya jambo lenye kuaibisha, tunapomvunja moyo mtu tunayempenda, au tunapofanya dhambi.

Bila shaka, wanadamu wote hukosea. Biblia inasema: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Lakini baadhi yetu hushindwa kurekebisha hali baada ya kukosea. Kijana mmoja anayeitwa Jason alisema hivi: “Mimi hujichambua sana. Ninapokosea, watu wanaweza kunicheka, lakini baada ya muda wao husahau. Hata hivyo mimi sisahau, badala yake mimi huendelea tu kufikiria kosa langu.”

Hakuna ubaya wowote kufikiria makosa ambayo umefanya, hasa ikiwa kufanya hivyo kutakuchochea ufanye maendeleo. Hata hivyo, unaweza kuumia unapoendelea kujichambua kwa muda mrefu. Methali 12:25 inasema: “Hangaiko katika moyo wa mtu huufanya uiname.”

Mfikirie Epafrodito anayetajwa katika Biblia. Alitumwa Roma akamsaidie mtume Paulo. Hata hivyo, Epafrodito akawa mgonjwa na kushindwa kutimiza mgawo huo. Ikambidi Paulo amtunze. Paulo alipanga Epafrodito arudi nyumbani naye akaliambia kutaniko la kwao kuwa mwanamume huyo mwaminifu alikuwa amehuzunika. Kwa nini? “Mlisikia alikuwa mgonjwa,” Paulo akaeleza. (Wafilipi 2:25, 26) Epafrodito alipojua kwamba wengine walifahamu alikuwa mgonjwa na hangeweza kutimiza migawo yake, alijihisi kuwa hafai. Si ajabu kwamba alivunjika moyo.

Je, kuna njia yoyote ya kuepuka huzuni inayotokana na kutofanikiwa?

Fahamu Kupungukiwa Kwako

Njia moja ya kuepuka kutofanikiwa ni kujiwekea miradi unayoweza kutimiza. Biblia inasema: “Wenye kiasi wana hekima.” (Methali 11:2; 16:18) Mtu mwenye kiasi hutambua kupungukiwa kwake. Ni kweli kwamba ni vizuri kujijaribu mara kwa mara uone ni nini unachoweza kutimiza, ili uweze kuboresha ustadi na uwezo wako. Lakini jiwekee miradi unayoweza kutimiza. Huenda usiwe stadi katika hesabu au usiwe na uwezo kama wa mchezaji hodari. Kijana mmoja anayeitwa Michael anasema hivi: “Ninajua kwamba mimi si mchezaji hodari. Kwa hiyo mimi hucheza lakini sijihusishi katika michezo ambayo ninajua siwezi kucheza vizuri.” Michael anaeleza: “Lazima ujiwekee miradi ambayo unaweza kutimiza.”

Ebu fikiria mtazamo wa Yvonne mwenye umri wa miaka 14, ambaye uti wake wa mgongo umejipinda na ana ugonjwa wa kupooza ubongo. Yvonne anasema: “Siwezi kutembea au kucheza dansi au kukimbia kama wengine. Mimi huvunjika moyo kwa sababu siwezi kufanya yale ambayo wengine hufanya. Wengi hawaelewi kwa nini mimi huvunjika moyo. Lakini mimi huvumilia tu hisia hizo.” Yeye anashauri hivi: “Usiache kamwe kujaribu. Usipofanikiwa kutimiza lengo lako, usikate tamaa. Endelea tu kufanya kadiri ya uwezo wako.”

Wakati huohuo, usijiumize kwa kujilinganisha na wengine isivyofaa. Andrew, mwenye umri wa miaka 15, anasema, “Mimi hujaribu kuepuka kujilinganisha na wengine kwa sababu sisi sote tuna uwezo na ustadi mbalimbali.” Maneno hayo ya Andrew yanapatana na yale ya Biblia kwenye Wagalatia 6:4: “Kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mtu yule mwingine.”

Wengine Wanapotazamia Utimize Mengi Mno

Nyakati nyingine, wazazi, walimu, na watu wengine wanaweza kutazamia utimize mengi mno. Na huenda ukajua kwamba hata ukijaribu jinsi gani, huwezi kuwapendeza. Wanaweza kukuvunja moyo kabisa kupitia maneno yenye kuumiza. (Ayubu 19:2) Lakini, bila shaka unatambua kwamba wazazi wako na wengine hawataki kukuhuzunisha kimakusudi. Kama vile Jessica anavyosema, “mara nyingi hata hawafahamu kwamba wanakuhuzunisha. Nyakati nyingine labda tu hawaelewi hali.”

Kwa upande mwingine, je, wanaona jambo fulani ambalo wewe huoni? Kwa mfano, labda hufanyi mambo kwa kadiri ya uwezo wako au unajidharau. Badala ya kupuuza maoni yao, ni jambo la hekima ‘kusikiliza nidhamu.’ (Methali 8:33) Michael anasema: “Ni kwa faida yako. Wao wangependa ufanye vizuri zaidi, uboreshe uwezo wako. Acha jambo hilo likuchochee kutenda.”

Vipi ukihisi kwamba wazazi wako na watu wengine wanakutazamia ufanye mengi kuliko uwezavyo, na kwamba hutafanikiwa? Basi ingefaa uwaeleze kwa heshima na waziwazi jinsi unavyohisi. Mkiwasiliana, mtaweza kuweka miradi ambayo unaweza kutimiza.

Kutofanikiwa Kiroho

Vijana ambao ni Mashahidi wa Yehova wanakabili hali ngumu wanapojitahidi kutimiza migawo yao wakiwa watumishi wa Mungu. (2 Timotheo 4:5) Ikiwa wewe ni kijana Mkristo, nyakati nyingine unaweza kuhisi kuwa hufai. Labda unahisi kwamba hutoi maelezo yanayofaa mikutanoni. Au labda wewe huona ni vigumu kuwahubiria wengine. Kwa mfano, Jessica alijifunza Biblia na msichana fulani. Msichana huyo alifanya maendeleo mazuri kwa muda fulani. Lakini punde si punde, msichana huyo akaamua kwamba hataki kumtumikia Mungu. Jessica anakumbuka, “Nilihisi kwamba mimi si mwalimu mzuri.”

Jessica angewezaje kuvumilia hisia kama hizo? Kwanza alihitaji kufahamu kwamba mwanafunzi wake amemkataa Mungu, wala si yeye. Pia alisaidiwa kwa kutafakari kuhusu mfano wa Petro unaopatikana katika Biblia. Petro alimcha-Mungu, lakini alikuwa na udhaifu mbalimbali. Jessica anaeleza hivi: “Biblia inaonyesha kwamba Petro alishinda udhaifu wake, naye alitumiwa na Yehova katika njia nyingi kuendeleza kazi za Ufalme.” (Luka 22:31-34, 60-62) Bila shaka, ikiwa unahitaji kuboresha uwezo wako wa kufundisha, jitahidi kufanya hivyo. (1 Timotheo 4:13) Omba Wakristo wakomavu wanaoweza kukufundisha na kukuzoeza wakusaidie.

Huenda ukaona ni vigumu sana kuhubiri nyumba kwa nyumba. Jason anasema hivi: “Mwenye nyumba anapokataa kusikiliza mimi huhisi kwamba sijafanikiwa.” Yeye hukabilianaje na hisia hizo? “Mimi hukumbuka kwamba hilo halionyeshi kuwa sijafanikiwa.” Ndiyo, yeye amefaulu kufanya kile ambacho Mungu ameamuru afanye, yaani, kuhubiri! Kwa kweli, ingawa si rahisi kuvumilia upinzani, si watu wote watakaopinga ujumbe wa Biblia. Jason anasema, “Ninapompata mtu ambaye anasikiliza, mimi hutambua kwamba jitihada zangu hazikuwa za bure.”

Makosa Mazito

Vipi ukifanya kosa au dhambi nzito? Ana, mwenye umri wa miaka 19, alifanya kosa kama hilo. * Yeye anakiri hivi, “Niliaibisha kutaniko, familia yetu, na hasa Yehova Mungu.” Unahitaji kutubu na kutafuta msaada wa wazee Wakristo katika kutaniko ili urudie hali yako. (Yakobo 5:14-16) Ana anakumbuka maneno ya mzee mmoja yaliyomsaidia: “Alinieleza kwamba haidhuru Mfalme Daudi alifanya makosa mengi kadiri gani, bado Yehova alikuwa tayari kumsamehe, naye Daudi alirudia hali yake. Maneno hayo yalinisaidia.” (2 Samweli 12:9, 13; Zaburi 32:5) Pia unahitaji kujitahidi kujiimarisha kiroho. Ana anasema, “Mimi hurudia kusoma kitabu cha Zaburi mara nyingi, nami nina kitabu cha kuandika maandiko yenye kutia moyo.” Kadiri muda unavyopita, mtu aliyefanya dhambi nzito anaweza kurudia hali yake. Methali 24:16 inasema: “Huenda mwadilifu akaanguka hata mara saba, naye hakika atasimama.”

Kufanya Maendeleo Baada ya Kukosea

Bila shaka hata makosa madogo yanaweza kuumiza hisia zako. Ni nini kitakachoweza kukusaidia ufanye maendeleo? Kwanza kabisa, kabiliana na makosa yako kulingana na uwezo wako. Michael anapendekeza: “Badala tu ya kujiona kuwa hufai, tambua ni jambo gani hasa ambalo hukufanya vizuri na sababu ya kutofanikiwa. Kwa njia hiyo unaweza kufanya vema zaidi wakati ujao.”

Epuka kujiona kuwa wa maana sana. Kuna “wakati wa kucheka,” na hilo linamaanisha pia kujicheka. (Mhubiri 3:4) Ukihisi kwamba umevunjika moyo, fanya jambo ambalo kwa kawaida huwa linakufurahisha, kama vile kucheza mchezo fulani. Kuwa ‘tajiri katika matendo mazuri’ kama vile kuwahubiria wengine, kunaweza kukusaidia ujiamini.—1 Timotheo 6:18.

Mwishowe, kumbuka kwamba “Yehova ni mwenye rehema na mwenye neema . . . Yeye hataendelea kutafuta makosa wakati wote.” (Zaburi 103:8, 9) Jessica anasema hivi: “Ninahisi kwamba kadiri ninavyozidi kumkaribia Yehova Mungu, ndivyo ninavyozidi kuwa na uhakika kwamba atanitegemeza na kunisaidia katika yale yote yatakayonipata.” Ndiyo, inafariji kama nini kujua kwamba Baba yako wa mbinguni anakuthamini, haidhuru makosa unayofanya.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 23 Jina lake limebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Ukihisi kwamba matarajio ya wengine yanakulemea, waeleze jambo hilo kwa heshima

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kufanya mambo ambayo wewe hufanya vizuri kunaweza kukusaidia kuepuka huzuni ya kutofanikiwa