Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

UKIMWI Utakwisha Lini?

UKIMWI Utakwisha Lini?

UKIMWI Utakwisha Lini?

Tangu wakiwa wachanga, vijana huathiriwa na habari nyingi kuhusu ngono ambazo huwashawishi kuishi maisha mapotovu. Watu wengi hujidunga sindano za dawa za kulevya ambazo pia hueneza sana virusi vya UKIMWI. Kwa kuwa kuna upotovu mwingi ulimwenguni na maoni ya kutojali, huenda ukajiuliza ikiwa UKIMWI utakwisha.

KWA kufaa, wataalamu wa afya wanasema kwamba mabadiliko katika tabia za watu ni njia muhimu ya kupambana na UKIMWI. Ripoti moja iliyochapishwa na Vituo vya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa ilisema kwamba “kila kizazi cha vijana kinahitaji kuendelea kuelimishwa sana kuhusu afya na kusaidiwa kujua jinsi ya kuepuka tabia zinazoweza kusababisha waambukizwe virusi vya UKIMWI. Wazazi na walimu wanapaswa kuhusishwa katika miradi hiyo ya kuwaelimisha vijana.”

Kwa wazi, wazazi wanahitaji kuwaelimisha watoto wao kuhusu hatari hizo kabla hawajapotoshwa na marafiki zao. Hilo si jambo rahisi, lakini linaweza kuokoa uhai wa mtoto wako. Huwezi kuwaharibu watoto wako kwa kuwafahamisha kuhusu ngono na matumizi ya dawa za kulevya. Kuwafahamisha mambo hayo kunaweza kuwazuia wasiharibike.

Ni Muhimu Wazazi Wawazoeze Watoto Wao

Wazazi waliomwabudu Mungu nyakati za kale walipaswa kuwafundisha watoto wao kuhusu ngono na jinsi wanavyoweza kutunza afya yao. Kwa kupendeza, sheria ambazo Waisraeli wa kale walipewa zilitia ndani miongozo hususa ya kiadili na vilevile mazoea ambayo walipaswa kuepuka ili wasipatwe na maambukizo. (Mambo ya Walawi 18:22, 23; 19:29; Kumbukumbu la Torati 23:12, 13) Watu wangefundishwaje sheria hizo? Yehova Mungu aliwaambia Waisraeli hivi: “Maneno haya ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako.” Kwanza, wazazi walipaswa kuelewa faida za kufuata sheria hizo na madhara ya kutozifuata. Kisha wakaagizwa hivi: “Uyakazie kwa mwana wako na kuyasema unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.”—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.

Neno la Kiebrania linalotafsiriwa ‘kazia’ linamaanisha “kurudia,” “kusema tena na tena,” au “kuingiza.” Bila shaka, wakati unahitajiwa ili kufanya hivyo. Wazazi wanaotenga wakati ili kuwafundisha wana na binti zao kuhusu hatari za matumizi ya dawa za kulevya na ngono haramu, wanaweza kufurahia kuwaona watoto wao wakiepuka tabia zinazoweza kuwafanya waambukizwe virusi vya UKIMWI na magonjwa mengine. *

Faraja kwa Wagonjwa wa UKIMWI

Jitihada za kuzuia UKIMWI haziwafariji sana mamilioni ya watu wenye virusi vya UKIMWI. Zaidi ya athari za kimwili wanazopata, mara nyingi wao hudharauliwa na kuepukwa. Jinsi gani? Watu wengi hufikiri kimakosa kwamba mtu anaweza kuambukizwa virusi vya UKIMWI kwa kumgusa mgonjwa. Tunaweza kuelewa sababu za watu kuogopa kupata UKIMWI, kwani huo ni ugonjwa wa kuambukiza na wa kufisha. Kwa sababu ya kuhofia kupata ugonjwa huo, watu fulani huwaogopa sana wale walio na virusi vya UKIMWI. Wagonjwa wa UKIMWI wamenyimwa matibabu, wamefukuzwa makanisani, na hata kushambuliwa kijeuri.

Watu fulani wamedai kwamba UKIMWI ni laana ya Mungu kwa waovu. Ni kweli kwamba kufuata viwango vya Biblia kuhusu ngono, dawa za kulevya, na damu kungewazuia watu wengi wasiambukizwe ugonjwa huo. (Matendo 15:28, 29; 2 Wakorintho 7:1) Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba Mungu hawaletei watu magonjwa ili kuwaadhibu kwa sababu ya dhambi fulani. Badala yake, Biblia husema hivi: “Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (Yakobo 1:13; Yohana 9:1-3) Mtu aliyeambukizwa UKIMWI kwa sababu ya kutotii viwango vya Biblia kisha akabadili mwenendo wake, anaweza kuwa na hakika kwamba Mungu hajamwacha.

Mwana wa Mungu, Yesu, alipokuja duniani, alionyesha wazi huruma na upendo wa Mungu kwa ajili ya wagonjwa mahututi. Wakati mmoja Yesu alipokutana na mtu mwenye ukoma, ‘alimsikitikia, naye akanyoosha mkono wake akamgusa.’ Yesu alitumia nguvu zake za kufanya miujiza kumponya mtu huyo mwenye ukoma. (Marko 1:40-42) Yesu hakuwadharau wagonjwa. Upendo wake kwao ulionyesha kikamili upendo wa Baba yake wa mbinguni.—Luka 10:22.

UKIMWI Utakomeshwa Karibuni!

Mbali na kutuhakikishia kwamba Mungu anatupenda, maponyo ya kimuujiza ya Yesu hutuhakikishia mengi zaidi. Biblia inatueleza kwamba sasa Yesu Kristo anatawala akiwa Mfalme mbinguni. (Ufunuo 11:15) Huduma yake alipokuwa duniani ilionyesha kwamba ana uwezo na nia ya kuponya magonjwa yote yanayowakumba wanadamu. Atafanya vivyo hivyo.

Unabii wa Biblia unatuhakikishia kwamba hivi karibuni “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24) Ijapokuwa wanadamu wameshindwa kuzuia UKIMWI usienee na kushindwa kuwawezesha wagonjwa wote kupata matibabu yanayofaa, tunaweza kuwa na hakika kwamba UKIMWI utakomeshwa. Mfalme Daudi alisema hivi: “Mbariki Yehova, Ee nafsi yangu, wala usiyasahau matendo yake yote, Yeye anayesamehe makosa yako yote, anayeponya magonjwa yako yote.”Zaburi 103:2, 3.

Hayo yatatukia lini? Mungu anataka watu wafanye nini ili wapate baraka hizo? Tunakuomba uwasiliane na Mashahidi wa Yehova ili ujifunze mengi zaidi kuhusu ahadi hizo za ajabu za Biblia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Wazazi wengi wameona kwamba kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, ni kifaa muhimu cha kuwafundisha watoto wachanga hatua kwa hatua kuhusu ngono na kanuni za msingi za maadili.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Unabii wa Biblia unatuhakikishia kwamba hivi karibuni “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa’”

[Picha katika ukurasa wa 10]

Watoto wako wanaweza kuepuka matatizo ukiwafundisha kuhusu ngono na dawa za kulevya

[Picha katika ukurasa wa 10]

Uwezo na nia ya Yesu ya kuwaponya wagonjwa ilionyesha yale atakayofanya wakati ujao