Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuepuka Hatari za Intaneti

Jinsi ya Kuepuka Hatari za Intaneti

Maoni ya Biblia

Jinsi ya Kuepuka Hatari za Intaneti

MKULIMA katika kijiji cha mashambani huko India, anachunguza bei ya maharagwe katika soko la Chicago, Marekani, ili kuamua wakati unaofaa zaidi wa kuuza mazao yake. Wakati huohuo, mwanamke mmoja aliyestaafu anatabasamu anaposoma barua-pepe kutoka kwa mjukuu wake, msafiri fulani anachunguza hali ya hewa ya mahali anapoelekea, na mama mmoja anatafuta habari ambayo binti yake anahitaji kwa ajili ya kazi za shule. Mambo hayo yote yanafanywa kwa kutumia Intaneti. Inakadiriwa kwamba watu milioni 600 ulimwenguni pote wanatumia Intaneti, na hilo limebadilisha kabisa njia za watu za kuwasiliana na kufanya biashara ulimwenguni pote.

Vijana, ambao wameitwa “Kizazi cha Kompyuta,” ndio hasa wanaotumia Intaneti. Badala ya vitabu, wanafunzi wengi zaidi hutumia Intaneti kutafuta habari na kufanya utafiti. Deanna L. Tillisch, msimamizi wa uchunguzi mmoja kuhusu wanafunzi wa vyuo nchini Marekani, anasema hivi: “Kwa ufupi, wanafunzi hawa . . . hutumia Intaneti katika shughuli zao zote za kujifunza.” Bila shaka, Intaneti ni chombo muhimu sana leo.

Kwa kawaida, mashine yenye uwezo mkubwa huwa hatari. Msumeno unaozungushwa kwa petroli unaweza kutimiza mengi kuliko msumeno wa kawaida, hata hivyo, mtu anahitaji kuwa mwangalifu sana anapoutumia. Ndivyo ilivyo na Intaneti. Ijapokuwa ni mashine yenye uwezo mkubwa ambayo hutuwezesha kufanya mengi, tunahitaji kuitumia kwa uangalifu kwani inaweza kuwa hatari sana. Hangaiko kuhusu hatari za kutumia Intaneti limefanya zaidi ya mataifa 40 yaliyo wanachama wa Baraza la Ulaya kuanzisha mswada wa kimataifa ambao umekusudiwa kulinda jamii dhidi ya uhalifu unaofanywa kwa kutumia Intaneti.

Kwa nini watu wanahangaishwa sana na jambo hilo? Mkristo anakabili hatari gani? Je, hilo lapaswa kukufanya uache kutumia Intaneti? Biblia hutoa mwongozo gani kuhusu jambo hilo?

Unahitaji Kuwa Mwangalifu

Karne kadhaa zilizopita, Biblia ilionya juu ya hatari ambazo zingetokana na watu waovu walio ‘mafundi wa mawazo ya uovu’ na ambao ‘hupanga hila ya kufanya ubaya.’ (Methali 24:8) Nabii Yeremia alisema kwamba wao ni “watu waovu” na ‘nyumba zao zimejaa udanganyifu.’ Kama wawindaji wa ndege, “wameweka mtego wenye kuharibu” ili kuwanasa watu na ‘kupata utajiri.’ (Yeremia 5:26, 27) Tekinolojia imewawezesha “watu waovu” wa leo kutega mitego ya hila ya aina mpya kabisa. Hebu tuchunguze baadhi ya mitego iliyo hatari sana kwa Mkristo.

Ponografia katika Intaneti ni biashara inayochuma dola bilioni 2.5 kwa mwaka. Idadi ya vituo vya ponografia katika Intaneti imeongezeka kwa asilimia 1,800 hivi kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita, na hilo ni ongezeko la haraka sana. Inakadiriwa kwamba kuna vituo zaidi ya milioni 260 vya aina hiyo, na kwamba idadi hiyo inaendelea kuongezeka haraka sana. Msimamizi wa kituo kimoja kinachoshughulikia watu walio na tatizo la kuzoea kutumia Intaneti, Dakt. Kimberly S. Young, anasema hivi: “Ponografia imeenea sana katika Intaneti hivi kwamba imekuwa vigumu kuiepuka, na hilo linafanya iwe rahisi sana kusitawisha mazoea ya kutazama ngono kwenye kompyuta.”

Biblia husema kwamba “kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe.” (Yakobo 1:14) Kwa kuwa watu wanaoeneza ponografia hufikiri kwamba itamvutia kila mtu aliye na kompyuta, wao hutumia mbinu mbalimbali ili kuchochea ‘tamaa ya mtu mwenyewe,’ yaani, “tamaa ya mwili na tamaa ya macho.” (1 Yohana 2:16) Nia yao ni kuwavutia watu wasio na habari ambao hutumia Intaneti, na ‘kujaribu kuwashawishi.’— Methali 1:10.

Kama vile watu waovu walioishi nyakati za Biblia, mara nyingi wale wanaoeneza ponografia hutumia udanganyifu. Inakadiriwa kwamba barua-pepe bilioni mbili hivi za ponografia hutumwa kila siku, ili kuvutia wateja wapya. Barua hizo hutumwa kwa watu wasiozitarajia, na kwa kawaida huwa na vichwa vya habari ambavyo havionekani kuwa na ubaya wowote. Hata hivyo, ukifungua barua moja ya aina hiyo unaweza kupata mfululizo wa picha chafu ambao si rahisi kuukomesha. Ukiomba usitumiwe tena habari hizo chafu, huenda ukapokea bila kutarajia ujumbe mwingine mwingi wa ponografia.

Mtu anayewinda ndege huangusha mbegu kwenye kijia kwa uangalifu. Ndege asiyetazamia hula mbegu hizo moja baada ya nyingine hadi mtego unapofyatuka na kumnasa. Udadisi unaweza kufanya watu fulani waanze kuvutiwa pole kwa pole na picha zinazoamsha hamu ya ngono. Wao huzitazama wakifikiri kwamba hawaonekani. Kwa kuwa hamu yao ya ngono huchochewa, baadhi yao hutazama picha hizo zaidi na zaidi. Huenda wakaaibika na kuhisi wana hatia. Muda si muda, wao huanza kuona mambo waliyokuwa wakichukia kuwa ya kawaida tu. Intaneti huchochea upesi sana tamaa ya watu ambao hupenda kutazama ponografia na hilo huwafanya watende dhambi. (Yakobo 1:15) Dakt. Victor Cline, mtaalamu ambaye ametibu mamia ya watu ambao walikuwa na tatizo la kutazama ponografia anasema kwamba hatimaye watu hao husitawisha “‘tabia mbovu’ ya kutaka kujitosheleza kingono bila kujali kanuni zinazofaa.”

Hatari za Vituo vya Maongezi

Mazungumzo kwenye vituo vya Intaneti hupoteza wakati mwingi sana, na kusababisha familia nyingi zivunjike. Mwanamume mmoja aliandika hivi kuhusu kiasi cha wakati ambacho mke wake hutumia kwenye kompyuta: “Mara tu anapofika nyumbani kutoka kazini, yeye huwasha kompyuta na anaweza kuitumia kwa saa tano au zaidi. Hilo limeathiri sana ndoa yetu.” Naam, kutumia Intaneti hukuzuia usifanye mambo na familia yako.

Angela Sibson, ambaye ni mshauri mkuu katika shirika moja la kutoa mashauri ya ndoa linaloitwa Relate, anasema kwamba Intaneti ni “njia ya kuanzisha uhusiano na watu wengine. Uhusiano huo unaweza kuimarika sana na kuvunja uhusiano mwingine wowote ambao mtu alikuwa nao mbeleni.” Mazungumzo ya kirafiki katika kituo cha mazungumzo cha Intaneti yanaweza kubadilika haraka na kuwa hatari. Wakiwa na nia ya kufanya matendo ya ukosefu wa adili, watu walio na “ujanja wa moyo” hutumia “ulimi laini” kuwaambia watu wengine mambo yanayowavutia. (Methali 6:24; 7:10) Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 26 anayeitwa Nicola, ambaye anaishi Uingereza, alidanganywa wakati mmoja kwenye Intaneti. Anasema hivi: “Aliniambia mara nyingi kwamba ananipenda. Alirudia-rudia kuniambia jinsi nilivyokuwa mrembo, nami nikadanganyika.” Dakt. Al Cooper, ambaye ni mwandishi wa kitabu Sex and the Internet: A Guidebook for Clinicians, anasema kwamba tunahitaji “kuwatahadharisha watu kuhusu hatari ya mzaha wa kimahaba unaoanzishwa katika kituo cha Intaneti na ambao mara nyingi husababisha talaka.”

Watoto hasa ndio wanaokabili hatari kubwa zaidi ya kudhulumiwa na “wahalifu wa ngono wanaotumia kompyuta.” Watu ambao hufanya ngono na watoto hutumia “maneno yaliyopotoka” na “hila ya midomo” kuwashawishi watoto wasio na ujuzi. (Methali 4:24; 7:7) Wao huwatayarisha watoto kwa ajili ya matendo machafu kwa kuwaelekezea sana fikira, kuwaonyesha upendo na fadhili nyingi, na hivyo kumfanya mtoto ajihisi kuwa ni wa maana sana. Ni kana kwamba wanajua mambo yanayompendeza mtoto, kutia ndani muziki na mambo anayofurahia kufanya. Wao hukazia sana matatizo madogo ambayo mtoto hukabili nyumbani na hivyo kumfanya aichukie familia yao. Ili watosheleze tamaa yao mbaya, watu hao wanaweza kuwatumia watoto tiketi za kusafiri. Matokeo huwa mabaya sana.

Kanuni za Biblia Zinaweza Kukulinda

Baada ya kufikiria hatari zinazohusika, watu fulani wameamua kuacha kabisa kutumia Intaneti. Hata hivyo, ni kweli kwamba vituo vya Intaneti vilivyo hatari ni vichache tu, na watu wengi wanaotumia Intaneti hawajakabili hatari kubwa.

Lakini, Biblia hutupa mwongozo ‘unaotulinda’ kutokana na hatari. Tunatiwa moyo tujipatie ujuzi, hekima, na uwezo wa kufikiri. Sifa hizo ‘zitatutunza’ na ‘kutukomboa kutoka katika njia mbaya.’ (Methali 2:10-12) Ayubu aliyemtumikia Mungu zamani aliuliza hivi: “Lakini hekima—hiyo inatoka wapi?” Jibu la swali hilo ni nini? “Kumwogopa Yehova—hiyo ndiyo hekima.”—Ayubu 28:20, 28.

“Kumwogopa Yehova,” ambako “humaanisha kuchukia yaliyo mabaya,” kutatuwezesha kusitawisha sifa zinazompendeza Mungu. (Methali 1:7; 8:13; 9:10) Ikiwa tunampenda Mungu na kumstahi, na vilevile tunaheshimu uwezo na mamlaka yake, tutachukia na kuepuka mambo mabaya ambayo yeye huchukia. Uwezo wa kufikiri vizuri na ujuzi sahihi kuhusu kanuni za Mungu, hutusaidia kutambua mambo hatari yanayoweza kuchafua akili na mioyo yetu, na kuharibu hali yetu ya kiroho. Hilo hutufanya tuchukie ubinafsi na pupa kwani mambo hayo yanaweza kuvunja familia zetu na kuharibu uhusiano wetu na Yehova.

Kwa hiyo, ikiwa unatumia Intaneti, tambua hatari zinazohusika. Azimia kutii amri za Mungu, na uepuke kuvutiwa na chochote kile ambacho kinaweza kukuhatarisha. (1 Mambo ya Nyakati 28:7) Hivyo, iwapo utakabili hatari za Intaneti utaweza kuzikimbia.—1 Wakorintho 6:18.

[Sanduku katika ukurasa wa 19]

EPUKA PONOGRAFIA!

“Uasherati na ukosefu wa usafi wa kila namna au pupa visitajwe hata kidogo katikati yenu, kama inavyowafaa watu watakatifu.”—Waefeso 5:3.

“Kwa hiyo, viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani.”—Wakolosai 3:5.

“Kwa maana haya ndiyo mapenzi ya Mungu, . . . kwamba kila mmoja wenu ajue jinsi ya kukiweza chombo chake mwenyewe katika utakaso na heshima, si katika hamu yenye tamaa ya ngono kama ile waliyo nayo pia mataifa wale wasiomjua Mungu.”—1 Wathesalonike 4:3-5.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Jihadhari na Vituo vya Maongezi vya Intaneti!

Mwanamke mmoja ambaye ni polisi wa upelelezi anayeshughulikia uhalifu katika Intaneti alimkaribisha mwandishi wa Amkeni! aone hatari zilizopo katika vituo vya maongezi kwenye Intaneti. Alifungua kituo kimoja na kujifanya eti yeye ni msichana mwenye umri wa miaka 14. Baada ya sekunde chache tu, watu kadhaa walikiandikia kituo hicho. Watu hao waliuliza maswali kama vile: “Unatoka wapi?” “Wewe ni msichana au mvulana?” “Je, tunaweza kuzungumza?” Majibu fulani yalitoka kwa washukiwa kadhaa wa uhalifu wa ngono waliokuwa wakitafutwa na polisi. Hiyo inaonyesha jinsi ilivyo rahisi kwa watu wanaofanya ngono na watoto kuanza mazungumzo na mtoto wako katika kituo cha Intaneti!

Wazazi fulani hudhani kwamba watoto wao wako salama wanapowasiliana katika vituo hivyo vya maongezi eti kwa sababu watu wote wanaotumia kituo hicho wanaweza kuona mambo yanayoandikwa wakati mazungumzo yanapoendelea. Hata hivyo, baada ya kuanza kuwasiliana katika kituo hicho unaweza kukaribishwa uwe na mazungumzo ya watu wawili pekee. Tume ya Intaneti ya Kuwalinda Watoto ya Uingereza inaonya hivi kuhusu zoea hilo: “Unapofanya hivyo ni kama unajitenga na watu kwenye karamu na kuingia katika chumba cha faragha ili uzungumze na mtu usiyemjua.”

Ni muhimu pia kwa wazazi kuelewa kwamba kusudi la watu wanaofanya ngono na watoto si kuzungumza na mtoto tu. Hati iliyotayarishwa na Internet Crime Forum iliripoti hivi: “Baada ya kuwasiliana katika kituo cha maongezi, watu wanaofanya ngono na watoto wanaweza kuendeleza uhusiano na mtoto kupitia njia nyingine za mawasiliano, kama vile barua-pepe na simu (za mkononi).” Ripoti ya Shirika la Ujasusi la Marekani inasema hivi: “Ingawa mhalifu wa ngono anayetumia kompyuta hufurahia kuzungumza na mtoto, huenda akakabili matatizo mbalimbali. Wengi hupenda kumpigia mtoto simu. Wao hupenda kuzungumza na watoto juu ya ngono kupitia simu, nao hujitahidi kupanga wakati ambapo watakutana ili kufanya ngono.”

Ili kutimiza jambo hili, kwa kawaida mhalifu wa ngono anayetumia kompyuta atampatia mtoto namba yake ya simu. Iwapo mtoto wako atampigia simu, mhalifu huyo atatambua namba ya simu ya mtoto. Wahalifu fulani wana namba ambazo hazitozwi chochote au wanaweza kumwambia mtoto apige simu kwa njia ambayo gharama italipwa na anayepigiwa. Wengine hata wamewanunulia watoto simu za mkononi. Pia, wahalifu wanaweza kuwatumia watoto barua, picha, na zawadi.

Sio watoto peke yao wanaoathiriwa. Hivi karibuni, mwanamume mmoja alitumia usemi laini kuwabembeleza wanawake sita huko Uingereza, naye akafanikiwa kuwavutia wote kwa wakati uleule. Mwanamke mmoja mrembo anayeitwa Cheryl, mwenye umri wa miaka 27, ambaye ni mwanafunzi aliyehitimu katika chuo kikuu, ni mmoja kati ya watu walioathiriwa. Alisema hivi: “Sijui niseme nini. Uhusiano wetu kupitia Intaneti ulikuwa wa ndani sana hivi kwamba uliongoza maisha yangu.”

Jenny Madden mwanzilishi wa Women in Cyberspace alisema hivi: “Wanawake huvutiwa kuwasiliana kupitia Intaneti kwa sababu hakuna anayeangalia sura yao. Lakini hilo hufanya iwe rahisi kwao kutumiwa vibaya kwa sababu watu wanapowasiliana kupitia vituo vya maongezi, wao huwa na mwelekeo wa kufunua siri zao nyingi haraka sana.”

Katika uchunguzi mmoja uliofanywa na Beatriz Avila Mileham wa Chuo Kikuu cha Florida, mwanamume mmoja alisema hivi: “Ninahitaji tu kufungua kompyuta yangu na kupata maelfu ya wanawake ninaoweza kuchagua.” Mileham alisema hivi: “Karibuni Intaneti itakuwa njia kuu ya kuwa na uhusiano wa kingono nje ya ndoa.” Dakt. Al Cooper, mhariri wa kitabu Sex and the Internet: A Guidebook for Clinicians alisema hivi: “Wataalamu nchini kote wanasema kwamba uhusiano wa kingono kupitia kompyuta ni kisababishi kikuu cha matatizo ya ndoa.”

Kwa kufikiria hoja hizo muhimu, ni jambo la hekima kujihadhari tunapotumia Intaneti. Zungumza na watoto wako na uwafundishe jinsi wanavyoweza kujilinda dhidi ya hatari hizo. Ukiwa na ujuzi, unaweza kuepuka hatari za Intaneti.—Mhubiri 7:12.